Habari za Punde

Hutuba ya Rais wa Zanzibar katika Sherehe za Maadhimisho ya Miaka 52 ya Mapinduzi ya Zanzibar.

HUTUBA YA RAIS WA ZANZIBAR NA MWENYEKITI WA BARAZA
LA MAPINDUZI, MHE. DK. ALI MOHAMED SHEIN, KATIKA
MAADHIMISHO YA SHEREHE ZA MIAKA 52 YA
MAPINDUZI YA ZANZIBAR, AMAAN STADIUM
TAREHE 12 JANUARI, 2016

Mheshimiwa Dk. John Pombe Magufuli;
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,

Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan;
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,

Mheshimiwa Majaliwa Kassim Majaliwa;
Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,

Mheshimiwa Maalim Seif Sharif Hamad;
Makamu wa Kwanza wa Rais, Zanzibar,

Mheshimiwa Balozi Seif Ali Iddi;
Makamu wa Pili wa Rais, Zanzibar,

Mheshimiwa Mzee Ali Hassan Mwinyi;
Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,

Mheshimiwa Benjamin William Mkapa,
Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,

Mheshimiwa Dk. Jakaya Mrisho Kikwete;
Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,

Mheshimiwa Dk. Salmin Amour Juma;
Rais Mstaafu wa Zanzibar,

Mheshimiwa Dk. Amani Abeid Karume;
Rais Mstaafu wa Zanzibar,

Waheshimiwa Mawaziri wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar,

Mheshimiwa Job Ndugai;
Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,

Mheshimiwa Pandu Ameir Kificho;
Spika wa Baraza la Wawakilishi la Zanzibar,

Mheshimiwa Othman Chande Mohamed;
Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,

Mheshimiwa Omar Othman Makungu;
Jaji Mkuu wa Zanzibar,

Waheshimiwa Mabalozi na Wawakilishi wa Mashirika ya Kimataifa,

Mheshimiwa Abdalla Mwinyi Khamis;
Mkuu wa Mkoa wa Mjini Magharibi,

Viongozi mbali mbali wa Serikali na Vyama vya Siasa,

Ndugu Wananchi,

Mabibi na Mabwana,

Assalamu Aleikum,

Awali ya yote, napenda nianze kwa kumshukuru Mola wetu Mtukufu mwenye kustahiki kushukuriwa na viumbe vyote kwa kutujaalia uhai na afya njema tukaweza kukutana katika hadhara hii muhimu kwa historia na harakati za maendeleo ya Zanzibar na Jamhuri ya Muungano waTanzania kwa jumla.  Leo tarehe 12 Januari, 2016 tunaadhimisha kilele cha sherehe za miaka 52 tangu yalipofanyika na kufanikiwa kwa Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar ya tarehe 12 Januari 1964.

Mwenyezi Mungu awape malazi mema waasisi na viongozi wetu wa Mapinduzi waliokwishatutangulia mbele ya haki na walio hai, Mwenyezi Mungu awape afya njema na umri mrefu ili tuzidi kunufaika na hekima zao.  Mwenyezi Mungu aijaaliye nchi yetu amani, umoja, mshikamano zaidi na atupe mafanikio katika utekelezaji wa mipango yetu ya maendeleo na kutuongezea ustawi wa jamii yetu.

Ndugu Wananchi,
Kwa niaba ya wananchi wa Zanzibar, napenda nimpongeze kwa dhati Mheshimiwa Dk. John Pombe Magufuli; Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan; Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuiongoza Awamu ya Tano ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.  Kuchaguliwa kwenu, ni kielelezo cha imani waliyonayo wananchi kwenu na kwa Chama cha Mapinduzi. Natoa shukurani zangu za dhati kwenu, kwa kuja kuungana nasi katika sherehe hizi za maadhimisho ya Miaka 52 ya Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar.  Tunakukaribisheni kwa furaha kubwa pamoja na viongozi wengine wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania mliohudhuria.

Kadhalika, napenda nitoe shukurani zangu za dhati kwa mabalozi, wawakilishi wa mashirika ya kimataifa, taasisi mbali mbali, wananchi na wageni waalikwa wote kwa kuhudhuria kwa wingi katika sherehe hizi muhimu na adhimu ambazo zimefana sana.  Kuwepo kwetu hapa siku hii ya kilele na mahudhurio makubwa kunadhihirisha kwamba Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar ya Januari 12, 1964 yanathaminiwa sana na yataendelea kudumishwa kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.

Ndugu Wananchi,
Leo ni siku adhimu na muhimu kwa Wananchi wa Zanzibar na Tanzania kwa jumla ambapo miaka 52 iliyopita waliikata minyororo ya utawala wa kikoloni na kisultani ambao ulidumu kwa miaka 132. Wananchi wanyonge walioongozwa na Chama cha Afro Shirazi walijitolea muhanga kufanya Mapinduzi dhidi ya wakoloni, mabwanyenye na mabepari waliokuwa wakiendeleza vitendo vya udhalilishaji, dhulma, unyonyaji na ubaguzi kwa wananchi.

