Na Salum Vuai, Maelezo
SHILINGI bilioni 6.189, zitatumika kwa ajili ya kuzifanyia matengenezo
barabara mbali mbali Unguja na Pemba.
Taarifa kutoka Mfuko wa Barabara zimefafanua kuwa shilingi bilioni 3.278
zitagharamia barabara za Unguja, na wakati zile za Pemba zitatumia shilingi
bilioni 2.264.
Aidha shilingi milioni 647 zimetengwa na mfuko huo kwa ajili ya kazi za
dharura, matengenezo ya vifaa na mchango kwenye miradi ya serikali, ambapo pia
kwa mwaka huu kazi zenye thamani ya ya shilingi bilioni 3.281 sawa na asilimia
53 ya fedha zote zitafanywa na wakandarasi binafsi.
Hafla ya utiaji saini mkataba wa kutekeleza kazi hizo, imefanyika jana
ambapo Mfuko wa Barabara uliwakilishwa wa Mwenyekiti wa Bodi, Ali Abdalla
Suleiman na Katibu Mkuu Wizara ya Miundombinu na Mawasiliano, Dk. Juma Malik
Akili alisaini kwa niaba ya wizara yake.
Kwa mujibu wa taarifa ya Bodi ya Mfuko huo, makubaliano hayo ya kazi
yanafanyika kukidhi mahitaji ya sheria mfuko kifungu 8 A (b) inayoiruhusu bodi
kuingia mkataba wa kazi na Wizara inayoshughulika na barabara au wakala mwengine
anaekubalika.
Utekelezaji wa kazi hizo unafanyika baada ya kukamilika kwa mpango kazi wa
matengenezo hayo kwa kipindi cha mwaka wa fedha unaoanzia Julai 2014 hadi Juni
mwaka 2015.
Taarifa iliyotolewa na Bodi ya Mfuko huo imesema mpango wa mwaka huu wa
matengenezo umezingatia zaidi kuhami barabara kubwa, madaraja na huduma za
usalama wa barabara.
Barabara zitakazonufaika na mpango huo kwa upande wa Unguja ni,
Mwanakwerekwe Makaburini/Fuoni, Bumbwini/Kiongwe skuli, Magereza/Kwa
Mchina/Tomondo na Michenzani/Mtendeni.
Nyengine ni Mshelishelini/Gamba, Amani/Mtoni na daraja la Kitope, alama za
barabarani na taa za kuongozea magari katika makutano ya barabara ya
Malindi.
Kwa upande wa Pemba ni Ole/Konde, Kangani/Mkanyageni, Chake Chake/Mkoani,
katika eneo la Kwachangawe, Pandani/Mlindo na barabara nyenginezo.
Bodi ya Mfuko wa Barabara imehakikisha kuwa wakati wote wa kazi hizo,
wataalamu wa kiufundi na fedha watafanya uangalizi wa karibu kuhakikisha
ufanisi wa kazi hizo.
Taarifa hiyo imeongeza kuwa, mwishoni mwa mwaka, Mfuko wa Barabara utaajiri
wakaguzi huru wa fedha na kazi kwa ajili ya kupata maoni yanayohusu namna fedha
hizo zitavyotumika.
No comments:
Post a Comment