Habari za Punde

Mvua imeleta madhara kwa mmoja ya Nyumba za Mji Mkongwe Zenj.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi akijumuika na baadhi ya Wananchi kuangalia athari iliyojichomoza kwenye nyumba ya Bwana Salim Ahmed Salim baada ya ukuta na dari yake kuanguka  saa sita usiku juzi mkabala na Skuli ya Sekondari ya Tumekuja Mtaa wa Vuga Mjini Zanzibar.
Sehemu ya mbele ya Nyumba ya Bwana Salim Ahmed Salim iliyoporomoka  Mtaa wa Vuga mkabala na Skuli ya Sekondari ya Tumekuja.Hata hivyo hakuna mtu aliyejeruhiwa kutokana na athari hiyo.
Athari ya nyumba iliyobomoka hapo Mtaa wa Vuga ilisababisha usumbufu wa watumiaji wa Bara bara itokayo Vuga kuelekea Shangani au Serena na kulazimika kufungwa kwa bara bara hiyo.

Mamlaka ya Hifadhi ya Mji Mkongwe wa Zanzibar, Jeshi la Polisi pamoja na Mamlaka ya Usafiri zimekumbushwa kuendelea kuzuia uingiaji wa  gari kubwa zenye uzito wa zaidi ya Tani Mbili katika eneo la Mji Mkongwe ili kunusuru majengo yaliyono ndani ya mamlaka hiyo.

Kumbusho hilo limetolewa na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alipofanya ziara fupi  kukagua athari ya nyumba  iliyoporomoka ukuta na Dari yake juzi usiku iliyopo Mkabala na Skuli ya Sekondari ya Tumekuja  Mtaa wa Vuga Mjini Zanzibar.

Balozi Seif alisema ukaidi wa baadhi ya madereva  wa gari kubwa kupitisha Gari gari zao katika eneo hilo umesababisha uchafuzi wa mandhari na haiba ya Mji mkongwe wa Zanzibar ambao hivi  sasa uko katika urithi wa Kimataifa.

“ Jeshi la Polisi wakati huu litahitajika kuwa na kazi ya ziada katika kuhakikisha agizo lililotolewa na Mamlaka ya Mji Mkongwe wa Zanzibar  linatekelezwa ipasavyo “. Alisisitiza Balozi Seif.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar akimpa pole Mmiliki wa Nyumba hiyo Bwana  Salim Ahmed Salim  kwa hasara  aliyoipata alimtaka kuwasiliana na Uongozi wa Mamlaka ya Hifadhi ya Mji Mkongwe wa Zanzibar  katika juhudi zaujenzi wa nyumba hiyo utakaozingatia  mpango  halisi wa uhifadhi wa Mji huo.

Akitoa ufafanuzi wa athari nyingi zilizojitokeza ndani ya nyumba za Mji Mkongwe, Mkuu wa Kitengo cha Ushirikiano na Utafiti cha Mamlaka ya Hifadhi ya Mji Mkongwe wa Zanzibar Bibi Madina Haji Khamis alisema ujenzi usiozingatia utaalamu wa Mamlaka  husika pamoja na upitishwaji wa gari kubwa ndio sababu kubwa za msingi za athari hizo.

Bibi Madina alifahamisha kwamba baadhi ya  wamiliki wa nyumba hizo walikuwa wakipandishia kuta  wakati wa ujenzi au matengenezo zaidi ya uwezo wa msingi wa nyumba hizo hali  inayoleta athari ya mipasuko ya nyumba hizo sambamba na mitetemeko ya gari kubwa zinazopitishwa pembezoni mwa nyumba hizo.


Mapema Mmiliki wa Nyumba hiyo Bwana Salim Ahmed Salim alimueleza Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar  Balozi Seif kwamba dalili za kuanguka kwa jengo hilo zilijionyesha mapema kutokana na kuvimba na baadaye kupasukwa kwa eneo la mbele la ukuta wa nyumba hiyo.

Bwana Salim alifahamisha kwamba kutokana na hali hiyo alilazimika kuuarifu Uongozi wa Mamlaka ya Hifadhi ya Mji Mkongwe wa Zanzibar uliolazimia baadaye kwa kushirikiana na jeshi la Polisi kuchukuwa hatua za kuifunga bara bara hiyo.

“ Nilijaribu kuufuata Uongozi wa Mamlaka ya Hifadhi ya Mji Mkongwe uniruhusu kuifanyia matengenezo makubwa nyumba yangu  ili baadaye niitumie kwa makazi na familia nyangu lakini bado sijapata jibu na huku inaporomoka “. Alieleza Bwana Salim Ahmed Salim.

Nyumba hiyo ya ghorofa moja mpaka inaporomoka ukuta na dari yake majira ya saa sita juzi usiku lakini hamna watu waliokuwa wakiishi ndani yake.

Mamlaka ya Mji Mkongwe wa Zanzibar kwa kushirikiana na Taasisi nyengine zimelazimika  kuzuia  Gari zote zinazotumia  Bara bara hiyo kutoka Vuga kuingia Shangani au kupitia Serena  ili kujaribu kuepuka hatari katika kipindi hichi cha Mvua za Masika.

Kwa mujibu wa hali halisi ilivyo hivi sasa gari zote zinazokusudia kuingia ndani ya eneo la Mamlaka ya Mji Mkongwe zinalazimika kutumia Bara bara itokayo Malindi na zisizidi uzito wa zaidi ya Tani mbili.


Mamlaka ya Hifadhi ya Mji Mkongwe wa Zanzibar kwa miaka kadhaa sasa imo ndani ya Ramani ya Dunia ya urithi wa hifadhi ya Kimataifa chini ya usimamizi wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu,Sayansi na Utamaduni  { UNESCO }.

1 comment:

  1. Sasa kipi ni sahihi kati ya kuporomoka kwa jengo hilo kati ya kupita magari makubwa,mvua,uchakavu wa umri wa jengo au majengo au ingredients zilizotumika katika kujenga jengo hilo.Wacheni kudanganyana jamani na mkazibwa macho na Unesco kwa uhifadhi wa mji mkongwe.Ikumbukwe kwamba majengo hayo yote ya mji mkongwe yalijengwa miaka 200 iliyopita kwa kuchanganywa dongo,chokaa na mawe.Sasa hayana uhimili tena maana yamechoka.Yakirowa maji yanajiachia,vishindo kidogo ndio safari.Ikumbukwe pia Unesco wanaziba macho suala la uhifadhi maana huko makwao Unesco majengo yaliyojengwa kwa saruji,na zege wakiyaona na athari kidogo tu basi ni kuvunjwa ku-demolish na kujengwa jipya lenye kila aina ya proof-kama ni fire proof,water proof au hata tetemeko - earthquake proof . Kwetu sisi wanatuziba macho kwa vijipesa wanavyochangia.Tusipokuwa macho naamini majengo ya mji mkongwe yataleta maafa makubwa kwa kupoteza roho za watu.

    ReplyDelete

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.