Madhila waliyotendewa wananchi yalihusu masuala yote muhimu ya maisha yakiwemo kubaguliwa katika elimu, matibabu, makaazi na matumizi ya ardhi na ubaguzi wa kukoseshwa haki za kiraia katika nchi yao wenyewe.  Haya yote leo yanabaki kuwa ni historia baada ya Waasisi wa Mapinduzi wakiongozwa na Jemedari wake Marehemu Mzee Abeid Amani Karume na Chama cha ASP kufanya Mapinduzi tarehe 12 Januari, 1964. Huo ndio mwanzo wa utawala wa wanyonge wa Zanzibar na kupata uhuru wao wa kweli, unaozingatia misingi ya usawa, utu na kuturejeshea heshima ya wafanyakazi na wakulima nchini mwetu iliyopotea kwa kutawaliwa.  

Leo tunaposherehekea miaka 52 ya Mapinduzi, vile vile, tunasherehekea umoja wetu unaotokana na nchi mbili zilizokuwa huru, Jamhuri ya Tanganyika na Jamhuri ya Watu wa Zanzibar na kuzaliwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.  Muungano wetu umetokana na dhamira ya dhati ya vyama vyetu vya ukombozi vya ASP na TANU na sasa CCM pamoja na uongozi bora na thabiti wa Waasisi wa nchi yetu, hayati Mwalim Julius Kambarage Nyerere na hayati Mzee Abeid Amani Karume.
Ndugu Wananchi,
Kwa hakika tuna wajibu wa kuwashukuru na kuwaombea dua Waasisi wa Mapinduzi kwani wao ndio msingi wa mafanikio makubwa wa maendeleo tuliyoyapata. Katika kipindi chote cha miaka 52, wananchi wote kwa nyakati tafauti wamefaidika na matunda ya Mapinduzi kutokana na malengo yake na mipango ya maendeleo iliyowekwa.  

Kwa hivyo, maadhimisho ya sherehe hizi yanatukumbusha umuhimu wa kuendelea kuyaheshimu, kuyatetea, kuyalinda na kuyadumisha Mapinduzi yetu, kwa faida ya kila mmoja wetu. Katika kuyathamini na kuyaenzi Mapinduzi yetu, Serikali imeamua kujenga mnara maalum wa kumbukumbu ya Mapinduzi katika eneo la Michenzani, Mwembekisonge, uliozinduliwa mwaka jana.  Naomba wananchi mwende mkautembelee mnara wa aina yake huu pale mtakapopata nafasi ambapo pia mtapata nafasi ya kuelezwa historia ya Mapinduzi iliyotayarishwa katika vyumba maalum.

Ndugu Wananchi,

Jitihada za Serikali, wananchi na washirika wetu wa maendeleo zimetuwezesha kuitekeleza mipango mikuu ya maendeleo katika kipindi cha mwaka mmoja uliopita kwa kuzingatia Dira ya Maendeleo ya 2020, MKUZA Awamu ya Pili na Ilani ya Uchaguzi Mkuu ya CCM ya mwaka 2010-2015 tuliyoitekeleza kwa kiwango kinachokadiriwa kufikia asilimia 90 pamoja na Malengo ya Milenia.  Maelezo nitakayoyatoa yanadhihirisha mafanikio yaliyopatikana katika mwaka 2015.



Ndugu Wananchi,
Katika mwaka 2015, Tume ya Mipango ya Zanzibar imeratibu mapitio ya Mkakati wa Kukuza Uchumi na Kupunguza Umasikini (MKUZA II) unaomaliza muda wake mwezi wa Juni 2016. Rasimu ya mwanzo ya mkakati mpya imefikia hatua ya kuchangiwa maoni na wahusika mbali mbali na inategemewa kuanza kutumika rasmi kuanzia bajeti ya mwaka 2016 /2017.


Vile vile, Serikali imefuta Sheria namba 1 ya mwaka 1999 ya miradi ya maridhiano na kutunga Sheria mpya ya mashirikiano baina ya sekta ya umma na sekta binafsi (PPP) namba 8 ya mwaka 2015. Ni matumaini ya Serikali kwamba wawekezaji binafsi wataitumia fursa ya mashirikiano baina ya sekta hizo mbili, kupitia sheria mpya, kwa lengo la kuongeza tija na ufanisi.

