Habari za Punde

Dk Shein Atembelea Mradi wa Maji Makunduchi Zanzibar.

STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar                                                                                                                        1.12.2015
---
RAIS  wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ametembelea mradi wa maji Makunduchi na kuwataka wananchi wa kijiji hicho kuendelea kuiamini Serikali yao ya Mapinduzi ya Zanzibar katika juhudi zake za kuukamilisha mradi huo na kuwapatia huduma ya uhakika ya maji safi na salama katika kipindi kifupi kijacho.

Dk. Shein aliyasema hayo leo, wakati alipokuwa akizungumza na wananchi waliofika katika eneo la Mradi huo huko Makunduchi Mkoa wa Kusini Unguja, mara baada ya kutembelea  mradi wa ubadilishaji wa tangi pamoja na kisima kipya kilichochimbwa katika eneo hilo la Mradi.

Katika maelezo yake Dk. Shein aliwaeleza wananchi waliohudhuria tukio hilo kuwa Serikali yao ya Mapinduzi ya Zanzibar ipo na inaendelea na kazi za kuwahudumia wananchi wote na kusisitiza kuwa kukamilika kwa mradi huo kutasaidia kwa kiasi kikubwa kupatikana huduma ya maji safi na salama kwa wananchi wa eneo hilo.

Dk. Shein alisema kuwa mradi huo unaotarajiwa kuzinduliwa katika sherehe za Mapinduzi utaweza kuongeza upatikanaji wa maji safi na salama na kuwaondoshea kabisa tatizo la huduma ya maji safi na salama wananchi wa maeneo hayo.

Aidha, Dk. Shein alisema kuwa visima vitatu ambavyo vitapeleka maji katika tangi hilo kubwa lililobadilishwa kikiwemo kisima kipya kiliopo karibu ya tangi hilo ambacho kinatarajiwa kukamilika ndani ya wiki moja ijayo, kisima kilichochimbwa kupitia mradi wa Ras el Khaimah na kile kilichochimbwa Mnywambiji huko Kibuteni vikiunganishwa kwa pamoja vitatoa maji ya kutosha kwa ajili ya matumizi ya wananchi.
 Pamoja na hayo, Dk. Shein alitumia fursa hiyo kutoa pongezi kwa wafanyakazi na uongozi wa Mamlaka ya Maji Zanzibar, (ZAWA) pamoja na Wizara ya Ardhi, Makaazi, Maji na Nishati, viongozi wa Jimbo  na wananchi wote waliounga mkono na kuonesha ushirikiano wao katika utekelezaji wa mradi huo ili kuhakikisha unakamilika na kutoa huduma kwa wananchi.
 Nae Waziri  wa Ardhi, Makaazi, Maji na Nishati Mhe. Ramadhan Abdalla Shaaban alisisitiza kuwa si muda mrefu wananchi wa maeneo hayo watafaidika na huduma ya maji safi na salama baada ya kukamilika kwa mradi huo wa maji Makunduchi.
 Waziri Shaaban alibainisha kuwa kazi ya ulazaji wa mabomba kutoka  kisima kipya cha pango la Mnywambiji kilichochimbwa huko Kibuteni nayo iko mbioni kumalizika ambapo kwa hivi sasa imebaki sehemu ndogo tu ya kuvuga barabara ya Makunduchi na kuingia tangini.
 Mapema Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya Maji Zanzibar (ZAWA), Dk. Mustafa Ali Garu alisema kuwa   visima hivyo vitatu vitakapokamilika vitaweza kutoa huduma ya maji safi na salama kwa asilimia zaidi ya 90 kwa wananchi wa Makunduchi.
 Alifafanua kuwa kisima cha Makunduchi kitaanza kutoa maji wiki ijayo wakati kile cha Kibuteni kitaanza kutoa maji baada ya kukamilika uwekaji wa umeme wa jua hivi karibuni.
 Alisema kuwa Mradi huo umeweza kutekelezwa kwa mashirikiano ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Uongozi wa Jimbo, Taasisi ya Milele Zanzibar Foundation pamoja na wananchi.
 Mkurugenzi Garu alisema kuwa mradi huo umeweza kupitia katika miongo mbali mbali ambao uliansihwa katika miaka ya 1960 kwa msaada kutoka Serikali ya Watu wa China na mnamo mwaka 2000 ukaimarishwa zaidi kwa kuwekwa tangi la sandarusi ambapo awamu hii limejengwa tangi jipya la chuma.
 Alieleza kuwa tayari kazi za uwekaji wa tangi hilo jipya zimeshafanywa na hivi sasa imeshakamilika na limeanza kutumika kwa kutiwa maji ambayo husambazwa kwa wananchi.
 Dk. Garu alisema kuwa kukamilika kwa mradi huo baada ya kukamilika kwa visima hivyo vitatu kutasaidia kutoa zaidi ya lita laki moja ambazo zitasambazwa na kuwasaidia wananchi wa Makunduchi na kulifanya tatizo la maji kuwa historia kijijini hapo.
 Sambamba na hayo, Garu alifafanua kuwa kisima hicho pia, kitapeka huduma hiyo ya maji kwa wananchi wa Mtende.
 Nao wananchi wa Makunduchi walitoa salamu zao za shukurani na pongezi kwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar chini ya uongozi wa Dk. Shein kwa kuendeleza juhudi za kuwapelekea huduma muhimu za kimaendeleo, kijamii na kiuchumi katika vijiji vyao huku wakiahidi kuendelea kumuunga mkono.
 Akitoa salamu hizo za shukurani Mkuu wa Mkoa wa Kusini Unguja Dk. Idriss Muslim Hija alieleza kuwa kuna kila sababu za kuendelea kuungwa mkono juhudi hizo za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na wananchi wa Makunduchi wanatoa shukurani za dhati kwa juhudi zinazofanywa na Serikali yao.
 Viongozi mbali mbali wakiwemo Mawaziri wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, wananchi pamoja na viongozi wa vyama vya siasa walihudhuria katika ziara hiyo.

Rajab Mkasaba.

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.