Habari za Punde

‘SMZ yajidhatiti kusaidia wananchi’

Na Mwantanga Ame,Pemba
MFUKO wa uwezeshaji wananchi kiuchumi, ni fursa mpya inayolenga  kuyasaidia makundi ya wananchi wa kipato cha chini,Makamu wa Pili wa Rais, Balozi Seif Ali Iddi, amesema.

Aliyasema hayo jana wakati akizindua utoaji wa mikopo ya mfuko wa uwezeshaji wananchi kiuchumi, kwa wananchi wa Pemba, katika uwanja wa skuli ya Micheweni wilaya ya kaskazini Pemba.

Alisema serikali imeamua kuanzisha mfuko huo kwa dhamira ya kuwasaidia wananchi kuwa na mbinu mbadala za kupambana na umaskini, hivyo wananchi wazitumie fursa zilizopo.

“Ujasiriamali ni ajira, msifikiri ajira ni kwenda jeshini, uhamiaji, KMKM, au vikosi vyengine, kuna watu wana ajira zinaweza kuwaingizia 100,000 kwa siku watu wametajirika kwa kuuza soji za punda tu, sasa msidharau hili,” alisema.

Alisema kuna benki 10 zinatotoa huduma za kifedha huku mifuko ya kutoa mikopo ikiwa miwili na SACCOS kubwa sita, jambo ambalo linaloonesha bado kuna mahitaji ya  wananchi kusaidiwa.


Aidha alisema serikali imeamua kuimarisha mfuko huo, ambao utakuwa hauna masharti magumu ili kuwawezesha wananchi kujituma na kujisaidia, kwani ni moja ya mfumo unaofuatwa na baadhi ya mataifa duniani.

Kwa mfano alisema India, Bagladesh, Bolivia, Indonesia na Uingereza, zimekuwa na mifuko ya aina hiyo ambayo  inawasaidia wananchi wake kupata uwezo wa kubadili maisha yao.

Alisema kila kijana kuanzia sasa atakuwa na uwezo kupata fursa hiyo, kwa kuzingatia utaratibu uliowekwa kwa kuhakikisha anakopa na kulipa madeni yao, kwani mikopo hiyo itakuwa ikitolewa kwa kila shehia za Zanzibar.

Alisema mfuko huo utakuwa unamilikiwa na wananchi wenyewe kwenye mauneo yao, jambo ambalo litaweza kuwaletea mafanikio makubwa katika siku chache zijazo.

Aliwakabidhi wananchi hao hundi ya shilingi milioni 25, kwa vikundi 13, kwa niaba ya wajasiriamali wa  Pemba, ambapo kwa awamu ya kwanza fedha zilizoidhinishwa ni shilingi 75,650,000 kwa wilaya nne za Pemba.

Waziri wa Wizara ya Ustawi wa Jamii, Vijana, Wanawake na Watoto, Zainab Mohammed, aliwataka wananchi waliopewa mikopo hiyo kuitumia vizuri na kuhakikisha inatimiza malengo yao.

Alisema jumla ya maombi 1,215 yenye thamani ya shilingi milioni 77.8 yamepokelewa kutoka  wilaya 10 za Zanzibar,   na mfuko umekamilisha kupitia  maombi 433 wanawake wakiwa 225 na wanaume 167.

Mapema Katibu Mkuu wa wizara hiyo, Asha Ali Abdalla, alisema hadi sasa mfuko huo una kiasi cha shilingi 972,140,000 ambazo ni sawa na asilimia 95.


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.