Ndugu Wananchi,
Kutokana na umuhimu wa utafiti, Serikali kupitia Tume ya Mipango kwa kushirikiana na COSTECH inatayarisha Mpango wa Utafiti wa Zanzibar wenye kushirikisha sekta zote. Rasimu ya awali ya mwongozo wa utekelezaji wa tafiti imetolewa ili kazi ya utafiti ifanyike kitaalamu kwa lengo la kupata taarifa sahihi na kuondoa kero za wananchi.

Katika mwaka 2014, Serikali iliandaa programu maalum za utekelezaji wa “Matokeo kwa Ustawi” kwa kupitia mfumo wa maabara katika sekta ya Utalii, uimarishaji wa biashara na upatikanaji wa Rasilimali Fedha.  Utekelezaji wa programu hizi umeonesha mafanikio ya kutia moyo. Kwa sasa, Tume iko katika hatua za matayarisho ya maabara ya Elimu na Afya kwa kushirikiana na taasisi zinazohusika.  Maabara hizo zinatarajiwa kufanyika mwaka huu.

Ndugu Wananchi,
Licha ya kuendelea kuwepo kwa matukio mbali mbali  yanayoathiri kasi ya ukuaji wa uchumi wa dunia, uchumi wetu umeendelea kuimarika katika  kila mwaka.  Mwaka 2014 Pato halisi la Taifa lilikua na kufikia asilimia 7.0.  Hali  hii imechangiwa zaidi na kuimarika kwa sekta ya viwanda na sekta ya huduma kwa kuongezeka  kwa idadi ya watalii wanaoingia nchini kutokana na kuwepo kwa vivutio vya utalii na amani na utulivu.  Kadhalika, Pato la Mtu binafsi limeongezeka hadi  kufikia TZS 1,552,000 (USD 939) mwaka 2014 ikilinganishwa na TZS 1,384,000 (USD 866) mwaka 2013 sawa na ongezeko la asilimia 12.1.  Kwa mujibu wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2010-2015, pato la mtu binafsi lilitakiwa lifikie TZS 884,000 ifikapo mwaka 2015. Ni dhahiri kwamba pato la mtu binafsi limepindukia kiwango kilichokadiriwa.

Ndugu Wananchi,
Katika kipindi cha robo mwaka ya kwanza ya mwaka 2015, kasi ya ukuaji wa uchumi  imefikia asilimia 6.1 na katika robo ya pili ya mwaka 2015 imefikia asilimia 7.0.  Kuendelea kuimarika kwa hali ya uchumi kwa robo mwaka ya kwanza na ya pili kwa mwaka 2015 kumetokana na kuimarika kwa sekta ya viwanda, sekta ndogo ya malazi, huduma za chakula, huduma za fedha, ufugaji, bima pamoja na ukuaji wa sekta ndogo ya ujenzi.

Katika mwaka 2015, kasi ya mfumko wa bei za bidhaa na huduma nchini imeendelea kuwa ya tarakimu moja kutoka asilimia 5.6 mwaka 2014 kufikia asilimia 5.7 mwaka 2015.  Serikali inaendelea na juhudi za kudhibiti kasi ya mfumko wa bei nchini kwa kupunguza ushuru wa bidhaa muhimu zinazoingizwa nchini na kuwasaidia wakulima kwa kuwapatia pembejeo kwa beif nafuu ili kuongeza uzalishaji wa mazao. 

Ndugu Wananchi,
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imeongeza ufanisi katika kuimarisha ukusanyaji wa mapato na kudhibiti uvujaji wa mapato hayo.  Katika kipindi cha miezi sita ya kwanza ya mwaka wa fedha 2015/2016, mapato ya ndani yalifikia TZS Bilioni 188.4 ikilinganishwa na kipindi kama hicho cha mwaka 2014/2015 ambapo TZS Bilioni 172.5 zilikusanywa,  sawa na ongezeko la mapato la asilimia 9.2.  Vile vile, Serikali inaendelea na juhudi za kuimarisha mapato ikiwemo kupunguza misamaha ya kodi katika baadhi ya miradi ya uwekezaji na kufanya marekebisho ya viwango vya ada mbali mbali.  Kadhalika, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imeanzisha kodi mpya ya miundombinu, ili kuhakikisha tunakuwa na fedha za kuiendeleza na kuitunza miundombinu yetu.

