Habari za Punde

Baadhi ya makosa yanayotokea wakati wa kutoa Zakaatul Fitr


Abu Ammaar

Baadhi ya makosa yanayotokea wakati wa kutoa Zakaatul Fitr

1     Kuitoa wakati wa Sala ya Idd, siku ya Idd yenyewe.

Zakaatul Firtr hupaswa kutolewa mapema ili iwafikie walengwa waliokusudiwa. Ikitolewa wakati wa Sala hukosa ile dhamira iliyokusudiwa ya kuwalisha maskini na wenye kuhitaji na kuwafika kwa wakati.
Ni Sunna ikatolewa siku moja au mbili kabla ya siku ya Idd. Baadhi ya Maulamaa wamejuzisha kutolewa hata kabla ya hapo ikiwa itakuwa na manufaa zaidi na kuweza kuwafika wahusika kwa wakati.

 2  Kuisafirisha kuipeleka sehemu nyengine bila ya dharura

Hasa ndugu zetu hupenda kupeleka Zakaatul fitr nchi walizotoka au huenda Misikitini na kuweka katika masanduku yaliyoandikwa Zakaatul Fitr wakidhani tayari wameshatekeleza wajibu.
Asli ya Zakaatul Fitr ni kutumika sehemu inayotolewa kama kuna wanaostahiki na wanahitaji. Kama hakuna hapo inajuzu kuisafirisha kuipeleka sehemu nyingine na huwajibika kwa mwenye kuitoa kwa njia hii kuhakikisha kwamba aliowapa ni watu thika wanaoaminika na ni kweli wataifikisha kwa wahusika kabla ya siku ya Idd.

Vyenginevyo bado mtoaji atakuwa na dhimma kwa Zakaah hii ikiwa haikuwafika walengwa katika muda unaotakiwa

3    Kutoitoa kabisa
Baadhi ya ndugu zetu katika dini wanadhani kutoa Zakaatul Fitr si wajibu au si lazima hiyo wakiitoa sawa na kama hawakuitoa pia ni sawa.
Zakaatul Fitr ni wajibu kwa kila Muislamu aliyeshuhudia mfungo wa Ramadhaan. Kama haikutolewa hiyo ni dhambi kubwa na mas’uuliyah (jukumu) kwa mhusika na atakwenda  kuulizwa na Mola wake. Hutolewa na mwenye kuisimamia familia na huwatolea wote wanaomtegemea katika familia yake. 
4    Kuchanganya kati ya Zakaatul Fitr na Zakaatul Maal
Baadhi ya ndugu zetu hawaoni tofauti kati ya Zakaah ya mali na Zakaatul Fitr hivyo hujiweka katika kundi la kwamba hawana sifa ya kuitoa.
 Zakaatul Fitr ni maalum kwa ajili ya mwezi wa Ramadhaan tu na haina uhusiano kabisa na Zakaatul Maal isipokuwa ni jina tu ndilo hushirikiana.
Na wanaowajibika kuitoa wana hukumu tofauti na Zakaah ya mali. Hivyo lazima itolewe bila ya kuihusisha na Zakaah ya mali.. 
5   Kuitoa na kuwapa pesa wanaostahiki badala ya chakula
Asli ya Zakaatul Fitr ni hutolewa chakula kwa mujibu wa Hadithi ya Mtume Swalla Allaahu ‘Alayhi Wasallam si pesa. Na kama itatolewa pesa basi walio na dhamana itawabidi wanunue chakula na kuwapa wanaostahiki kwa siku hii ye Idd ili nao wawe miongoni mwa walio katika furaha katika siku hii muhimu. 

Baadhi ya Maulamaa wamejuzisha kutolewa pesa ikiwa tu kama itakuwa na manufaa zaidi kwa wanaohitajia kuliko chakula.
6   Kuwapa Zakaatul Fitr wasiokuwa Waislamu
Moja ya malengo ya kutolewa Zakaatul Fitr ni kuwalisha maskini na wenye kuhitaji miongoni mwa Waislamu siku ya Idd. Hivyo Zakaatul Fitr ni maalum kwa masikini na wanaohitaji miongoni mwa Waislamu tofauti na sadaka ambayo wanaweza kupewa wasiokuwa Waislamu .

 7  Zakaatul Fitr kutumika katika miradi mengine
Baadhi ya ndugu zetu hutoa Zakaatul Fitr kwa ajili ya kuchangia Msikiti au ujenzi wa Madrasah, kujenga kisima na kadhalika.

Zakaatul Fitr haiwezi kutumika katika malengo yasiyokusudiwa hata kama yatakuwa ni ya kheri kwani dini yetu ina taratibu zake kwa kila kinachotolewa kwa mujibu wa munasaba wake. Zakaah hii ni kwa ajili ya wanaohitajia miongoni mwa Waislamu na si vyenginevya na kiwango chake ni kidogo mno ambapo kila mmoja wetu ana uwezo wa kukitoa.
 
Na Allaah ndie ajuaye

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.