Habari za Punde

Sita atangaza Ratiba ya kutafuta katiba mpya


MWENYEKITI wa Bunge Maalum la Katiba, Mhe. Samuel Sitta amesoma ratiba kamili ya mchakato wa katiba mbele ya wajumbe ili kuhakikisha kuwa malengo ya upatikanaji wa katiba hiyo yanafikiwa.

Mhe. Sitta ametoa ratiba hiyo siku ya tarehe 15 Septemba mwaka huu akisema kuwa siku ya Jumatano ya tarehe 17 Septemba, 2014 kutakuwa na Semina ambayo mtoa mada atakuwa ni Mzee Kingunge Ngombale Mwiru na mada kuu ya semina hiyo itahusu dhana yote ya Ukombozi wa Mwafrika na nafasi ya Tanzania katika Ukombozi kuanzia Ukoloni hadi kufikia vita vya ukombozi za Kusini mwa Afrika na kufikia katika ukombozi wa aina ya tatu ambao ni uchumi pamoja na nafasi ya Tanzania kuwa mstari wa mbele katika kuleta dhana mpya ya ukombozi wa kiuchumi kwa Watanzania.

Sitta ameongeza kuwa siku ya Alhamisi ya tarehe 18-20 siku hizo zitaachwa kwa jili ya Kamati ya Uandishi kuweza kutulia na kufanyia kazi michango ya wajumbe kwa muda wa siku tatu.

Aidha, siku ya tarehe 21 Jumamosi, Kamati ya Uongozi itaketi ili kuona namna ilivyokaa Rasimu ya mwisho, ambapo tarehe 22 siku ya Jumatatu, Kamati ya Uandishi itawasilisha bungeni hapo Rasimu hiyo kwa muda wa Nusu siku ambapo wajumbe watapewa muda wa kuitafakari rasimu hiyo siku ya Jumatatu na Jumanne.

“Siku ya tarehe 24 na 25 yaani Jumatano na Alhamisi, Wajumbe wa bunge hilo watakuwepo bungeni hapo kwa muda wa siku zote mbili kwa lengo ya kufanya kazi ya kuhakiki na sio kufungua upya mjadala, uhakiki huo unamaanisha kupata kujua juu ya yale waliyokubaliana kama kweli yamo kisha badala ya uhakiki huo, watarejesha kwa kamati ya uandishi ili ifikapo siku ya tarehe 26 kamati hiyo iweze kufanya kazi ya kurekebisha kulingana na yale wajumbe watakayowaambia kamati hiyo”, alisema Mhe. Sitta.

Septemba, 27 Kamati ya Uandishi itawasilisha kwa mara ya pili Rasimu iliyoboreshwa.“Tunataka kitu kizuri hapa ndo mana tunakwenda kwa uangalifu, hapa itawasilishwa Rasimu inayoitwa Rasimu ya mwisho na nawaombeni sasa mkishaipata mtakuwa nayo, mnaweza kusema maneno machache pale lakini tunakuombeni siku ya Jumapili siku ya tarehe 28, tafadharini wajumbe wote wa bunge Maalum mtaingia kwenye kamati zenu saa Nne asubuhi, malengo ni mawili, moja ni kujiridhisha jinsi ilivyokaa sasa rasimu, itakuwa kama semina kwa kila kamati kuelekezwa juu ya namna ya kupiga kura”, alisisitiza Mhe. Sitta.

Kura zitaanza kupigwa siku ya Jumatatu ya tarehe 29 saa tatu asubuhi kwa kuanza na Ibara ya kwanza mpaka ya mwisho pasipo kubadilishwa badilishwa ambapo zoezi hilo linatazamiwa kumalizika kati ya tarehe mbili au tatu asubuhi.

“Itakuwa ni zawadi nzuri sana kwa Rais wetu Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete kama tutamaliza zoezi hili tarehe tatu ili tuwe na Katiba inayopendekezwa”, alisema Mhe. Sitta.

Imeandikwa na Benedict Liwenga, Dodoma/Tanzania Government Blog

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.