Ndugu Wananchi,
Serikali iliendelea kuwashajiisha wawekezaji wa ndani na nje kuwekeza katika sekta zote kuu za kiuchumi na kijamii. Katika kipindi cha Januari hadi Disemba 2015, jumla ya miradi 31 yenye thamani ya Dola za Marekani Milioni 316.0 imeidhinishwa katika sekta mbali mbali katika miradi hio, miradi mingi ni ya utalii. Miradi hii itakapomalizika itatoa nafasi za ajira 2,500.
Juhudi kubwa zilifanywa zilizopelekea kuanzishwa kwa utekelezaji wa kuyaendeleza Maeneo Huru ya Uchumi kwa vitendo. Mradi wa Ujenzi wa Mji Mpya wa Fumba umeanza, ambapo kiwanda kikubwa cha maziwa  kimejengwa na kimeanza kazi Julai, 2014.  Mji huo utajumuisha ujenzi wa nyumba 650 zitakazouzwa kwa watu mbali mbali.  Ujenzi wa nyumba hizo unatarajiwa kuanza Februari mwaka huu.   Kadhalika, bandari ndogo itakayotoa huduma kwa wananchi na wageni itajengwa katika eneo hilo. Serikali, kwa kushirikiana na Kampuni ya “Union Property Developer” na “Coastal Dredging” hivi sasa inaendelea na ujenzi wa miundombinu, ikiwemo barabara mpya zenye upana wa mita 15, mita 30 pamoja na barabara kuu ya mita 60.

Ndugu Wananchi,
Kwa upande wa Mkoa wa Kaskazini Unguja, Mradi wa ujenzi wa mji wa kisasa wa kibiashara pamoja na hoteli kubwa za kisasa, nyumba za kuishi, uwanja wa ndege mdogo na uwanja wa kimataifa wa “golf ” wa kisasa vitajengwa.  Kampuni ya “Pennyroyal ya Gibralter” imetenga jumla ya Dola za Kimarekani milioni 800 kwa ajili ya mradi huu.  Kampuni hiyo hivi sasa inaendelea na ujenzi barabara ya kisasa inayotoka Mkwajuni kupitia Kijini hadi Mbuyutende na imefikia hatua nzuri.

Katika kuliendeleza eneo la Bwawani mnamo mwezi wa Novemba 2015, Serikali ilitiliana saini Mkataba na Kampuni ya “Quality Group Limited” ambayo itaanzisha mradi mkubwa wa kuendeleza Hoteli ya Bwawani na maeneo yaliyoizunguka.  Kampuni hiyo imetenga Dola za Marekani zipatazo Milioni 200 zitakazotumika kwa ajili ya kuifanyia matengenezo makubwa Hoteli ya Bwawani, ili ifikie kiwango cha nyota tano.  Kadhalika, kampuni hiyo ya “Quality Group Limited” itajenga majengo ya biashara na kituo cha mikutano ya Kimataifa katika eneo hilo la Bwawani.

Aidha, Serikali imeidhinisha mradi wa uimarishaji wa Hoteli ya “Mtoni Marine”, wenye lengo la kutengeneza ufukwe maalum kwa ajili ya mapumziko ya wageni na wenyeji.  Sambamba na uimarishaji huo, utaanzishwa mji mdogo wa kisiwa kwa lengo la kuikuza sekta ya utalii.

Ndugu Wananchi,
Uongozi wa Mfuko wa Hifadhi ya Jamii Zanzibar (ZSSF) nao umeshajiika kuwekeza katika ujenzi wa majengo ya kisasa, ili kubadilisha taswira ya Zanzibar. Katika mwaka huu wa fedha, 2015/2016, ZSSF imeanza kutekeleza Mradi wa ujenzi wa nyumba za kisasa katika eneo la Mbweni – Unguja.  Mradi huu unajumuisha ujenzi wa jumla ya majengo 18 ya ghorofa 7 kila moja na yatakapomalizika, jumla ya nyumba (flats) 252 zitapatikana. Mradi huu unatarajiwa kumalizika katika kipindi cha miaka mitatu ijayo.

Ndugu Wananchi,
Katika mwaka 2015, suala la kuimarisha mazingira ya biashara lilipewa umuhimu mkubwa. Serikali ilichukua hatua ya kuhakikisha kuwa bidhaa za chakula zinakuwepo nchini wakati wote. Takwimu zinaonesha kuwa katika kipindi cha mwaka 2015 hakukuwa na upungufu wa bidhaa hizo. Serikali imeanzisha Baraza la Kusimamia Utoaji wa Leseni kwa lengo la kuweka mfumo mzuri na ulio bora katika utoaji wa leseni na vibali vya biashara.

Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ililinunua jumla ya tani 2,826.5 za karafuu 2,826.5 zenye thamani ya TZS bilioni 39.5 kutoka kwa wakulima  katika mwaka 2014/2015, hadi kufikia tarehe 4 Januari, 2016, Serikali ilinunua jumla ya tani 3,235.1 zenye thamani ya TZS bilioni 45.3.

Kwa upande wa mauzo, katika mwaka 2014/2015, Serikali iliuza nchi za nje jumla ya tani 2,766.2 za karafuu zenye thamani ya TZS bilioni 53.3.  Kwa  mwaka 2015/2016 hadi kufikia tarehe 31 Disemba, 2015, Serikali imeuza karafuu nchi za nje tani 2,122.0 zenye thamani ya  TZS  bilioni 36.0.  Msimu wa karafuu wa mwaka huu bado unaendelea na wakulima wanaendelea kuuza karafuu zao ZSTC na matarajio ya Serikali ni kununua tani 5,500 za karafuu.

