Na Mwandishi wetu
ZAIDI
ya shilingi bilioni nne zimenusurika
kuibwa katika mfuko mkuu wa hazina ya serikali baada ya mtandao wa watuhumiwa
wa wizi wa kimataifa kutiwa mbaroni walipowasilisha madai ya kughushi ya
kulipwa euro milioni 200 na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.
Watuhumiwa
hao ambao ni raia wa Marekani, Oman na Tanzania, waliwasilisha nyaraka hizo kwa
Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha Zanzibar, Khamis Mussa, ili walipwe kiwango hicho ambacho wanadai kuikopesha
serikali ya wamu ya sita.
Uchunguzi
uliofanywa na gazeti hili, umegundua kwamba watuhumiwa hao walifanikiwa
kughushi saini za aliekuwa Rais wa Zanzibar wa awamu ya sita, Dk. Amani Abeid
Karume, Waziri aliekuwa akisimamia masuala ya fedha, Dk. Mwinyihaji Makame
Mwadini na Katibu Mkuu Wizara ya fedha wakati wa utawala wa serikali ya awamu
ya tano, Dk. Salmin Amour Juma, Omar
Sheha Mussa.
Hata
hivyo, walipotakiwa kueleza kitu gani walichoikopesha serikali walishindwa
kuainisha.
Kwa mujibu wa wapasha habari wetu, baada
ya kuwasilisha madai hayo, Katibu Mkuu fedha alishtuka kuiona saini ya aliekua Katibu Mkuu wa wizara
hiyo katika serikali ya awamu ya tano, Omar Sheha, ambae hakuwahi kuwa Katibu
Mkuu fedha katika serikali ya awamu ya sita, huku watuhumiwa wakidai kwamba
wameikopesha serikali ya awamu ya sita.
“
Watuhumiwa wa wizi huu walishtukiwa baada ya kutakiwa kuleta mikataba yao
waliotiliana saini na Serikali na kutakiwa kueleza waliikopesha nini Serikali
ndipo walipoleta mikataba ya kughushi na kukutikana saini za viongozi hao
ambazo inaaminika kuwa sio sahihi,” alisema mmoja wa wapasha habari wetu ambae
hakutaja jina lake litajwe gazetini.
Watuhumiwa hao walitambulika kwa majina
ya Said Gamaleldin mwenye paspoti ya
Marekani, Yaqoob Sulaiman Al- Mahrouqi raia wa Oman na mwenyeji wao Mtanzania alietambulika kwa jina
la Shiraz Haroun Jaffer mkaazi wa Moroko
jijini Dar es Salaam.
Alipoulizwa Naibu Mkurugenzi wa makosa ya
jinai Zanzibar (DCI), Yussuf Ilembo, juu ya suala hilo alikiri kukamatwa kwa
watu hao.
Alisema kwa vile upepelezi bado
haujakamilika ni mapema kutoa taarifa za wahusika hao kwa kuepuka kuharibu
upelelezi.
“Ni kweli tumewakamata watu watatu
wanaosadikiwa kufanya kosa hilo ila kwa sasa bado mapema kutoa taarifa zao kwa
kuepuka kuharibu upelelezi, tutapokamilisha upelelezi tutatoa habari zao,”
alisema.
Habari kutoka mahakamani zinasema
kuwa washtakiwa hao tayari
wameshafikishwa mahakama ya mkoa Vuga , chini ya Hakimu George Kazi ambapo
walisomewa mashitaka mawili.
Shitaka la kwanza ni la kughushi nyaraka
za serikali na la pili ni la kuwasilisha nyaraka za kughushi za serikali kwa Katibu
Mkuu wa Wizara ya fedha kwa lengo la
kulipwa euro milioni 200.
Washitakiwa hao wote watatu wamepelekwa
rumande hadi Julai 10 ambapo kesi yao itatajwa tena.
Aidha dhamana yao ilikataliwa baada ya upande wa
mashtaka uliongozwa na Wanasheria wa Serikali, Walid Mohamed Adam, Mohammed
Saleh na Karima Alawi kukataa dhamana kwa madai kuwa upelelezi wa shauri hilo
bado haujakamilika.
Aidha
walisema washtakiwa wawili kati ya watatu ni wageni hivyo kupewa dhamana
wanaweza kukimbia.
Itakumbukwa katika kikao cha Bajeti cha
Baraza la Wawakilishi kinachoendelea hivi sasa Waziri wa Fedha, Omar Yussuf
Mzee, alitoa tahadhari ya kuwa fedha za Serikali hazitolipwa kiholela bila ya
kufanyiwa uchunguzi wa kina.
No comments:
Post a Comment