HOTUBA
YA MAKAMU WA PILI WA RAIS WA ZANZIBAR, BALOZI SEIF ALI IDDI ALIYOITOA KATIKA UZINDUZI WA MPANGO WA MIKOPO KWA WASTAAFU
KUPITIA BENKI YA POSTA TAREHE 19 JULAI, 2014
Afisa Mtendaji Mkuu wa Benki ya Posta,
Mkurugenzi Mwendeshaji, Mfuko wa Hifadhi ya Jamii, Zanzibar,
Ndugu Wafanyakazi wa Mfuko wa Hifadhi ya Jamii na Benki ya
Posta,
Ndugu Wanahabari,
Ndugu
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana.
Assalaam
Alaykum Warahmatullahi Wabarakatuh.
Naomba
kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujaalia kufika hapa siku hii ya leo tukiwa
wazima, hatuna budi kumshukuru Mola wetu kwa ukarimu wake.
Napenda
kutoa shukrani zangu za dhati kwa
uongozi wa Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa kunipa heshima ya kunialika kuwa mgeni
rasmi katika hafla hii ya uzinduzi wa mpango wa kutoa mikopo kwa waastafu.
Ahsanteni sana, na naahidi kuienzi heshima hii kubwa mliyonipa katika mwezi huu
Mtukufu wa Ramadhan.
Aidha, naomba
kuushukuru Mfuko wa Hifadhi ya Jamii Zanzibar pamoja na Benki ya Posta
kwa kubuni mpango maalum wa kutoa mikopo
kwa wastaafu ili waweze kuishi maisha yenye matumaini. Uzoefu wa maisha yetu ya kila siku unaonyesha
kuwa wastaafu hupata taabu ya kukopeshwa kwa kuwa wanajulikana mapato yao
yamepungua, na pale wanapobahatika kukopeshwa hufuatwa siku ile ile wanayolipwa
pensheni zao za kila mwezi. Wakati
mwengine matangazo ya radio ya kuitwa wastaafu kwenda kuchukuwa pensheni zao
Wizara ya Fedha huleta huzuni kwa wastaafu wadaiwa.
Ndugu Wastaafu,
Mpango huu wa
utoaji mikopo kwa wastaafu ambao umeshaanza kutekelezwa una lengo la kuleta
faraja na kuwasaidia wastaafu katika kukidhi mahitaji yao ya mbali mbali ya
kimaisha. Mikopo inayotolewa huwasaidia wastaafu kulipia gharama za matibabu,
ada za shule za watoto au wajukuu zao au kuendesha biashara ndogo ndogo
zitakazosaidia kupunguza ukali wa maisha ya kila siku.
Azma ya
Serikali yenu ya Mapinduzi ya Zanzibar ni kujenga mazingira mazuri kwa wastaafu
wake ili kustaafu kusiogopwe na kuonekana ni mwanzo wa kuanza kwa kipindi cha
maisha ya shida, yasiyokuwa na matumaini. Tunataka wafanyakazi wetu wanapopata
barua za kustaafu wasianze kuhuzunika kama ilivyozoeleka.
Ndugu Wastaafu,
Napenda kutoa
wito kwa wale wastaafu wenye sifa za kuomba mikopo hii wajitokeze kwa
wingi. Hii ni fursa muhimu kwenu
kujiendeleza kimaisha. Ni imani yangu
kuwa pindipo tutaitumia mikopo hii vizuri tutaishi maisha mazuri pia. Kuitumia mikopo vizuri maana yake ni kuitumia
mikopo kwa shughuli tulizoziombea mikopo hiyo, na siyo vyenginevyo.
Kwa wastaafu
watakaopenda kukopa, ushauri wangu wa bure
mtu akope kwa mujibu wa uwezo wake.
Na akumbuke kuwa mkopo ni lazima kulipwa kwa kupitia pencheni zenu
pamoja na asilimia ya riba ambayo Benki imejipangia. Wadaiwa wote watalazimika kurejesha mikopo
hiyo katika kipindi cha mwaka mmoja hadi miaka mitatu kulingana na umri wa
mwombaji. Aidha, ni vyema tukajipanga vizuri kabla ya kukopa kwani mkopo sio
sadaka.
Mwisho,
napenda kuhitimisha hotuba yangu kwa kuwaomba wastaafu watakaochukuwa mikopo
kwa kufanya biashara kuhakikisha kuwa biashara wanazotaka kuzifanya wanazielewa
vizuri ili kuepukana na hasara.
Kwa mara
nyengine tena nawapongeza wale wote waliobuni mpango huu wa kutoa mikopo kwa
wastaafu. Hakika mpango huu ni mkombozi
kwa mstaafu na pia utasaidia Taifa letu kupambana na umasikini wa kipato. Ni matarajio yangu kuona wastaafu
wanajitokeza kwa wingi kuchukua mikopo ili kuweza kujiendeleza kimaisha kwa
kuwekeza mikopo hiyo kwenye miradi yenye faida nzuri.
Baada ya
kusema hayo, napenda kutamka kuwa Mpango wa Mikopo kwa Wastaafu umezinduliwa
rasmi na nyote mnakaribishwa na mtapokelewa kwa mikono miwili.
Ahsanteni kwa kunisikiliza.
No comments:
Post a Comment