Kadhalika, katika kipindi cha mwaka 2014/2015, Serikali imetoa mikopo yenye thamani ya TZS milioni 342.3 kwa wakulima 126 wa karafuu wa Unguja na Pemba. Mikopo hiyo imewasaidia kununua pembejeo na vitendea kazi.  Nachukua nafasi hii kuwapongeza wakulima wa Unguja na Pemba kwa juhudi zao wanazozichukua katika kuliendeleza zao la karafuu kwa kushirikiana na Serikali.

Aidha kwa lengo la kuliendeleza zao la karafuu, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ilizindua Mfuko wa Maendeleo ya Karafuu Zanzibar ambao Shirika la ZSTC limeweza kulipa fidia kwa walioanguka kwenye mikarafuu jumla ya TZS milioni 60 na kutoa mikopo.



Ndugu Wananchi,
Juhudi za kufufua viwanda zilipata mafanikio zaidi katika mwaka 2015 ikilinganishwa na miaka iliyopita. Bidhaa zilizozalishwa viwandani kwa mwaka 2015 zikiwemo maziwa, sukari, maji ya kunywa, unga wa ngano, juisi, sabuni,  bidhaa za nguo na viungo zilikuwa na thamani ya TZS bilioni 136.0, ikiwa ni ongezeko la asilimia 5.51 ikilinganishwa na mwaka uliopita ambapo bidhaa zilizozalishwa nchini zilikuwa na thamani ya TZS bilioni 128.9.  Kuimarika kwa viwanda vyetu kutaongeza ajira kwa wananchi na kuwapunguzia umasikini.

Ndugu Wananchi,
Serikali imepanga na kutekeleza mikakati mbali mbali ya kuiendeleza sekta ya utalii ambayo hivi sasa ndiyo sekta kiongozi kwa uchumi wetu. Wawekezaji wameshajiishwa katika ujenzi wa hoteli ambapo hoteli ya “Park Hyatt” ilifunguliwa hivi karibuni. Kamisheni ya Utalii imejitangaza katika masoko mapya ya huko China na India.  Kamisheni hio imefungua Ofisi ya Uwakala huko Mumbai, India, kwa lengo la kuimarisha utalii.  Katika kuimarisha huduma za utalii na upatikanaji wa ajira, hatua zimechukuliwa kwa kuanzisha mafunzo ya fani mbali mbali za utalii yanayotolewa katika kiwango cha Stashahada katika Chuo Cha Maruhubi na Shahada na Stashahada katika Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar. Katika mwaka wa mafunzo uliomalizika wanafunzi 1028 wamemaliza yao kwenye vyuo hivyo.  Katika mwaka ujao tunatarajia Chuo cha Utalii Maruhubi kitaunganishwa na SUZA.

Katika mwaka 2015, watlii waliendelea kuitembelea Zanzibar kutokana na vivutio viliopo, pamoja na kuwepo amani na utulivu.  Jumla ya watalii 254,699  waliitembelea Zanzibar katika kipindi cha Januari-Novemba, 2015.   Wito wangu kwa wananchi ni kuwa tuendelee kushirikiana katika kulifanikisha lengo letu la Utalii kwa Wote, ili mafanikio haya tunayoyaona yapatikane zaidi na yazidi kuimarisha uchumi wetu.

Ndugu Wananchi,
Jitihada kubwa imefanywa na Serikali katika kuimarisha sekta ya Kilimo kwa lengo la kuhakikisha kuwa uhakika wa chakula na lishe unakuwepo. Serikali imeendelea kutoa ruzuku ya asilimia 75 kwa wakulima ya gharama za pembejeo za kilimo na huduma za matrekta kwa Unguja na Pemba. Katika msimu wa kilimo wa mwaka 2015/2016, tayari tani 750 za mbolea na lita 15,000 za dawa ya kuulia magugu zimenunuliwa kwa lengo kuwapa wakulima, ili kuimarisha kilimo. 

Kuhusu kilimo cha mpunga cha umwagiliaji maji, Serikali imekamilisha awamu ya kwanza ya Utekelezaji wa Mradi wa Ujenzi wa Miundombinu ya umwagiliaji maji ambao ukimalizika utaongeza uzalishaji wa mpunga kutoka kiwango cha sasa cha wastani wa tani 30,000 kwa mwaka hadi kufikia tani 45,000 kwa mwaka.  Shughuli za utafiti katika Taasisi ya Kilimo Kizimbani zimeimarishwa.  Kuhusu Chuo cha Kilimo cha Kizimbani, jumla ya wahitimu 93 wamemaliza masomo yao Stashahada na Cheti katika mwaka 2015 na tunatarajia wahitimu hawa wataajiriwa, ili kuongeza nguvu shughuli za ugani na ufugaji. 

