STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar
10.3.2015
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la
Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amesema kuwa juhudi zinazochukuliwa na Serikali
za Kuwait, India na Oman katika kuwaunga mkono ndugu zao wa Zanzibar katika kuimarisha
sekta za maendeleo ni chachu ya kuendeleza uhusianio na ushirikiano wa
kihistoria uliopo kati ya Zanzibar na nchi hizo.
Dk. Shein
aliyasema hayo leo huko Ikulu mjini Zanzibar kwa nyakati tofauti wakati alipofanya mazungumzo na Balozi mpya wa
Kuwait nchini Tanzania Mhe. Jasem Ibrahim Al Najem, Balozi Mdogo mpya wa India
aliyepo Zanzibar Mhe. Satender Kumar na Mhe. Ali Abdulla Al-Rashdi Balozi mdogo
mpya wa Oman aliyepo Zanzibar.
Katika mazungumzo
kati yake na Balozi wa Kuwait nchini Tanzania, Mhe. Jasem Ibrahim Al Najem, Dk. Shein alisema kuwa Kuwait imekuwa mshirika mzuri katika
kuisaidia Tanzania ikiwemo Zanzibar hatua ambayo imeianza kwa muda mrefu.
Dk. Shein alisema
kuwa nchi hiyo imeweza kusaidia sekta mbali mbali zikiwemo miundombinu ya
mawasialiano ya barabara, madaraja, maji safi na salama, elimu na sekta
nyenginezo kwa pande zote za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Mfuko wa
fedha wa nchi hiyo.
Aidha, Dk. Shein
alimpongeza Balozi huyo kwa kuteuliwa kuja kuifanyia kazi nchi yake hapa
Tanzania na kutumia fursa hiyo kutoa shukurani zake kwa Balozi huyo kwa azma
yake ya kuitangaza Zanzibar nchini mwake kupitia makampuni kadhaa ya uwekezaji.
Sambamba na hayo,
Dk. Shein alitumia fursa hiyo kuwakaribishwa wawekezaji kutoka nchini Kuwait
kuja kuekeza katika sekta mbali mbali hapa Zanzibar zikiwemo viwanda, uvuvi,
utalii na nyenginezo.
Dk. Shein alimueleza
Balozi Jasem Ibrahim Al Najem mafanikio
yaliopatikana Zanzibar katika sekta ya utalii ambayo ndio sekta muhimu na inayochangia
kwa kiasi kikubwa pato la taifa sambamba na juhudi za Serikali inazozichukua katika
kuiimarisha sekta hiyo ili izidi kuimarika.
Pamoja na hayo,
Dk. Shein alimueleza Balozi huyo mafanikio yaliopatikana katika kuuimarisha Muungano
wa Tanganyika na Zanzibar unaofikia miaka 51 tangu kuasisiwa kwake ambao ni wa
kupigiwa mfano katika bara la Afrika sambamba na kumueleza mafanikio
yaliopatikana katika Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar yenye muundo wa Serikali
ya Umoja wa Kitaifa anayoiongoza hapa Zanzibar.
Nae Balozi Al
Najem alimueleza Dk. Shein jinsi nchi hiyo inavyothamini uhusiano na
ushirikiano uliopo kati ya Zanzibar na Kuwait na kusisitiza kuwa nchi yake
itaendelea kuiunga mkono Zanzibar na Tanzania kwa jumla ili kukuza uhusiano na
ushirikiano huo.
Balozi huyo
alieleza kuwa Kuwait ni mshirika mzuri wa maendeleo hapa Tanzania hatua ambayo
imeweza kusaidia kwa kiasi kikubwa kuimarisha sekta za maendeleo katika Jamhuri
ya Muungano wa Tanzania.
Katika maelezo
yake, Balozi huyo alimueleza Dk. Shein kuwa juhudi za makusudi zitachukuliwa na
Kuwait katika kuhakikisha wawekezaji
kutoka kampuni mbali mbali za nchini humo wanafika Zanzibar kuangalia maeneo ya
kuekeza.
Alisema kuwa tayari
Kuwait kupitia wawekezaji na wafanyabiashara kutoka nchi hiyo wanafanya
shughuli zao katika nchi za Afrika ikiwemo Kenya, Afrika Kusini na nyenginezo,
hivyo kuna haja ya kuja kufanya shughuli zao kama hizo hapa Zanzibar.
Wakati huo huo, Dk. Shein alifanya mazungumzo na Balozi mdogo
mpya wa India anayefanya kazi zake hapa Zanzibar Mhe. Satendar Kumar ambapo
katika mazungumzo hayo viongozi hao wameahidi kuendeleza uhusiano na
ushirikiano wa muda mrefu kati ya pande mbizi hizo.
Dk. Shein kwa
upande wake aliipongeza Serikali ya India kwa kuendelea kuiunga mkono Zanzibar
katika kuimarisha sekta mbali mbali za maendeleo ikiwemo sekta ya afya, elimu,
kilimo na nyenginezo.
Kwa upande wa
sekta ya afya, Dk. Shein alimueleza Balozi huyo mashirikiano mazuri yaliopo kati ya Zanzibar
na India hasa kufuatia ziara aliyoifanya Februari, 2014 ambapo mambo kadhaa ya
kimaendeleo yalijadiliwa kati yake na viongozi wa nchi hiyo ukiwemo utiaji
saini kati ya Zanzibar na hospitali ya Manipal iliyopo Bangalore nchini India.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la
Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein pia, alikutana na Balozi Mdogo mpya wa Oman anayefaya kazi zake hapa Zanzibar Mhe.Ali
Abdulla Al Rashdi na kufanya nae mazungumzo yaliyojikita zaidi katika
kuimarisha uhusiano na ushirikiano wa kihistoria kati ya Zanzibar na Oman.
Katika mazungumzo
hayo, Dk. Shein alitoa pongezi kwa Serikali ya Oman chini ya kiongozi wake
Sultan Qaboos Bin Said Al Said kwa kuiunga mkono Zanzibar katika kuimarisha
sekta mbali mbali za maendeleo ikiwemo sekta ya afya kwa msaada wake mkubwa wa
ujenzi wa Chuo cha Afya, hapa Zanzibar.
Balozi huyo wa
Oman aliahidi kuendeleza ushirikiano na uhusiano kati ya Zanzibar na Oman hasa
katika uimarishaji wa sekta za maendeleo huku akisisitiza azma ya nchi yake ya
kuendelea kuiunga mkono Zanzibar hasa katika sekta ya afya na uvuvi sambamba na
kusaidia vifaa kwa ajili ya Kiwanda cha Uchapaji cha Serikali.
Rajab
Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024
2231822
E-mail:
rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment