Habari za Punde

TMA kuweka kituo bandarini Zanzibar



Na Husna Mohammed
MAMLAKA ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) kanda ya Zanzibar, inakusudia kufungua  ofisi yake bandarini Zanzibar kwa lengo la kuimarisha shughuli zake.
Ofisi za mamlaka hiyo inatarajiwa kufunguliwa wakati wowote kuanzia mwezi wa Machi mwaka huu.
Akizungumza na gazeti hili ofisini kwake, Mkurugenzi wa Mamlaka hiyo Zanzibar, Khamis A. Suleiman, alisema wameamua kufungua ofisi hiyo kwa lengo la kusogeza karibu huduma kwa wananchi katika eneo hilo la bandari.
“Kwa kuwa sehemu zinazotumika kwa usafiri kama viwanja vya ndege ni lazima kuweko na ofisi hivyo tumezingatia kwa kina kufungua ofisi bandarini kwa ajili ya kuwapa taarifa wananchi kwa urahisi taarifa za hali ya hewa,” alisema.

Hata hivyo, Mkurugenzi huyo alisema wamekuwa wakikabiliwa na upungufu mkubwa wa vitendea kazi jambo ambalo linawapa ugumu katika kutekeleza majukumu yao.
Alisema kiujumla mtandao wa vituo vya kupokea taarifa bado ni mdogo Unguja na Pemba jambo ambalo linachangiwa na upungufu wa vifaa.
Mamlaka ya hali ya hewa Zanzibar ni moja ya taasisi muhimu ambayo imekuwa ikitoa taarifa za mara kwa mara za hali ya hewa kwa wananchi na hasa wasafiri, wakulima na wanaotembelea mwambao wa pwani ya Afrika Mashariki.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.