Habari za Punde

Pemba watakiwa kuwa wabunifu

Na Mwandishi wetu
 
MKUU wa Mkoa wa Kusini Pemba, Juma Kasim Tindwa, amewataka wananchi wa kisiwani hapa kuwa wabunifu katika shughuli zao za kila siku, ili kubadilisha hali ya maisha waliyonayo na kuingia katika ushindani wa kimaendeleo.
 
Tindwa alitoa kauli hiyo kisiwani Pemba jana wakati akifungua majadiliano ya ushirikiano kwa manufaa ya wote (smart partnership dialogue) ikiwa ni mwendelezo wa majadiliano yanayofanyika katika kanda mbalimbali nchini.
 
“Watu wa kisiwani Pemba lazima tubadilike, tuondoe ule uzamani tulionao, majadiliano haya yana maana kubwa sana kwetu, ni lazima tuzingatie yale yatakayozungumzwa na watoa mada ili tukitoka hapa tuwe na mtazamo tofauti,” alisema Tindwa.
 
Alisisitiza kutokana na kaulimbiu ya majadiliano haya kuwa ni ‘matumizi ya teknolojia katika kuleta maendeleo endelevu’, ni lazima watu wabadilike kwa kila nukta ya kazi zao wanazofanya, waweke ubunifu zaidi ya kukaa na kushikilia yale ya zamani,” alisema.
 
Alisema Baraza la Biashara la Zanzibar (ZBC) liko bega kwa bega na Baraza la Taifa la Biashara (TNBC) katika kuhakikisha majadiliano haya yanaleta tija na nguvu ya pamoja katika kuleta maendeleo ya wananchi wa Tanzania Bara na Tanzania Visiwani.
 
Mkuu wa Fedha na Utawala wa TNBC, Oliva Vegulla, alisifu ushiriki na michango mbalilimbali kutoka kwa washiriki wote katika mkutano huo.
 
TNBC ndio waliopewa dhamana ya kuratibu majadiliano hayo ya kikanda na ya kitaifa pia.
 
Chanzo - Tanzania Daima

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.