Na Benedict Liwenga,
Maelezo, Dodoma
Ofisi ya Bunge Maalum la
Katiba, imetoa ufafanuzi juu ya taarifa zilizotolewa kwenye vyombo vya habari
kuhusu kuchelewa kwa malipo ya posho za wajumbe wa bunge hilo.
Mkurugenzi wa Habari na
Itifaki, Jossey Mwakasiyuka, alitoa ufafanuzi huo wakati akizungumza na waandishi
wa habari kwa lengo la kutoa ufafanuzi kuhusiana na taarifa hizo, ambazo
alisema zimelikera bunge la katiba.
Alisema ofisi ya Bunge
Maalum imekerwa na kuchapishwa kwa taarifa hizo kwani ni za upotoshaji na zina
lengo la kuwadhalilisha wajumbe na kuwafanya waonekane wenye kuishi na kufanya
kazi kwa kutegemea posho wanazolipwa.
“Ni vyema ikaeleweka
kwamba wajumbe wa bunge maalum wote ni watu wenye nafasi zao katika jamii na ni
wenye kazi au shughuli zao mahususi zinazowaingizia kipato na kwamba ujumbe wa bunge
maalum ni nafasi ya muda tu ya kutimiza jukumu la kuliandalia taifa katiba kpya,”
alisema.
Alisema si vyema kwa
vyombo vya habari kuwadhalilisha wajumbe hao kwa njia yoyote ile kwani kwa
kufanya hivyo kunawavunja moyo na kuwafanya washindwe kuifanya kazi ya bunge maalum
vizuri kama ilivyotarajiwa na wananchi.
Akifafanua kuhusiana na
malipo ya posho hizo, aliviambia vyombo vya habari kuwa, wajumbe wote wa bunge maalum
ambao wanahudhuria vikao vinavyoendelea wamelipwa posho zao zote kama
wanavyostahili.
“Ni vyema ikaeleweka
kwamba malipo ya posho yanafuata taratibu za fedha za umma na yanapita mchakato
maalum unaojumuisha kupata orodha za mahudhurio ya wajumbe kwenye kikao,
upatikanaji wa fedha kutoka hazina, na upatikanaji wa fedha kutoka benki, hivyo
wakati mwingine huchukua siku kadhaa hadi kukamilika,” alisema.
Alivitahadharisha vyombo
vya habari vinavyondika habari za Bunge Maalum kuzingatia maadili na kanuni za uandishi
wa habari zinazotolewa katika vikao vya bunge maalum ili taarifa kama hizo za
upotoshaji zisijirudie tena.
“Kumbukeni kuwa wajibu
wenu ni kuhabarisha umma na sio kupotosha umma na hata kuleta usumbufu kwa
jamii kutokana na uandishi usio makini,” alisema.
Katika kanuni za bunge maalum,
kanuni ya 77 inawataka waaandishi wa habari kuandika habari za bunge maalum kwa
weledi mkubwa kwa kuzingatia maadili ya uandishi wa habari ili kuondoa uandishi
wenye kuleta chuki kati ya serikali na wananchi wake.
Ukweli hasa hizi posho bora ziondoshwe hili bunge maalum lipate kwisha , zikisitishwa tu makubaliano yatapatikana . Na pesa hizo zote zitumike kwa mengine ya maana , likes , madeksi ya maskuli , magodoro ya hospitali , wasisubiri misaada tu
ReplyDelete