Na Joseph Ngilisho,Arusha
SIKU chache baada ya Sheikh Mkuu wa Tanzania, Mufti Shabaan bin Simba,
kutangaza uongozi mpya wa msikiti wa Ijumaa na msikiti wa Quba iliyopo
jijini hapa,Sheikh wa msikiti wa Qiblatan,Sood Ally Sood (37), amejeruhiwa baada
ya kushambuliwa kwa bomu la kurushwa kwa mkono nyumbani kwake wakati akila daku
na kujeruhiwa vibaya.
Aidha mbali na Sheikh huyo,mtu mwingine aliyekuwa nyumbani kwake,
aliyetajwa kwa jina la Muhaji Kifea (38) mkazi wa Sinza jijini Dar es Salaam,
naye amejeruhiwa vibaya na wote wamelazwa hospitali ya mkoa Mount Meru kwa
matibabu.
Sheikh huyo alijeruhiwa miguu yote miwili na mapajani huku Kifea akipata
majeraha makubwa miguuni na kupoteza baadhi ya vidole vya miguu yote miwili.
Akizungumza hospitalini hapo, Sheikh Sood, alisema tukio hilo lilitokea
nyumbani kwake eneo la majengo ya
chini,usiku wa kuamkia jana majira ya saa 5:00
wakati yeye pamoja na mgeni wake wakila chakula sebuleni .
Alisema alishangaa kusikia mripuko mkubwa ulioambatana na vyuma na kujikuta
akiwa na majeraha makubwa.
“Hawa watu kimsingi wanafahamika maana walishawahi kunitishia kupitia waraka
wa maandishi pamoja na kunifyatulia risasi,” alisema.
Alisema siku tatu kabla ya tukio hilo alikoswa kuuawa kwa risasi na watu
wasiofahamika wakati akitoka msikitini na kutoa taarifa kituo kikuu cha polisi
jijiji hapa.
Akizungumzaia tukio hilo Mkuu wa Mkoa wa Arusha ,Magesa Mulongo,alichukizwa
na kitendo hicho na kusema hatua zitachukuliwa kwa wahusika.
Aidha alisema polisi linawashikiwa baadhi ya watuhumiwa wa matukio ya mabomu.
Naye kamanda wa polisi mkoani Arusha, Liberatusi Sabasi ,alithibitisha kutokea
kwa tukio hilo na kueleza kuwa majeruhi bado wanaendelea na matibabu.
Mbunge wa Arusha mjini,Godbless Lema,alilitaka jeshi la polisi kurejesha amani
jijini hapa kwa kulichukulia kwa umakini suala hilo.
No comments:
Post a Comment