Habari za Punde

Rais Dk Shein Azungumza na Balozi wa Algeria Ikulu Zanzibar

STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
  Zanzibar                                                                                                                         29.8.2015
---
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein amesema kuwa Algeria na Tanzania ni nchi zenye historia katika uhusiano na ushirikiano wao ulioanzishwa na waasisi wa nchi hizo Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere pamoja na Rais wa kwanza wa Algeria Mhe. Ahmed Ben Bella.

Dk. Shein aliyasema hayo leo wakati wa mazungumzo kati yake na Balozi mpya wa Jamhuri ya Demokrasia ya Watu wa Algeria katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Belabed Saad, huko Ikulu mjini Zanzibar.

Katika mazungumzo hayo, Dk. Shein alisema kuwa uhusiano na ushirikiano kati ya Tanzania na Ageria ni wa kihistoria hivyo kuna kila sababu ya kuuimarisha zaidi kwa kufuata nyayo zilizowekwa na waasisi hao wa nchi hizo.

Dk.Shein alisema kuwa kwa  upande wa  Zanzibar, nchi ya Algeria ina uhusiano mzuri na wa muda mrefu tokea wakati wa Rais wa Kwanza wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Marehemu Mzee Abeid Amani Karume ambapo nchi hiyo ni ya kwanza katika bara la Afrika kuyatambua Mapinduzi ya Januari 12, 1964 hatua ambayo ilipelekea kuitwa jina la Skuli ya Ben Bella ambayo ipo Zanzibar kama alama ya uhusiano huo.

Katika historia ya kumbukumbu za kupigania uhuru wa Tanzania na Algeria mashirikiano makubwa yalikuwepo kwa waaasisi wa nchi mbili hizo ambapo Dk. Shein alisisitiza kutunzwa, kuenziwa na kuendelezwa kwa manufaa ya pande mbili hizo.

Aidha, Dk. Shein alisema kuwa Algeria imekuwa na ushirikiano na uhusiano mzuri na Zanzibar  katika uimarishaji wa sekta ya elimu kwani imeweza kuwapatia nafasi za masomo vijana wengi wa Kitanzania wakiwemo kutoka Zanzibar.

Hivyo kutokana na ushirikiano huo katika sekta hiyo, Dk. Shein alisisitiza haja ya kuongezwa kwa nafasi za masomo kwa vijana wa Zanzibar nchini humo.

Sambamba na hayo, Dk. Shein alieleza kuwa mbali ya kuwepo kwa ushirkiano katika sekta hiyo ya elimu kuwa kuna haja kuwepo kwa mashirikiano katika sekta nyenginezo za maendeleo ikiwemo uwekezaji. huku alieleza iwapo nchi hiyo itakuwa tayari kununua zao la karafuu kutoka Zanzibar basi Zanzibar iko tayari baada ya kupokea maombi.

Dk. Shein pia, alieleza kuwa mbali ya sekta hizo Zanzibar pia, ina mengi ya kujifunza kutoka Algeria ikiwa ni pamoja na mafanikio yaliopatikana katika miundombinu, mafuta, gasi na nguvu za umeme.

Nae Balozi mpya wa Jamhuri ya Demokrasia ya Watu wa Algeria katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Belabed Saad alieleza kuwa Algeria inathamini sana uhusiano na ushirikiano wa muda mrefu uliopo katika ya Tanzania na nchi hiyo ambao uliasisiwa na viongozi wake wa mwanzo.

Balozi Saad alieleza kuwa Algeria itaendeleza uhusiano huo na ushirikiano uliopo sambamba na kuendeleza zaidi uimarishaji katika sekta za maendeleo sambamba na kuimarisha uchumi wa kidiplomasia kati ya nchi mbili hizo.

Mapema Dk. Shein alifanya mazungumzo na Mhe. Irene Florence Mkwawa, Balozi mpya wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini Uholanzi, mazungumzo yaliofanyika Ikulu mjini Zanzibar.

Katika Mazungumzo hayo, Dk. Shjein alimueleza Balozi Mkwawa kuwa Tanzania na Uholanzi ina uhusiano na ushirikiano wa muda mrefu ambao umeweza kusaidia uimarishaji wa sekta mbali za maendeleo Zanzibar na Tanzania Bara zikiwemo afya, mapambano dhini ya UKIMWI, elimu, uwekezaji na sekta nyenginezo.

Kwa upande wa Zanzibar, Dk. Shein alimueleza Balozi huyo kuwa Uholanzi imeweza kutoa ushirikiano mwema katika uimarishaji wa sekta ya afya, elimu na nyenginezo huku akisisitiza kuwa nchi hiyo imekuwa na mashirikaino mazuri na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kupitia Wizara ya Afya.

Dk. Shein alimueleza Balozi huyo kuwa Serikali ya Uholanzi imeweza kuiunga mkono Zanzibar katika ujenzi wa wodi mpya ya akina mama na watoto chini ya Mradi wa ORIO na miradi mengineyo huku Dk. Shein akimueleza Balozi Mkwawa umuhimu wa kuimarisha uchumi wa Kidiplomasia katika ya Tanzania na nchi hiyo.

Aidha, Dk. Shein alimueleza Balozi huyo maelewano yaliofikiwa kati ya Zanzibar na Uholanzi hasa kupitia Kampuni yake ya mafuta ya SHELL ambapo Zanzibar ilitiliana saini makubaliano ya ushirikiano katika kuendeleza sekta ya mafuta na gessi Agosti 2013 mjini Hague wakati wa ziara yake ya kikazi.

Alieleza kuwa makubaliano hayo ya awali kati ya Zanzibar na Kampuni hiyo ni pamoja na kufanya utafiti wa mafuta na gesi baada ya kumaliza taratibu za nchi ambapo tayri hivi sasa vikao kadhaa vimeshakaa kwa lengo la kujadili suala hilo muhimu la kimaendeleo.

Dk. Shein alieleza kuwa mbali ya kuimarika kwa uchumi wa Zanzibar katika hatua hiyo pia, suala la ajira na elimu kwa vijana wa Kizanzibari nalo litaimarika kwani litapewa kipaumbele zaidi mara baada ya kuanza mchakato huo.

Sambamba na hayo, Dk. Shein alimueleza Balozi huyo haja ya kuendelea kuimarisha uhusiano na ushirikiano katika sekta ya utalii, kwani watalii wengi wamekuwa wakitokea nchini humo.

Aidha, alimueleza Balozi huyo azma ya kuimarishwa na kuendelezwa suala zima la Diaspora na Serikali zote mbili ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na kumsisitiza kuwasihi wanadiaspora wa Tanzania nchini humo kuja kuekeza na kujenga nyumbani.

Nae, Balozi Irene Florence Mkwawa alimuahidi Dk. Shein kuwa atatumia uwezo wake wote kwa mashirikiano ya pamoja katika kutekeleza majukumu yake ikiwa ni pamoja na kuhakikisha uhusiano na ushirikiano kati ya Tanzania na Uholanzi unaimarika zaidi.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.