Na Mwandishi wetu
TANZANIA iko tayari
kushirikiana na wanachama wote wa Umoja wa Mataifa (UN) kufikia makubaliano ya
Malengo ya Maendeleo mapya baada ya Malengo ya Milenia (MDGs) ya sasa kufikia mwisho
wake ifikapo mwaka 2015.
Rais Kikwete alisema hayo
wakati akihutubia Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa (UNGA) jijini New York,
Marekani.
Agenda ya kikao cha Baraza Kuu
la UN mwaka huu ni "Delivering on and Implementing a Transformative Post
2015 Development Agenda" ambapo alisema anatarajia majadiliano yatatoa
nafasi kwa nchi kupanga mipango ya baadae kwa manufaa ya vizazi vijavyo.
"Tutumie muda huu
kuendeleza mafanikio na mafunzo kutoka nchi mbalimbali na pia tujifunze
kutokana na changamoto za kushindwa kufikia malengo ya milenia, na kuzitumia
kama viashiria vya ajenda ya maendeleo baada ya mwaka 2015," alisema.
Aliiasa dunia kuwa wakati huu
ambapo inajadili ajenda ya maendeleo baada ya mwaka 2015, isisahau malengo ya
milenia ambayo hayajakamilika na kuyaweka vizuri katika ajenda mpya ya baada ya
malengo ya sasa kufikia tamati mwaka ujao.
Pamoja na kwamba dunia
inazungumzia ajenda mpya ya baada ya mwaka ujayo, alizitaka nchi kuhakikisha na
kuongeza kasi ya utekelezaji katika kipindi cha siku 461 zilizobakia kufikia
mwisho.
Pamoja na umuhimu wa MDGs Rais
Kikwete alizungumzia suala la tabianchi na kuzitaka nchi zote duniani kukusanya
nguvu katika suala hilo ili kuiokoa dunia kutokana na majanga ya tabianchi.
Masuala mengine ni kuhusu mageuzi
katika UN, ambapo alisema kusuasua kwa mazungumzo ya kuleta mageuzi kunakatisha
tamaa na kuomba yafufuliwe.
Masuala mengine ni kuhusu hali
ya usalama duniani ambapo ugaidi umechukua mkondo wa kutishia amani duniani na
kuzitaka nchi zote kupambana na ugaidi.
Masuala mengine ni uhasama
baina ya Israeli na Palestina ambalo limedumu kwa muda mrefu hivyo kuutaka
Umoja wa Mataifa kulitafutia suluhu ya kudumu; suala la Sahara Magharibi ambalo
pia limedumu kwa muda mrefu bila ufumbuzi na vikwazo kwa Cuba ambavyo navyo vimekuwepo kwa
muda mrefu sana.
Alizungumzia ugonjwa wa Ebola
ambao tayari umeua watu wapatao 2,400 na bado haujadhibitiwa.
Alisema ugonjwa wa Ebola ni
tishio kwa nchi zilizoathirika, jirani na dunia kwa ujumla hivyo, juhudi za
pamoja zinahitajika kwani ndio njia sahihi ya kuutokomeza.
No comments:
Post a Comment