Habari za Punde

Wakenya wasali kuliombea amani taifa



Na Mwandishi maalum, Kenya
MAELFU ya Wakenya kutoka dini na makabila tafauti jana walikusanyika katika viwanja vya Uhuru kuiombea amani nchi hayo, siku tano tu kabla ya kuingia katika uchaguzi mkuu utakaofanyika Machi 4.
Sala hiyo ambayo iliongozwa na Mchungaji, David Owuor pia ilihudhuriwa na wagombea wote wa kiti cha urais, isipokuwa Musalia Mudavadi.
Tofauti na mikusanyiko mengine, katika ibada hiyo wagombea wote walikaa jukwaa moja na kuungana na Wakenya kusali pamoja na baadae kuomba dua ya kuliombea taifa hilo.
Wagombea wote waliahidi kukubali matokeo kama uchaguzi huo utafanyika kwa misingi ya uhuru na haki.


Mgombea urais kupitia chama cha Narc-Kenya, Martha Karua  aliwambia Wakenya waliokusanyika katika viwanja hivyo kuwa atakubali kushindwa kwa lengo la kudumisha amani na mshikamano wa Wakenya.
Alisema atafanya kila analoweza kuhakikisha uchaguzi huo unakuwa wa amani  na kuwaomba raia wote pamoja na wagombea wengine kuhakikisha amani na utulivu inadumishwa nchini humo.
Kwa upande wake, Waziri Mkuu, Raila Odinga alisema  amani itaendelea kudumishwa nchini Kenya kabla na baada ya uchaguzi na kuahidi kuwa uchaguzi huo utakuwa huru.
Naibu Waziri Mkuu, Uhuru Kenyatta alisema atakubali kushindwa kama rais atakaechaguliwa atashinda kihalali.
Wakati huo huo, mgombea urais kupitia muungano wa Amani,Musalia Mudavadi amewaonya Wakenya kutowachagua wagombea wanaokabiliwa na kesi katika mahakama ya kimataifa ya uhalifu (ICC) akisema uhusiano wa Kenya na nchi za magharibi utaharibika kama wagombea hao watachaguliwa kuiongoza nchi.
Mudavadi alisema Kenya iwe tayari kukabiliwa na vikwazo vya kiuchumi ambavyo vitaathiri kasi ya ujenzi wa uchumi wa taifa.
“Sina mamlaka ya kuzungumza kwa niaba ya nchi za magharibi, lakini ninachowambia ni uzoefu nilionao kama nchi hizi zitatuwekea vikwazo vya kiuchumi,” alisema Mudavadi.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.