Habari za Punde

Dk Shein akutana na Balozi wa Uholanzi nchini

 Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein akizungumza na Balozi wa Jamhuri ya Uholanzi nchini Tanzania Mhe,Jaap Fredriks alipofika Ikulu Mjini Zanzibar leo,[Picha na Ikulu.]
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein akifuatana na mgeni wake  Balozi wa Jamhuri ya Uholanzi nchini Tanzania Mhe,Jaap Fredriks alipofika Ikulu Mjini Zanzibar leo baada ya mazungumzo yao,[Picha na Ikulu.]

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein akiagana na mgeni wake  Balozi wa Jamhuri ya Uholanzi nchini Tanzania Mhe,Jaap Fredriks alipofika Ikulu Mjini Zanzibar leo baada ya mazungumzo yao,[Picha na Ikulu  
STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
  Zanzibar                                                                                                           2.3.2015
---
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein amesema kuwa hatua za mwanzo zinazoendelea katika ujenzi wa wodi mpya ya mama wajawazito na watoto katika hospitali ya Kuu ya Mnazi Mmoja chini ya Mradi wa ORIO zinaleta matumaini katika kuimarisha sekta ya afya hapa nchini.
 
Dk. Shein aliyasema hayo katika mazungumzo kati yake na Balozi wa Uholanzi nchini Tanzania Mhe. Jaap Fredriks yaliyofanyika Ikulu mjini Zanzibar.
 
Katika mazungumzo hayo Dk. Shein aliipongeza Serikali ya Uholanzi kwa hatua yake ya kuunga mkono juhudi hizo za ujenzi wa wodi hiyo mpya chini ya Mpango wa ORIO ambapo alisema hatua hiyo inaonesha azma ya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kuimarisha sekta ya afya na kukuza huduma kwa jamii.
 
Dk.Shein alisema kuwa hatua za awali za ujenzi huo zimekuwa zikienda vizuri na kueleza matumaini yake makubwa ya kukamilika kwa mradi huo kwa wakati uliopangwa ili uweze kuleta manufaa kwa wananchi sambamba na kukuza sekta ya afya.
 
Aidha, Dk. Shein alisema kuwa mashirikiano hayo yanayotolewa na Serikali ya Uholanzi katika ujenzi wa wodi hiyo mpya ya akina mama na watoto yatasaidia zaidi katika kufikia lengo la Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia Wizara yake ya Afya ya kuifanya hospitali ya Mnazi Mmoja kuwa ya rufaa.
 

Dk. Shein pia, alitumia fursa hiyo kutoa pongezi kwa Uholanzi kwa kuendelea na juhudi zake za kuunga mkono na kutoa ushirikiano wake katika utekelezaji wa Mradi wa ORIO katika ujenzi wa Kiwanda cha dawa na vituo vya afya hapa Zanzibar.
 
Sambamba na hayo, Dk. Shein alipongeza azma na utayari wa Uholanzi wa kuendelea kutoa mafunzo kwa wataalamu mbali mbali juu ya sekta ya nishati hapa nchini kwa kutegemea mahitaji ya serikali.
 
Dk. Shein alitumia fursa hiyo kutoa pongezi kwa Uholanzi kwa kuendelea kuiunga mkono Zanzibar katika kuimarisha sekta mbali mbali za maendeleo na kuahidi kuwa Zanzibar itaendelea kuimarisha uhusiano na ushirikiano wake kati yake na Uholanzi.
 
Nae Balozi wa Uholanzi nchini Tanzania Mhe. Jaap Fredriks alimueleza Dk. Shein juhudi zinazochukuliwa na Uholanzi katika kuhakikisha mradi huo wa ujenzi wa wodi mpya unakwenda vizuri ili kufikia lengo lililokusudiwa.
 
Alisema kuwa Uholanzi itaendelea kuiunga mkono Zanzibar katika kuimarisha sekta zake za maendeleo ikiwemo sekta ya afya na nyenginezo kwa kutambua malengo yake ya kukuza uchumi wake na kuimarisha sekta za kijamii sambamba na kupambana na umasikini.
 
Balozi Fredriks, alisema kuwa Uholanzi kupitia Mradi wake wa ORIO utahakikisha mradi huo wa ujenzi wa wodi mpya ya akina mama na watoto unaleta tija kwa Serikali na wananchi kwa jumla hasa akina mama na watoto ambao ndio walengwa wakuu.
 
Pamoja na hayo, Balozi huyo wa Uholanzi katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania alisema kuwa mbali ya Mradi huo Serikali ya Uholanzi pia, inaendelea kuunga mkono ujenzi wa Kiwanda cha Madawa na vituo vya Afya kupitia Mradi wake huo wa ORIO.
 
Kwa upande wa vituo vya Afya, Balozi Fredriks alisema kuwa juhudi za makusudi zinachukuliwa na Ubalozi wake katika kuangalia utekelezaji huo unafanikiwa vyema kwa upande wa Unguja na Pemba.
 
Nae Mratibu wa Kanda anaeshughulikia nishati kwa nchi ya Tanzania na Msumbiji Bibi Marijn Noordam alimueleza Dk. Shein  azma na utayari wa Uholanzi wa kuendelea kutoa mafunzo kwa wataalamu wa Zanzibar juu ya sekta ya nishati.
 
Alisema kuwa tayari mipango maalum imeshawekwa juu ya utoaji wa mafunzo hayo kwa kutegemea mahitaji ya Serikali.
 
Uholanzi na Zanzibar zimekuwa na mahusiano mazuri na ya kihistoria ambapo mahusiano hayo na ushirikiano huo uliimarika zaidi pale Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein alipofanya ziara nchini humo mnamo mwezi Ogasti mwaka juzi.
 
Katika ziara yake hiyo Dk. Shein alifanya mazungumzo na viongozi mbali mbali wa Serikali ya Uholanzi pamoja na wakuu wa Kampuni za kibiashara, Watanzania wanaoishi nchini humo na kutembelea sehemu za kihistoria.
 
Wakati huo huo, mnamo Februari 20 mwaka jana Waziri wa Biashara za Nje na Ushirikiano wa Maendeleo Bibi Lilianne Ploumen alifika nchini akiongoza ujumbe wa wawakilishi wa Makampuni 25 ya kibiashara ya Uholanzi.
 
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.