Habari za Punde

Zaidi ya kilo 2,000 za samaki wa kufuga zakosa soko

Na Rehema Mohamed, Pemba
USHIRIKA wa ufugaji samaki cha Chambani unakabiliwa na tatizo la soko la kuuzia samaki wao, ambapo kwa sasa wana zaidi ya kilo 2,000 za samaki.

Kilo moja ya samaki inauzwa kati ya shilingi 7,500 na 8,000, lakini kwa sababu ya ukosefu wa soko la uhakika wanalazimika kuuza kilo moja kwa shilingi 2,000 hadi shilingi 2,500.

Akizungumza na mwandishi wa habari hizi kijijini kwao Chambani, Katibu wa Ushirika huo, Nassor Suleiman Nassor, alisema wakati mwengine hata bei ya shilingi 2,000 kwa kilo moja, huikosa na baadhi ya samaki huwagawa kwa wanachama.

Alisema pamoja na kuanzisha ushirika huo kwa lengo la kujikwamua na hali ngumu ya maisha, bado wanakumbana na hali gumu kutoka na ukosefu wa soko.


Alisema ushirika wao wenye wanachama zaidi ya 20, umeanzisha mradi wa ufugaji samaki ambao kwa kiasi kikubwa umepata mafanikio lakini tatizo kubwa ni soko.

Samaki wanaofugwa ni mwatiko, mizira na chaa na wanatarajia kuongeza samaki wa aina nyengine ambao wanakubaliana na hali yoyote ya hewa katika kipindi cha kiangazi.

Mwenyekiti wa ushirika, Said Omar Haji, alisema wamekuwa wakivuna samaki mara mbili ambapo, wastani wa kilo 4,000, kila mwaka hupatikana.


Mwenyekiti huyo alisema mafunzo ya ufugaji samaki aliyapata China na aliporudi aliwafundisha wenzake mbinu za ufugaji wa kisasa wa samaki.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.