Na Mwandishi wetu
RAIS wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania, Jakaya Kikwete, amesema yeye hana tatizo kukutana na
wajumbe wa Bunge Maalum la Katiba kutoka Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA).
“Wanajua jinsi ya kukutana nami, ili tuweze
kutafuta namna ya kumaliza tofauti hizi,”alisema wakati akizungumza na
wanafunzi wa Chuo Kikuu Mzumbe Morogoro, viongozi na wakazi wa vijiji jirani na
chuo.
Aidha alisema ana
matumaini kuwa mchakato wa katiba unaoendelea utaweza kuwapatia Watanzania
katiba mpya.
“Mimi naishi kwa
matumaini. Naamini kuwa tutafika mwisho vizuri. Mchakato ni mgumu lakini
barabara ndefu haikosi kona. Tukidhamiria kweli tutafika tuendako vizuri,”
alisema.
Aliwambia mamia ya
wanachuo, watumishi wengine wa chuo hicho: “Maoni yenu ndiyo maoni yangu. Ni
jambo la kusikitisha kuwa tofauti hizi za viongozi wa siasa zinaleta mfarakano
wa namna hii. Tokea mwanzo niliwaambia kuwa wakiruhusu kushindana na kuviziana
katika mchakato huo watakwama.”
“Aidha, niliwaambia kuwa Katiba inayotafutwa
siyo katiba ya CCM, ama ya CHADEMA, ama ya NCCR, ama ya CUF. Niliwaambia kuwa
hii ni katiba ya wananchi wa Tanzania. Ni vyema tukakubaliana kuwa yenye
kutugawa tukayaacha kwa sasa na kukubali kwa yale ambayo hatuna tofauti,”
alisema.
Mapema wanafunzi wa chuo
hicho waliunga mkono mchakato wa Bunge
Maalumu la Katiba wakisema wanaridhishwa na hatua iliyofikiwa na mwendo mzima wa
bunge hilo na kuwa mwafaka unawezekana kuhusu vipengele viliyobakia na
kupatikana kwa theluthi mbili za kupitisha katiba mpya.
Katika risala hiyo
iliyosomwa na Rais wa Chama cha Wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Mzumbe, Boniface
Maige Juma, wanafunzi hao walisema ni vyema mchakato huo ukaungwa mkono na kila
Mtanzania ili kuuwezesha kuleta neema na matarajio yanayokusudiwa.
“Tunaridhishwa na hatua iliyofikiwa na Bunge
Maalum la Katiba. Tunaamini kuwa mwafaka unawezekana kwa vipengele vingine vya
rasimu ya katiba. Aidha, tunaamini kuwa theluthi mbili za kupitisha katiba mpya
zinawezekana kupatikana,” alisema.
No comments:
Post a Comment