Na Hafsa Golo
WAJUMBE wa Baraza la Wawakilishi wamesikitishwa na vitendo
vya kutosimamiwa na kutotekelezwa sheria zinazopitishwa na baraza hilo.
Wawakilishi hao walieleza hayo wakati wakichangia mswada wa sheria ya
marekebisho ya sheria ya usafiri wa baharini nambari 5 ya mwaka 2006 katika
kikao cha baraza la wawakilishi kinachoendelea mjini hapa.
Mwakilishi wa Jimbo la Kiwani, Hija Hassan Hija alisema Zanzibar kumekuwa na
sheria nyingi lakini hazisimamiwi ipasavyo jambo ambalo limekuwa likisababisha
kutokea kwa matatizo mengi.
Alisema mswada huo ni muhimu kwa maisha ya watu hivyo ni
lazima sheria isimamiwe ipasavyo ili kuwaondolea majanga wananchi.
“Kila siku tumekuwa tukipitisha sheria lakini usimamiaji wa
sheria ni mbaya na hivyo kuwapa mwanya watu kufanya wanavyotaka jambo ambalo
linasababisha matatizo kwa watu wetu” alisema.
Aidha Hamza Hassan Juma (Kwamtipura), alisema Zanzibar ni nchi
inayoongoza kwa kuwa na sheria nyingi lakini kutokana na usimamizi mbovu wa
sheria hizo ndiko kunasababisha matatizo mbalimbali.
“Zanzibar inaongoza kwa kuwa na sheria nyingi Afrika lakini
usimamiaji na utekelezaji wake ni mbaya na ndio maana kukawa na matatizo
mbalimbali yanayotokea kila siku,” alisema.
Alisema sheria ya usafiri wa baharini ni muhimu kwa maisha
ya wananchi na nchi kwa hivyo ni lazima kuwe na usimamizi madhubuti wa sheria
hiyo.
Nae Mwakilishi wa jimbo la Muyuni, Jaku Hashim Ayoub,
alisema usimamiaji wa sheria bado ni mbovu.
Kwa upande wake Mwakilishi wa nafasi za wanawake, Mgeni
Hassan Juma,alisema bila ya kuwa makini katika utekelezaji wa sheria
nchini,wananchi watakuwa wanaendelea kutumia huduma ya usafiri wa baharini kwa
kubahatisha.
Aidha alisema wakati umefika hivi sasa kuondoa muhali
katika usimamizi wa utekelezaji wa sheria hasa ikizingatiwa kumekuwa na sheria
nyingi zilizopitishwa katika baraza ikiwemo unyanyasaji wa wanyama, lakini
hazitekelezwi.
Nae Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais,
Mohammed Aboud Mohammed, alisema serikali itachukua jitihada kuhakikisha ajali
zilizotokea za meli hazitokei tena na kama zitatokea ziwe za bahati mbaya sana.
Alisema majanga makubwa ya kuzama meli mbili muda mfupi
yameiumiza serikali na wananchi kwa ujumla kwa kupoteza mali na roho za watu jambo ambalo
linapaswa kuangaliwa kwa umakini mkubwa.
Aidha alisema kuwa Mamlaka za Usafiri Baharini za ZMA na
SUMATRA ni lazima zihakikishe zinashirikiana kuhakikisha wanasafiri wanakuwa
salama na mali
zao.
Mapema Makamu
Mwenyekiti wa Kamati ya Mawasiliano na Ujenzi ya Baraza la Wawakilishi, Hassan
Hamad Omar, alisema sekta ya usafiri wa baharini ni lazima ufanyiwe marekebisho kutokana na sekta hiyo
kuchangia mapato ya nchi yanayotokana na uwekezaji.
Waziri wa Miundombinu na Mawasiliano, Rashid Seif Suleiman
alisema lengo la marekebisho ya mswada
huo, ni kuleta mabadiliko katika uendeshaji wa majukumu ya taasisi ya mamlaka
ya usafiri wa baharini na kuweza
kufanyakazi zake kwa ufanisi zaidi na kuondosha changamoto ambazo zingeweza
kuwakwaza kutokana na kutokidhi haja utumiaji wa sheria zilizopo.
Aidha alisema
marekebisho hayo ambayo yatachunguza na
kutilia mkazo zaidi juu ya usalama wa abiria na mabaharia katika vyombo vya
baharini na kuweka msisitizo juu ya
matumizi ya vyombo vyenye ubora na viwango kilingana na sheria za kimataifa za
(IMO).
No comments:
Post a Comment