Kwa upande wa uendelezaji wa maliasili zetu, Serikali inaendelea kusimamia ulinzi na udhibiti wa misitu yetu ikiwemo msitu wa Jozani Unguja na msitu wa Ngezi Pemba na misitu mingine ya asili kwa kushirikiana na wananchi.  Juhudi zitaendelea kufanywa kuwahamasisha wananchi juu ya ufugaji nyuki wa kisasa.

Ndugu Wananchi,
Jitihada kubwa zilifanywa katika kuiendeleza sekta ya uvuvi.  Katika mwaka 2015, kiwango cha samaki waliovuliwa kilifikia tani 31,439.0 zenye thamani ya TZS bilioni 123.80 ikilinganishwa na tani 30,108.6 zenye thamani ya TZS bilioni 116.3 zilizovuliwa mwaka 2014 sawa na ongezeko la asilimia 6.  Uzalishaji wa zao la mwani umeongezeka kutoka tani 13,301 mwaka 2014 hadi kufikia tani 15,076 mwaka 2015.  Ongezeko hili ni sawa na asilimia 13.

Hivi karibuni Serikali inatarajia kuanza utekelezaji wa mradi wa ujenzi wa kituo cha kuzalisha vifaranga vya samaki huko Beit el Ras kwa ufadhili wa Shirika la Maendeleo la Korea (KOICA). Kadhalika, Serikali imetiliana saini makubaliano ya awali na Kampuni ya Hairu kutoka Sri-Lanka ambayo itawekeza katika kiwanda cha kutengeneza boti zenye urefu wa mita 6, na mita 9 kwa ajili ya wavuvi wadogo na mita 18 zitakazofika bahari kuu.  Vile vile, kampuni hiyo itaweka mitambo ya kusindika samaki na mazao mengine ya baharini. 

Kadhalika, Serikali inategemea kuanzisha mradi wa ujenzi wa diko la kisasa Malindi katika mwezi wa Novemba, 2016.  Mradi huu unafadhaliwa na Serikali ya Japan na unategemewa kugharimu Dola za Kimarekani milioni 9.3 na unatarajiwa kukamilika katika kipindi cha miaka miwili.  Madhamuni makubwa ya mradi huu ni kuwawezesha watumiaji wa diko la Malindi kuuza na kununua samaki wao wakiwa katika kiwango bora, kuwaongezea tija wavuvi, wachuuzi, madalali na wafanyabiashara wadogo wa diko hilo pamoja na kuweka mazingira mazuri ya kuweka vyombo vya uvuvi bandari.  


Ndugu Wananchi,  
Kuhusu sekta ya ufugaji, juhudi kubwa zimefanywa ya kuwaendeleza wafugaji wetu kupitia Programu mbali mbali. Juhudi hizo zimeleta hamasa katika ufugaji wa kisasa na kuongeza idadi ya wafugaji wa ng’ombe na mbuzi wa maziwa kutoka wafugaji 9,795 mwaka 2014 hadi kufikia 10,082 mwaka 2015 sawa na ongezeko la asilimia 2.9. Juhudi hizi zimepelekea kuwepo kwa ongezeko la uzalishaji wa nyama na maziwa. 

Kwa lengo la kuwaendeleza wafugaji, jumla ya wafugaji 16,819 walitembelewa na kupatiwa mafunzo ya kitaalamu ya ufugaji bora wa ngo’mbe, mbuzi, kuku na mifugo mingine.  Idadi hiyo ni sawa na asilimia 84 ya lengo la kuwafikia wafugaji 20,000. Vile vile, wawekezaji wa ndani wameshajiishwa, ili wawekeze katika vikundi vidogo vidogo vya kuongeza thamani bidhaa za mifugo.  Aidha, kwa lengo la kukabiliana na maradhi mbali mbali ya mifugo,  Serikali inaendelea kuziimarisha huduma za uchunguzi wa maradhi ya mifugo kwa kuongeza wataalamu, vifaa na kuimarisha miundombinu ya maabara huko Maruhubi pamoja na kuendeleza ujenzi wa miundombinu ya mifugo ikiwemo vituo vya karantini na vituo vya uzalishaji.

Ndugu Wananchi,
Katika kukabiliana na changamoto za kimazingira, Serikali imeandaa na kupitisha sheria mpya ya usimamizi wa mazingira Zanzibar Nambari 3 ya mwaka 2015.  Lengo kuu la sheria hiyo ni kuimarisha uhifadhi wa mazingira nchini.  Aidha, kupitia sheria hiyo, Serikali imeanzisha Mamlaka ya Usimamizi wa Mazingira Zanzibar (ZEMA) ili kuyashughulikia masuala muhimu yanayohusu mazingira na kuhakikisha kuwa kila mmoja wetu anazingatia masharti ya sheria ya mazingira.

