Habari za Punde

TASAF yatumia 227m/- miradi saba Pemba



Haji Nassor na Ali Khamis, Pemba
ZAIDI ya shilingi 227 milioni, zimetumiwa na Mfuko wa Maendeleo ya Jamii Tanzania (TASAF), ili kufanikisha miradi saba ya maendeleo kwa wananchi mbali mbali kisiwani Pemba, ikiwa ni pamoja na mradi wa ujenzi wa barabara ya Matale- Chambani.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Mratibu wa TASAF kisiwani humo, Issa Juma Ali, kati ya fedha hizo zaidi ya shilingi 78 milioni zimetolewa na wananchi wenyewe katika kuunga nguvu miradi hiyo.

Alisema shilingi 149 milioni zilitolewa na TASAF awamu ya pili, kwa miradi hiyo ambapo baadhi imeshakamilika.
Aliitaja miradi hiyo kuwa ni pamoja na ujenzi wa barabara ya Matale- Chambani yenye urefu wa kilomita 1.3 ambao umegharimu zaidi ya shilingi 44 milioni ambapo fedha zote zilitolewa na TASAF na wananchi kuchangia nguvu kazi.

Mradi mwengine ni upandaji miti uliopo shehia ya Chumbageni wilaya ya Mkoani ambao umegharimu shilingi 35,995,850 ikiwa ni mchango wa TASAF pekee na wananchi pamoja na kikundi cha ushirika kuchangia nguvu kazi.


Mratibu huyo wa TASAF aliutaja mradi mwengine ambao pia wanajamii hawapaswi kuchangia ni ule wa kilimo cha umwagiliaji maji uliopo shehia za Mgogoni na Wawi wilaya ya Chake Chake.

Katika awamu ya kwanza kwa shehia ya Wawi, TASAF ilitoa zaidi ya shilingi 39 milioni, na awamu ya pili ya mradi huo kwa shehia ya Mgogoni TASAF ilitoa zaidi ya shilingi 44 milioni.

“Miradi kama hii mara zote TASAF haiwalazimishi wanajamii kuchangia na badala yake wao hupata ajira ya muda kwani hushiriki katika kazi mbali mbali kama vile uchimbaji wa misingi na kuchota udongo na kisha kulipwa,” alieleza Mratibu huyo wa TASAF.

Hata hivyo ameitaja miradi ya ufugaji wa kuku wa mayai na ufugaji wa ng’ombe wa kienyeji na mbuzi kuwa wanajamii hupaswa kuchangia fedha kwa asilimia 20 na kiasi kilichobakia hutolewa na TASAF.

Alifafanua kuwa mradi wa ufugaji wa kuku wa mayai uliopo shehia ya Mbuguwani wilaya ya Mkoani kuwa jumla ya shilingi 10 milioni zilitumika kwa kufanikisha mradi huo.

Kati ya fedha hizo jamii yenyewe ilichangia shilingi 490,000 wakati TASAF ilitoa zaidi ya shilingi 9 milioni sawa na asilimia 80 ya gharama za mradi huo.

Kuhusu mradi wa ufugaji wa ng’ombe wa kienyeji, kuku pamoja na mbuzi uliopo shehia ya Jombwe Mwembe wilaya ya Mkoani, Mratibu huyo alisema, miradi hiyo imewanufaisha wananchi 108 wanaounda vikundi 9 wakiwemo wanawake na wanaume.

Alisema mradi wa ng’ombe pekee umegharimu zaidi ya shilingi 58 ambapo umehusisha ununuzi wa ng’ombe 65 wakiwa madume watano na kuhusisha vikundi vitano vya wananchi wa shehia hiyo.

Alifafanua kuwa kati ya fedha hizo jamii ilichangia zaidi ya shilingi milioni 28 na TASAF ulitoa shilingi zaidi ya shilingi 30 milioni.


Kuhusu miradi mitatu ya ufugaji wa mbuzi wa asili na mmoja wa ufugaji wa kuku, alisema jumla ya shilingi milioni 87 zilitumika, ambapo TASAF ilitoa zaidi ya shilingi 44 milioni, na wanajamii wenyewe walichangia shilingi 43 milion.

Mratibu huyo wa TASAF aliwataka wananchi waliofaidika na miradi hiyo kuhakikisha wanaitunza na kuienzi ili iwe endelevu na kuwanufaisha wao na kizazi kijacho.

Aidha alisema TASAF awamu ya tatu iko njiani na itaangalia pamoja na miradi mikubwa ili kuzidi kuwang’arisha wananchi kimaendeleo katika maeneo yao siku hadi siku.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.