Habari za Punde

Wanadiaspora wakumbushwa kukumbuka nyumbani


  
STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
 Dar-es-Salaam                                                                                                 14.8.2015
---
SERIKALI ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, kwa kutambua umuhimu wa ushiriki wa Diaspora katika maendeleo ya Tanzania zilianzisha Idara maalum za uratibu na kuwahamasisha Watanzania wanaoishi nje ya nchi ili waweze kushiriki katika maendeleo ya nchi yao.

Dk. Shein aliyasema hayo leo katika hotuba iliyosomwa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Ikulu na Utawala Bora Mhe. Dk. Mwinyihaji Makame wakati wa kufunga Kongamano la Pili la Diaspora huko katika Hoteli ya Serena, mjini Dar-es-Salaam.

Katika hotuba hiyo, Dk. Shein alitoa wito kwa Watanzania wanaoishi nje ya nchi kuzitumia ipasavyo Taasisi hizo kwa kutambua na kujua fursa mbali mbali zilizopo Tanzania.

Dk. Shein aliwaeleza Wanadiaspora popote pale walipo ni muhimu kukumbuka nyumbani kwa lengo la kuwasaidia ndugu zao kupata ajira sambamba na kuwekeza nyumbani ili kuwapa ajira Watanzania wenzao.

Aidha, Dk. Shein aliwaahimiza Wanadiaspora kuendelea kutoa ushirikiano wao kwa wadau wote pale inapohitajika sambamba na kutoa taarifa zao kwenye afisi zinazowakilisha kwa lengo la kutoa kumbukumbu na mipango sahihi.


Alisema kuwa ushirikiano wao ndio uliofanikisha Kongamano hilo na kuonesha imani yake kwa kila mmoja wao na kueleza matumaini yake kuwa utaratibu huo utaendelea ili lengo liweze kufikiwa la kuitetea nchi pamoja na kuijengea heshima.

Pamoja na hayo, Dk. Shein alitumia fursa hiyo, kumshukuru Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa upendo wake na ushirikiano wake anaouonesha katika uongozi wake.

Pia, alitoa shukurani za dhati kwa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Ofisi ya Rais Ikulu Zanzibar na Ofisi ya Waziri Mkuu kwa kuendeleza juhudi za kuwaunganisha Wanadiaspora na kuongoza timu inayoandaa Kongamano hili.



Dk. Shein alipongeza hatua zilizofikiwa katika mijadala ya Kongamano hilo kwani imeweza kuimarisha na kujenga daraja la mahusiano na mashirikiano ya uzalishaji na kibiashara kati ya sekta ya biashara ndogo ndogo na za kati zilizomo ndani na nje ya nchi.

Kongamano hilo ni la Pili, kufuatia lile la kwanza lililofanyika mwezi Agosti mwaka jana katika hoteli hiyo ya Serena mjiniDar-es-Salaam, ambapo Kongamano lijalo hapo mwakani linatarajiwa kufanyika Zanzibar.

 "Tutaendelea kuamini kuwa ushirikiano mliouonyesha katika Kongamano hili utaendelea kuwepo katika Makongamano yajayo na katika shughuli mbali mbali za kuwashirikisha Watanzania waishio nje ya nchi",alisema Dk. Shein.

Sambamba na hayo, Dk. Shein aliwapongeza Wanadiaspora kwa kuzitumia kikamilifu siku mbili za Kongamano hilo kwa kubadilishana mawazo, uzoefu, kupeana taarifa za fursa mbali mbali za uwekezaji na biashara zilizopo hapa nchini na zile zinzopatikana nje ya nchi.

Nao washiriki wa Kongamano hilo walitoa shukurani kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Jakaya Mrisho Kikwete pamoja na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein kwa juhudi zao za kuhakikisha suala zima la Diaspora linaimarika sambamba na kuwaunganisha na kuwashajiisha vilivyo Wanadiaspora wa Tanzania waliopo nchi mbali mbali duniani.


Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.