Jitihada zinaendelea kuchukuliwa na Serikali kwa kushirikiana na washirika wa maendeleo katika kukabiliana na athari za kimazingira pamoja na kuchukua hatua madhubuti za kudhibiti vitendo vya uharibifu wa mazingira vinavyosababishwa na shughuli za ujenzi, ukataji wa miti ovyo, utupaji wa taka za plastiki ngumu na vifaa vya kielektroniki. Katika kukabiliana na uharibifu wa mazingira jumla ya mikoko milioni 50 sawa na hekta 20 zimepandwa katika maeneo tisa ya Unguja na Pemba ili kuhuisha maeneo yaliyokatwa mikoko. 

Ndugu Wananchi,
Kuhusu miundombinu, katika  mwaka 2015 Serikali imekamilisha ujenzi wa barabara za lami mbili ambazo ni barabara ya Konde hadi Wete (km.15) na kutoka Wete hadi Konde (km.15).  Ujenzi wa barabara za lami sasa unaendelea katika barabara  ya Ole hadi Kengeja huko Pemba (km. 35). Kwa barabara za Unguja ujenzi unaendelea kwa barabara za Jendele kupitia Cheju hadi Kaebona (km. 11.7) na Koani hadi Jumbi (km. 6.3) na Mwanakwerekwe  hadi Fuoni (km. 4).  Kadhalika, Serikali inaendelea kuifanyia matengenezo makubwa ya barabara ya Ole hadi Konde kuanzia eneo la Meli 5 hadi Chwale (km. 13) huko Pemba kwa kufumuliwa na kutiwa lami upya.

Katika mwaka wa fedha 2015/2016, Serikali kwa upande wa Unguja ina lengo la kujenga barabara ya Bububu kupitia Mahonda hadi Mkokotoni (km30), barabara ya Matemwe-Mbuyutende-Muyuni (km 11.5), Pale hadi Kiongele (km 5), Mkwajuni-Kijini-Mbuyutende (km 9),  barabara kutoka Fuoni hadi Kombeni (km 7).  Kwa upande wa Pemba  itajengwa upya barabara ya Wete hadi Chake Chake (km 22.1).  Wito wangu kwa wananchi ni kuendelea kuzitunza barabara zetu na kutoa ushirikiano kwa Serikali na wakandarasi wanaojenga barabara zetu.

Ndugu Wananchi,
Kuhusu ujenzi wa bandari mpya ya Mpigaduri, Serikali imekamilisha matayarisho yote ya bandari hiyo katika mwaka 2015.  Ujenzi wa bandari hii unategemewa kuanza katika robo ya kwanza ya mwaka 2016.  Aidha, katika mwaka 2015, Serikali imejenga gati ndogo katika Kisiwa cha Tumbatu inayotarajiwa kumalizika Februari, 2016 na imekamilisha matengenezo ya jengo la abiria katika bandari kuu ya Malindi.

Katika azma ya kuimarisha usafiri wa baharini, Serikali ilitengenezesha meli mpya MV Mapinduzi II katika kampuni ya Daewoo ya Jamhuri ya Korea.  Meli hio iliwasili nchini tarehe 2 Disemba, 2015.  Meli hiyo yenye uwezo wa kuchukua abiria 1,200 na mizigo tani 200, imeanza ratiba zake tarehe 8 Januari, 2016 kwa safari ya kwenda Pemba.  Vile vile, Serikali imeamua kununua meli nyengine mpya ya mafuta mwaka huu.

Ndugu Wananchi,
Katika hatua za kuimarisha usafiri wa anga, Serikali imechukua hatua madhubuti ya kukamilisha ujenzi wa jengo jipya la abiria katika Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Abeid Amani Karume. Katika mwaka 2015, tuliukamilisha na kuuzindua mradi wa ujenzi wa maegesho ya ndege na njia za kupitia ndege katika kiwanja hicho.

Aidha, Kiwanja cha Ndege cha Pemba kimeimarishwa kwa kutiwa taa za kuongozea ndege za kisasa.  Mradi huo umekamilia na kuzinduliwa tarehe 7 Januari, 2016.  Hatua inayofuata sasa ni ujenzi wa  jengo jipya la abiria la kisasa, kuongeza urefu wa njia ya kurukia na kutulia ndege (Runway) kutoka urefu wa sasa 1.5km hadi kufikia 2.5km. Katika kutekeleza mpango huu, Serikali tayari imekubaliana na Benki ya Maendeleo ya Afrika (ADB) katika utekelezaji wa mradi huo.

