STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF
THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar 28.9.2015

VIONGOZI wa CCM Zanzibar wamewataka wananchi wa Zanzibar kuendeleza amani,
utulivu na mshikamano uliopo na kuwaonya wale wote wanaokusudia kufanya vurugu
wakati wa uchaguzi mkuu wajue kuwa Serikali pamoja na vyombo vyake vya Dola viko
macho.
Viongozi hao waliyasema hayo leo katika
Mkutano wa Kampeni ya uchaguzi wa CCM
uliofanyika katika uwanja wa Garagara, Jimbo la Mtopepo, Mkoa wa Mjini Magharibi uliohudhuria na maelfu ya wanaCCM na
wananchi ambapo mgeni rasmi alikuwa mgombea Urais wa Zanzibar kwa tiketi ya
CCM, Dk. Ali Mohamed Shein.
Nae Mjumbe wa Kamati Kuu na Makamu wa
Pili wa Rais Balozi Seif Ali Idd alisema kuwa vyama vya upinzani hawana Sera na
hoja na hivi sasa wamebaki kubwabwaja.
Balozi Seif alisisitiza haja ya
kuimarishwa kwa umoja na mshikamano kwa wananchi na wanaCCM kwa jumla na kusema
kuwa umoja ndio silaha ya kushinda kwa CCM.
Alisema kuwa kuwepo kwa amani na utulivu ni
jambo la lazima na kuwaonya wale wote waliodhamiria kufanya fujo wakati wa
uchaguzi kuachana na azma yao hiyo na kuwaonya wanachama wa CUF wasije kujaribu
kufanya fujo huku akiwataka wazee wa Darajabovu kutowaachia vijana wao kufanya
fujo.
Aidha, Balozi Seif aliwataka wazee wasije
kuilaumu Serikali iwapo watoto wao watafanya fujo kwani Dola haijaribiwi wala
haichezewi na kueleza kuwa anaetaka kujaribu akale muhogo ajue kama ni mtamu
ama mchungu lakini sio serikali.
Alisema kuwa Serikali iko macho kwa
kuwadhibiti wale wote walio na lengo la kufanya vurugu siku ya tarehe 25 na 26.
"Wao wanasema watakuja kuingoa na
mimi nna jua unaongolewa ni muhogo kama Serikali basi kuna taratibu zake
kidemokrasia....kama unataka kungoa aende akangoe kwenye shamba la baba
ake", alisema Balozi.
Alisema kuwa huu si wakati wa kuwasemea
wananchi, na hakuna serikali ya mkataba kwani serikali ya mkataba lengo lake ni kuvunja Muungano, na CCM haiko tayari
kuwepo kwa serikali ya Mkataba na kueleza kuwa CCM wanachokijua wao ni serikali
mbili.
Alisema
kuwa ndani ya miaka mitano maendeleo makubwa yamepatikana Unguja na
Pemba huku akitolea mfano miundombinu ya barabara pamoja na kuwepo huduma
nyengine za maendeleo.
Nae Spika wa Baraza la Wawakilishi Pandu
Ameir Kificho alitumia fursa hiyo kwa kusema kuwa Dk. Shein ni mtu muadilifu,
makini, muangalifu na katika maamuzi yake hakurupuki na kwa mwenendo na tabia
hizo hakuna mgombea wa urais wa kumpa kura nyingi za ndio isipokuwa Dk. Shein.
Kificho aliwaomba wananchi kuwapeleka Wawakilishi
wa CCM na Wabunge wa CCM kwani wao ndio wanaofanya kazi vizuri kwa maendeleo ya
Watanzania na wananchi wa Zanzibar kwa jumla na hawana mtindo wa kutoka toka
katika nyumba hizo za kutunga sheria.
Nae Waziri wa Maji,Ardhi na Nishati
Ramadhani Abdalla Shaaban alishangazwa
na kauli za CUF zinazosema kuwa ndani ya
miaka 50 Zanzibar haina maendeleo na kusema kuwa mbali ya miaka hiyo wanayosema
wapinzani tayari ndani ya miaka mitano tu ya Dk. Shein maendeleo yaliopatikana
Unguja na Pemba ni makubwa.
Alieleza kuwa tayari wanaCCM na wananchi
wameshaamua tarehe 25 kummiminia kura zote Dk. Shein na kusema kuwa Serikali ya
Mapinduzi ya Zanzibar chini ya CCM uchumi umeimarika.
Pamoja na hayo, alieleza kuwa angalau CUF wanakiri kuwa kifungu cha Katiba
mpya inayopendekezwa cha 23 na 26 kimeelezea kwamba ardhi, mafuta na gesi yatashughulikiwa
na Zanzibar, na kusema kuwa kinachosubiriwa ni wakati wa kuipigia kura Katiba
inayopendekezwa ifanye kazi.
Alisema kuwa tayari Rais Jakaya Mrisho
Kikwete na Dk. Shein wameshakubaliana juu
ya Sheria ya mafuta na gesi, na tayari sheria hiyo imeshakwenda kwenye Bunge la
Muungano kwa lengo la kuwa Zanzibar ishughulikie wenyewe rasilimali hizo.
Nae Bi Fatma Karume mke wa muasisi wa
Zanzibar marehemu Mzee Abeid Amani Karume, alisema kuwa wanawake walidhalilishwa,
walitupwa lakini ASP ikaliona hilo na hatimae kuwasimamisha akina mama kwenda
katika mikutano ya hadhara na kupiga kura kwani hapo mwanzo hawakupewa fursa hizo.
Bi Fatma, alitoa pongezi kwa akina mama
kwa kupokea wito na kujitokeza kwa wingi katika mikutano ya Kampeni ya CCM ambapo alitumia fursa hiyo
kumuombea kuwa Dk. Shein, Dk. Magufuli, Samia, Wabunge, Wawakilishi pamoja na
Madiwani wote huku akieleza kuwa Zanzibar tayari imeshakuwa huru tokea Januari 12, 1964.
Nae Mwenyekiti wa CCM, Mkoa wa Mfenesini
Yussuf Mohammed Yussuf aliwataka wanaCCM kuzitunza shahada zao za kupigia kura
na kuwataka kuwapigia kura wagombea wote wa CCM.
Alisema kuwa CUF hawana hoja na
kushangazwa na kauli inayotoa kuwa Zanzibar haina Mamlaka kamili wakati tayari
Zanzibar inayo mamlaka Kamili ila nia ya chama hicho ni kurudisha uongozi wa
Kifalme.
Rajab Mkasaba,
Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024
2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment