Habari za Punde

Innaa Lillaahi Wainnaa ilayhi Raajiuun :Mazishi ya Aliyekuwa Mwandishi wa Habari wa Gazeti la Zanzibar Leo Marehemu Juma Masoud

 Wananchi na Waumini wa Dini ya Kiislam wakiitikia dua baada ya kuusalia mwili wa marehemu Juma Masoud, aliefarikin jana hafla, mazishi hayo yamefanyika Kijiji kwao Bambi Wilaya ya Kati Unguja na kuhudhuriwa na Waandishi mbalimbali wa vyombo vya Serekali na Binafsi Zanzibar.

 Wananchi wakiwa wameubeba mwili wa Mwandishi Mkongwe Zanzibar Marehemu Juma Masoud, aliefariki jana  hafla katika hospitalim Kuu ya Mnazi mmoja, Marehemu amefanyakazi Redio Zanzibar, Gazeti la Nuru na kumalizia ajira yake katika gazeti la Serekali la Zanzibar Leo,  

Mhariri Mkuu (mstaafu) wa Shirika la Magazeti ya Serikali Zanzibar, linalochapisha magazeti ya Zanzibar Leo, Zanzibar Leo Jumapili na Zaspoti, Juma Massoud Ali, amefariki dunia akiwa na umri wa miaka 61.
Alifariki alfajiri ya kuamkia jana katika hospitali kuu ya Mnazi Mmoja  kutokana na kusumbuliwa na ugonjwa sukari na shinikizo la damu.
Marehemu alizikwa jana kijijini kwao Bambi wilaya ya Kati Unguja,ambapo mazishi yake yalihudhuria na maelfu ya wananchi, ndugu, jamaa na marafiki pamoja na wafanyakazi wenzake wa zamani.
Marehemu alianza kufanya kazi katika vyombo vya habari kuanzia mwaka 1975 katika  chumba cha habari cha kituo cha redio  Zanzibar (sasa ZBC redio) akiwa kama mwandishi wa habari.
Mwaka 1976, alijiunga na Chuo cha Uandishi wa Habari (TSJ) mpaka mwaka 1979 na kutunukiwa Diploma ya uandishi wa habari.
Baada ya kurudi kituo chake cha kazi, kuanzia mwaka 1994-1998 alifanya kazi magazeti ya Uhuru na Mzalendo akitokea gazeti la Nuru aliloanza nalo mwaka 1992.
Baada ya kumaliza mkataba na magazeti ya Uhuru na Mzalendo alirejea kulitumikia gazeti la Nuru na alikuwa miongoni mwa waandishi wa habari wa kwanza walioanzisha gazeti la kila siku la serikali la Zanzibar Leo mwaka 2002, Mhariri Mwandamizi.
Aliendelea kupanda cheo na baada ya kuanzishwa Shirika la Magazeti ya Serikali chini ya sheria namba 11 ya mwaka 2008, aliteuliwa kuwa Mhariri Mkuu, cheo ambacho aliendelea kukishikilia hadi alipostaafu Septemba 1, mwaka 2013.
Marehemu ameacha kizuka mmoja na watoto saba.
Mungu ailaze roho ya marehemu mahala pema peponi, Amiin.
Xxxxxxxxxxx
Wanasheria:Kamishna wa Polisi Z’bar anavunja Katiba
Wanadi amepora mamlaka ya DDP
Na Mwandishi wetu
CHAMA cha Wanasheria Zanzibar (ZLS) kimesema kitendo kinachofanywa na Kamishna wa Polisi Zanzibar cha kuwakamata watuhumiwa, kuwasafirisha na kuwafungulia mashtaka nje ya Zanzibar, kimepora mamlaka na madaraka ya kikatiba  aliyokabidhiwa Mkurugenzi wa Mashtaka wa   Zanzibar.
Aidha kitendo cha polisi kukabidhi washtakiwa kwa mamlaka zilizo nje ya Zanzibar ni kumdharau na kumkiuka Mkurugenzi wa Mashtaka.
