Habari za Punde

CCM yalaani vitendi vya kuchanwa picha za wagombea CCM

Pemba                                                                                              
CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar, kimelaani vitendo vinavyofanywa na wafuasi wa chama cha CUF cha kuwapiga wafusi wa CCM wanaobandika picha za wagombea wao pamoja na kuzichana picha za wagombea wa CCM zinazobandikwa sehemu mbali mbali kwa ajili ya Kampeni.

Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar, Vuai Ali Vuai alilaani vitendo hivyo katika mkutano wa Kampeni ya uchaguzi wa CCM uliofanyika Konde, Wilaya ya Micheweni, Mkoa wa Kaskazini Pemba uliohudhuriwa na maelfu ya wanaCCM na wananchi ambapo mgeni rasmi alikuwa mgombea Urais wa Zanzibar kwa tiketi ya CCM, Dk. Ali Mohamed Shein.

Vuai alisema kuwa Chama cha CUF ndio kilichoanza kuzindua Kampeni zake za uchaguzi mapema kabla ya CCM, pia ndicho kilichoanza kubandika picha za wagombea wao Unguja na Pemba bila ya kufanyiwa fujo wala vurugu zozote lakini anashangazwa na vitendo vya wafuasi wa CUF kuwapiga vijana wa CCM wanaobandika picha pamoja na kuzichana picha za wagombea wa CCM.

Katika maelezo yake, Vuai alisema Chama cha CUF ndio cha mwanzo kuanza fujo na vurugu lakini pia ndio cha mwanzo kupita kwenye vyombo vya habari, Tume ya Uchaguzi na kusema uongo kuwa wao ndio wanaofanyiwa fujo.

Naibu Katibu Mkuu huyo  wa CCM alisema kuwa chama hicho kimesaini kanuni za maadili ya uchaguzi na kuahidi kuendesha kampeni za kistaarabu bila ya kuwepo vitisho, kutukanana, kupigana na hata kuchana picha za wagombea iweje leo CUF tayari wameshaanza kufanya vitendo hivyo ambavyo alisema ni vya kusikitisha.

Aidha, alisema kuwa makubaliano yalifanyika kwa vyama vya CUF na CCM baada ya kuwepo siasa chafu kwa muda mrefu makubaliano ambayo yalifanyika mara tatu na hatimae kupatikana muwafaka uliopelekea kuundwa Serikali ya Mapoinduzi ya Zanzibar yenye Muundo wa Umoja wa Kitaifa chini ya uongozi wa Dk. Shein lakini alionesha kushangwazwa na CUF kuanza dalili za kuvunja makubaliano hayo.

Mapema Spika wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar, Mhe. Pandu Ameir Kificho  alisema kuwa kuna haja ya kumchagua Dk, Shein kwani anaijua siasa sambamba na kutekeleza suala zima la amani na utulivu kwa vitendo.



Alisema kuwa mara zote wanapofika wageni kutoka sehemu mbali mbali duniani afisini kwake huwaeleza namna Dk. Shein alivyodhamiria kuhakikisha uchagauzi mkuu wa mwaka huu unakuwa huru na haki pamoja na juhudi zake za kuhakikisha amani na utulivu uliopo vinaendelea.

Aidha, alieleza kuwa amekuwa akitumia nafasi kuwaeleza wageni hao jinsi Dk. Shein anavyofuata sheria pamoja na kuitekeleza na kuilinda Katiba ya Zanzibar na ile ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Kutokana na juhudi hizo Spika Kificho alisema kuwa hiyo ndio sababu ya kutosha kwa Dk. Shein kupewa nafasi ya kuongoza kwa mara ya pili kuwa Rais wa Zanzibar.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais Mohammed Aboud alisema kuwa CCM imefanya mambo mengi katika kipindi cha miaka mitano iliyopita ikiwa ni pamoja na kuimarisha miradi ya maendeleo.

Aboud alisema kuwa Dk.Shein amejenga misingi imara ya kuleta maendeleo hivyo kuna kila sababu ya wananchi kumchagua yeye pamoja na viongozi wengine wa CCM wanaowania nafasi katika uchaguzi wa mwaka huu.

Alisema kuwa tayari chama cha CUF kimeshaonesha dalili mbaya ya kushindwa kutokana na kiongozi wake mkubwa Juma Duni kuanza kuhama hama kwa kutokana na uchoyo wa madaraka na fedha.

Dk. Maua Daftari akimnadi Dk. Shein pamoja na wagombea wote wa CCM kwa upande wa Zanzibar na wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania alisema kuwa mafanikio makubwa yameweza kupatikana katika uongozi wa CCM chini ya Dk. Shein katika kipindi chake cha miaka mitano.

Dk. Daftari alisema kuwa juhudi zilizochukuliwa na Serikali katika kuimarisha miradi ya maendeleo ikiwemo kilimo zimeanza kuzaa matunda na hivi sasa wananchi walio wengi wanajishughulisha na kilimo cha mboga mboga hapa Pemba na hivi sasa hawaagizii tena bidhaa hizo kutoka Tanzania Bara.

Aidha, alisema kuwa tayari miradi ya maendeleo imekamilishwa ikiwemo miradi ya barabara,afya, elimu, maji, umeme sambamba na kukua kwa sekta ya utalii kwa kuwepo hoteli yenye chumba chini ya bahari ambacho ni kivutio kikubwa cha watalii hivi sasa ambao wamekuwa wakija Pemba.

Dk. Daftari alitumia fursa hiyo kutoa shukurani kwa Dk. Shein kwa kusimamia amani na utulivu pamoja na maendeleo makubwa yaliopatikana huku akisisitiza haja ya kuendelea kumchagua yeye na viongozi wote wa chama hicho wanaowania nafasi ya Urais wa Jamhuri ya Muungano, Urais kwa Zanzibar,Ubunge, Uwakilishi na Udiwani.

Nae Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM Khadija Aboud aliwataka wanaCCM kutofanya kosa la kutomchagua Dk. Shein kwani ndio kiongozi mwenye Sera za kuleta maendeleo pamoja na kuwataka kuwachagua viongozi wote wa CCM


Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.