Habari za Punde

Balozi Seif Azungumza na Mwakilishi wa Kampuni ya Ms Shimoja. ya Marekani

Balozi wa Heshima wa Tanzania Nchini Marekani ambae pia ni Mkurugenzi wa Kampuni ya Ms Shimoja ya Nchini Marekani Dr. Robert Shumake akisalimiana na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi Ofisini kwake iliyopo katika Jengo la Msekwa ndani ya Viunga vya Bunge la Jamuhuri nya Muungano wa Tanzania Mjini Dodoma.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif akibadilishana mawazo na Balozi wa Heshima wa Tanzania Nchini Marekani ambae pia ni Mkurugenzi wa Kampuni ya Ms Shimoja  ya Nchini Marekani Dr. Robert Shumake Bungeni Mjini Dodoma.(Picha na – OPMR)
Na Othman Khamis. OMPR 
Kampuni ya Ms Shimoja  yenye Makao Makuu yake katika Jimbo la Michigan  Nchini Marekani iko mbioni kutaka kuanzisha kituo cha Matangazo ya Televisheni Mjini Dar es salaam Nchini Tanzania kitakachotoa huduma ndani ya Ukanda wa Afrika Mashariki.
Mkurugenzi wa Kampuni hiyo ambae pia ni Balozi wa Heshima wa Tanzania Nchini Marekani Dr. Robert Shumake alieleza hayo wakati akizungumza na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi Ofisini kwake katika Jengo la Msekwa ndani ya viunga vya Bunge la Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Mjini Dodoma.
Dr. Shumake alisema licha ya kwamba matangazo ya Televisheni yanachukuwa sehemu kubwa ya burdani lakini Kituo hicho kitalenga zaidi kutoa vipindi wa Elimu vitakavyowasaidia wananchi na hasa wanafunzi wa elimu ya msingi, sekondari na vyuo vikuu Afrika Mashariki.
Alisema mipango inaandaliwa na Kampuni hiyo katika kuyashirikisha Makampuni ya Mitandao ya Mawasiliano Duniani ya Google na Microsoft ili kuona Elimu inayokusudiwa kufikishwa kwa umma kupitia matangazo ya Kituo hicho yanafanikiwa kwa kiwango kikubwa.

Dr. Shumake alifahamisha kwamba mpango huo unakusudiwa kwenda sambamba na ule utakaoandaliwa na Kampuni hiyo wa kuwapatia mafunzo vijana wapatao 50,000 kutoka Bara la Afrika katika Jimbo la Michigan Nchini Marekani.
Alisema hatua hiyo inakusudia kuwajengea uwezo wa ajira vijana hao katika fani ya  ujasiri amali utakaowapa fursa nzuri ya kufanya kazi katika taasisi na mashirikia yoyote ya Kitaifa na Kimataifa.
“ Tumejipanga kuwapatia mafunzo maalum viiana wa Bara la Afrika ili kusaidia kupunguza wimbi la vijana wasio na ajira ndani ya Bara hili “. Alifafanua Balozi huyo wa Heshima wa Tanzania Nchini Marekani Dr. Shumake.
Naye Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alimshukuru Dr. Robert  Shumake pamoja na Kampuni yake kwa uamuzi huo wa busara utakaowezesha kuisaidia pia Serikali katika mapambano dhidi ya uhaba wa ajira Nchini.
 Balozi Seif alisema Serikali zote mbili ile ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania na ya Mapinduzi ya Zanzibar zimeweka milango wazi kwa taasisi na mashirika ya Kitaifa na Kimataifa kuwekeza miradi yao kwa kutumia rasilmali zilizopo nchini ili kusaidia nguvu za kiuchumi na kupunguza ukali wa maisha.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar alimshauri Mkurugenzi huyo wa Kampuni ya Ms Shimoja ya Nchini Marekani kuangalia fursa nyingi zaidi  za uwekezaji zilizopo Nchini Tanzania ambazo Kampuni yake inaweza kuongeza uwekezaji zaidi.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.