Akizungumza na waandishi wa habari jana, Rais wa Chama hicho, Awadh Ali Said, alisema hali hiyo imesababisha watuhumiwa kukosa haki zao jambo ambalo ni uvunjifu mkubwa wa haki za binaadamu  hasa ikizingatiwa kwamba watuhumiwa hao wamekuwa wakiteswa kudhalilishwa kulikovuka viwango vya ubinaadamu, madai ambayo hayakukanushwa na mamlaka husika.
Alisema chama hicho kinalaani uvunjaji wa katiba ya Zanzibar na ukiukwaji mkubwa wa sheria za usimamizi na uendeshaji wa makosa ya jinai Zanzibar na vitendo vya udhalilishaji wanavyofanyiwa watuhumiwa.
Alisema masuala ya jinai, sheria zake, usimamizi  na uendeshaji wake sio mambo ya Muungano na ndio maana Zanzibar na Tanzania Bara kila moja ina sheria tofauti zinazosimamia utaratibu wa mwenendo wa  makosa ya jinai.
Aidha alisema pande hizo mbili zina sheria za ushahidi tofauti na ndio maana zina taasisi tofauti zinazosimamia mambo ya uendeshaji wa mashtaka ya jinai.
Alisema pamoja na Tanzania kuwa na jeshi moja la polisi, jeshi hilo kwa upande wa Zanzibar linasimamia sheria za Zanzibar na upande wa Tanzania Bara linasimamia sheria za huko.
“Na hata pale mtuhumiwa anapotuhumiwa kuvunja sheria ambayo inahusu mambo ya kimuungano, bado sheria zinazotumika kuendesha mashtaka hayo ni za Zanzibar kupitia taasisi za Zanzibar- hili limefanyiwa maamuzi kadhaa na mahakama ya Rufaa Tanzania,” alisema.
Alisema kwa upande wa Zanzibar, sheria ziko wazi kwamba jukumu la polisi ni pamoja na kuwakamata watuhumiwa wa uhalifu kufanya upelelezi wa makosa ya jinai na baadae kuwasilisha ushahidi kwa Mkurugenzi wa Mashtaka wa Zanzibar ambaye kwa mujibu wa katiba ya Zanzibar ndie pekee aliyepewa mamlaka ya kuendesha mashtaka katika mahakama za Zanzibar.
“Katiba ya Zanzibar haijatoa mwanya wowote kwa Mzanzibari anayetuhumiwa na makosa ya jinai kukamatwa na kusafirishwa nje ya Zanzibar na kumkabidhi kwa mamlaka nyenginezo ambazo hazikuidhinishwa na Katiba ya Zanzibar,” alisema.
Chama hicho kimezitaka Mamlaka zilizokabidhiwa jukumu ama la kiushauri au la kiutendaji chini ya katiba ya Zanzibar hususan Mkurugenzi wa Mashtaka, Mwanasheria Mkuu wa Zanzibar na Waziri wa Katiba na Sheria, kuchukua hatua za dharura kuhakikisha watuhumiwa waliosafirishwa nje ya Zanzibar wanarudishwa mara moja katika mahakama za Zanzibar kwa mujibu wa sheria.
Pia kimeitaka Serikali ya Zanzibat kuunda Tume Huru ya Uchunguzi itakayopewa jukumu la kuchunguza uhalali wa kikatiba na kisheria wa maamuzi wa kuwakamata watuhumiwa na kuwasafirisha nje ya Zanzibar na kuwakabidhi kwa mamlaka ambazo hazijaidhinishwa na katiba.
Aidha imeomba mamlaka itakayoundwa ichunguzi malalamiko yote ya uvunjifu wa haki za binaadamu, mateso na udhalilishaji waliyofanyiwa watuhumiwa kama walivyoyatoa mahakamani.




No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.