Habari za Punde

Wananchi watakiwa kulipa kodi kwa mujibu wa sheria ili serikali iweze kutekeleza majukumu yake


 

 

STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY

PRESS RELEASE

  Zanzibar                                                                                                           19.02.2015

---

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dkt. Ali Mohamed Shein amesisitiza umuhimu wa wafanyabiashara na wananchi wote kwa jumla kuendelea kulipa kodi kwa mujibu wa sheria za nchi ili kuiwezesha Serikali kutekeleza majukumu yake ipasavyo ikiwemo kutekeleza miradi ya maendeleo na kutoa huduma bora kwa wananchi.

 

Akizungumza na uongozi wa Wizara ya Fedha Zanzibar katika mkutano wa kutathmini utekelezaji wa mpango kazi na bajeti ya Wizara ya Fedha Zanzibar huko Ikulu leo, Dk. Shein amesema hakuna namna ambayo itaiwezesha Serikali kufanya kazi zake kwa ufanisi bila ya kuwa na nyenzo ya fedha ambazo upatikanaji wake unatokana na makusanyo ya kodi.

 

“hakuna namna ya kuendesha serikali bila ya mapato yanayotokana na kodi, na suala hili ni la kihistoria halikuanza leo, kila mtu ni lazima alipe kodi kwa mujibu wa sheria”, alisisitiza.

 

Rais wa Zanzibar ametumia fursa hiyo kuipongeza Wizara ya Fedha kwa kusimamia vyema ukusanyaji wa mapato ya ndani katika kipindi cha miezi sita Julai – Disemba 2014, ambapo jumla ya Shilingi 175,659 milioni sawa na asilimia 91 ya makadirio ya miezi sita zilikusanywa.

 

Fedha hizo zinajumuisha mapato ya kodi ya TZS 86,185 milioni yaliyokusanywa na Bodi ya Mapato ya Zanzibar ZRB ambayo ni sawa na asilimia 96 ya makadirio na  TZS 70.402 yaliyokusanywa na Mamlaka ya Kodi Tanzania  TRA kwa upande wa Zanzibar ambayo ni sawa na asilimia 86 ya makadirio.

 

Makusanyo hayo pamoja na makusanyo mengine yasiyokuwa ya kodi katika kipindi cha miezi sita iliyopita yameonesha ongezeko la asilimia 12 ikilinganishwa na makusanyo ya kipindi kama hicho mwaka uliopita.

 

Vile vile Rais wa Zanzibar ameipongeza Wizara hiyo kwa kuweza kusimamia vyema ugawaji na matumizi ya fedha hizo ambazo kwa mujibu wa taarifa za Wizara zote zilizowasilisha taarifa zake kwenye vikao hivyo zimeonesha mafanikio makubwa ya utekelezaji kifedha.

 

Akizungumzia maendeleo ya utekelezaji wa mradi wa huduma za jamii Zanzibar (ZUSP), Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi ameelezea kuridhishwa kwake na hatua ya utekelezaji wa mradi huo, ambao unajumuisha kazi kadhaa ikiwemo kazi za ujenzi wa njia za kupitishia maji ya mvua, taa za mjini na ukarabati wa ofisi ya Baraza la Manispaa.

 

Hata hivyo, ametoa wito wa kuandaliwa utaratibu maalum wa kuwasilisha taarifa hizo kwa wananchi, kwani alisema bado baadhi ya wananchi hawana taarifa za kutosha juu ya maendeleo ya mradi huo.

 

Amefahamisha kuwa wananchi wamekuwa wakisubiri kwa hamu kukamilika kwa mradi huo kutokana na ahadi walizoahidiwa na viongozi mbali mbali, hivyo ni vyema wakaarifiwa ipasavyo kuhusiana na maendeleo yake.

 

Akiwasilisha taarifa ya Wizara yake, Waziri wa Fedha Mheshimiwa Omar Yussuf Mzee amesema pamoja na mafanikio makubwa yaliyopatikana na Wizara yake, bado wanakabiliwa na changamoto ya kutotabirika kwa mapato yasiyokuwa ya kodi na mapato yatokanayo na misaada na hivyo kupelekea ugumu wa kujua muda na kiasi cha fedha ambacho kitapatikana kila mwezi.

 

Changamoto nyengine ni kwa baadhi ya walipa kodi kushindwa kuwajibika kulipa kodi ipasavyo na kuongezeka matumizi ya dharura yasiyokuwemo katika bajeti ya Serikali ya mwaka 2014/2015.

 

Hata hivyo amesemam changamoto hizo zote zimo ndani ya uwezo wa Wizara na zinaendelea kupatiwa ufumbuzi.

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.