Habari za Punde

Shirika la ndege la Rwanda kuanzisha safari za Zanzibar


 
STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY

PRESS RELEASE

  Zanzibar                                                                           6.2.2015

---

SHIRIKA la ndege la Rwanda linampango wa kuanzisha safari zake kati ya Zanzibar na Rwanda ikiwa ni njia moja wapo ya kukuza uhusiano na ushirikiano uliopo sambamba na kuimarisha na kukuza sekta za biashara na utalii kati ya nchi mbili hizo.
 
 Balozi wa Rwanda nchini Tanzania Mhe. Eugene Kayihura aliyasema hayo wakati alipofanya mazungumzo na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dk. Ali Mohamed Shein, Ikulu mjini Zanzibar.
 
Katika maelezo yake, Balozi Kayihura alimueleza Dk. Shein kuwa tayari Shirika la Ndege la Rwanda linafanya safari kati ya nchi za Afrika Mashariki ikiwemo Tanzania katika mikoa ya Arusha, Mwanza na Dar-es-Salam hivyo haoni sababu ya kutofanya safari za kuja Zanzibar.
 
Alisema kuwa Shirika hilo lina sababu mbali mbali za kufanya safari zake hapa Zanzibar hasa ikizingatiwa kuwa  Rwanda hivi sasa imo katika mchakato mkubwa wa kukuza sekta ya utalii na biashara hivyo hatua hiyo itasaidia kuimarisha sekta hizo.
 
Balozi Kayihura alisema kuwa wapo watalii wanaotembelea Rwanda, Uganda na Kenya ambao hutumia Shirika hilo la ndege kwa safari zao hizo za kitalii, hivyo itakuwa ni jambo la busara kuunganisha safari hizo na Zanzibar hasa ikizingatiwa kuwa Zanzibar imepiga hatua kubwa kitalii pamoja na kuwepo vivutio vingi vya kitalii.

 
Aidha, alisema kuwa Rwanda ina mambo mengi ya kujifunza na kupanua wigo kutoka Zanzibar kutokana na mafanikio makubwa yaliopatikana katika sekta ya utalii ambapo pia, alisisitiza kuwa mbali ya sekta hiyo, sekta ya biashara nayo inaweza kuimarika pale safari za Shirika hilo zitakapoanza kati ya Rwanda na Zanzibar.
 
Alieleza kuwa hivi sasa wafanyabiashara wengi wa nchi za Congo, Garbon na nyenginezo zilizopo Afrika ya Kati wanataka kuja Zanzibar kwa lengo la kufanya biashara hivyo kuaza kwa safari za Shirika hilo kutawawezesha kufikia lengo lao.
 
Sambamba na hayo, Balozi huyo alieleza kufurahishwa kwake na mafanio yaliopatikana hapa Zanzibar hasa katika sekta ya Utalii na kupongeza juhudi zinazochukuliwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar chini ya uongozi wa Dk. Shein katika kufanikisha sekta hiyo.
 
Pamoja na hayo, Balozi huyo wa Rwanda alisema kuwa nchi yake imo katika hatua za kuimarisha uhusiano na ushirikiano kati yake na Zanzibar hasa  katika sekta ya elimu huku akikisisitiza kuwa Rwanda iko tayari kutoa ushirikiano wake katika suala zima la mafunzo katika mazingira sambamba na kueleza siri ya mafanikio hayo.
 
Nae Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa  Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein alisema kuwa Zanzibar inathamini uhusiano na ushirikiano uliopo kati ya Rwanda na Zanzibar ambao ni wa muda mrefu.
 
Dk. Shein alisema kuwa kuanza kwa safari za Shirika la Ndege la Rwanda hapa Zanzibar kutasaidia kuimarisha na kukuza sekta hizo za maendeleo huku ikizingatiwa kuwa watu wengi waliopo Zanzibar na wale wa Rwanda wana hamu ya kutembeleana na kukuza uhusiano wao lakini kinachowakwanza ni suala zima la usafiri.
 
Akizungumza ushirikiano katika sekya ya elimu, Dk. Shein alisema kuwa Zanzibar imebarikiwa kuwa na Chuo kikuu chake ambacho ndani yake mna Taasisi ya Lugha za Kigeni hivyo miongoni mwa lugha zinazofundishwa ni Kiswahili na Kifaransa.
 
Kutokana na hali hiyo, itakuwa ni jambo la busara kwa nchi ya Rwanda kuleta vijana wake ili kujifunza Kiswahili na kwa upande wa Zanzibar kupeleka vijana wake ili waende kujifunza kifaransa nchini humo hatua ambayo itaimarisha uhusiano na ushirikiano sambamban na kuweza kubanilishana uzoefu.
 
Pamoja na hayo, Dk. Shein alimueleza Balozi Kayihura kuwa kutokana na Rwanda kupiga hatua katika suala zima la usafi wa mazingira, Zanzibar inampango wa kupanua wigo kutokana na mafanikio hayo kupitia Baraza lake na Manispaa pamoja na Idara husika ya Mazingira iliyopo chini ya Afisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais kwenda kujifunza kwa kuona hatua zilizofikiwa na Rwanda na hatimae kupata mafanikio hayo.
 
“Lazima tujifunze kupitia sisi wenyewe kati nchi zetu hizi kwani Rwanda imepiga hatua kubwa sana katika suala zima la usafi wa mazingira”,alisema Dk. Shein.
 
Aidha, Dk. Shein alisisitiza kuwa Zanzibar itaendelea kuimarisha uhusiano na ushirikiano kati yake na Rwanda.
 

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.