Ndugu Wananchi,
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imeendelea na kazi ya usambazaji wa umeme vijijini.  Katika kipindi cha Januari hadi Novemba, 2015, kazi kubwa ya uwekaji wa laini za umeme imefanywa,  ambapo kilomita 47.25 za laini ndogo na kilomita 31.85 za laini kubwa ya umeme zimewekwa Unguja na Pemba.  Kazi ya kupeleka umeme katika visiwa vya Makoongwe na Kisiwapanza huko Pemba imekamilika.  Nalipongeza Shirika la Umeme la Zanzibar (ZECO) kwa kukamilisha kazi ya kuvusha umeme chini ya bahari na kuupeleka kwenye visiwa hivi kwa wakati uliopangwa.  Kisiwa cha Shamiani kilichopo katika Wilaya ya Mkoani  kinatarajiwa kupatiwa umeme katika mwaka huu wa fedha, 2015/2016.

Ndugu Wananchi,
Vile vile, katika jitihada za kushughulikia utafutaji wa mafuta na gesi, Serikali tayari imekamilisha Rasimu ya Sera ya Mafuta na Gesi.  Kuhusu Sheria ya Mafuta na Gesi asilia, rasimu yake ipo katika hatua za mwisho za matayarisho na inatarajiwa kukamilika baada ya muda si mrefu.    Nachukua nafasi hii kwa kumpongeza kwa dhati Rais Mstaafu wa Serikali ya Awamu ya Nne, ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Jakaya Mrisho Kikwete kwa kuhakikisha kwamba kabla ya kuondoka madarakani, suala la Zanzibar kusimamia mafuta na gesi asilia  wenyewe, linapatiwa ufumbuzi. Sheria ya Bunge ya 2015 ilitungwa ambapo sasa Zanzibar itakuwa na uwezo wa kuchimba mafuta na gesi yake  kwa kutunga sheria yake wenyewe itakayosimamia nishati hii pamoja na faida zake zote.  Hatua hii tuliyoifikia ni kubwa kwa ajili ya maendeleo ya Zanzibar. 

Ndugu Wananchi,
Jitihada kubwa zimefanywa na Serikali kwa kushirikiana na washirika wa maendeleo katika kuimarisha elimu.  Idadi ya skuli za maandalizi zimeongezeka na zimefikia 270 katika mwaka 2015,  skuli za msingi zimeongezeka kutoka skuli 359 mwaka 2014 hadi skuli 370 mwaka 2015 na skuli za sekondari zimeongezeka na kufikia skuli 263 mwaka 2015 kutoka skuli 210 mwaka 2014.

Serikali kwa kushirikiana na Washirika wa Maendeleo ina mpango wa kujenga skuli za msingi mpya 11 katika mwaka huu wa fedha wa 2015/2016. Kati ya skuli hizi, skuli 9 ni za ghorofa, maandalizi ya ujenzi wa skuli hizi yameshaanza ambapo fedha za mradi huo zitatokana na Mfuko wa OPEC.

Aidha, vituo vipya vya mafunzo ya amali vitajengwa kuanzia mwaka huu huko Makunduchi katika Mkoa wa Kusini Unguja na Mtambwe kwa Mkoa wa Kaskazini Pemba kwa mkopo wa Benki ya Maendeleo ya Afrika, ili kuwapa fursa vijana kujifunza kazi za amali zikiwemo ufundi wa aina mbali mbali.

Ndugu Wananchi,
Elimu ya juu inayotolewa na vyuo vikuu viliopo Zanzibar inaendelea kuimarishwa kwa kuongezwa Idara mpya na vitivo vya vyuo hivyo. Idadi ya wanafunzi wa vyuo vikuu vitatu vya Zanzibar imefikia 5,923, hadi kufikia mwezi wa Novemba mwaka 2015. Aidha, kwa kushirikiana na Serikali ya Falme ya Saudi Arabia, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ina mpango wa kujenga Chuo Kikuu kipya katika eneo la Dole. Idadi ya wanafunzi wanaopata mikopo katika vyuo vya ndani na nje ya Tanzania sasa imefikia 3,016 ambapo jumla ya TZS bilioni 9.3 zilitengwa mwaka jana kukidhi mikopo hiyo.  Hadi sasa wanafunzi 1,016 wameanza kurejesha mikopo yao kati ya wanafunzi 3,800 waliohitimu masomo yao.

Ndugu Wananchi,
Jitihada kubwa zimefanywa katika kuimarisha upatikanaji wa huduma za maji safi na salama kupitia miradi na programu mbali mbali za maji mijini na vijijini.  Hali ya upatilkanaji wa maji safi na salama imefikia wastani wa asilimia 87 mijini na asilimia 70 katika vijiji, katika mwaka 2015.  Lengo la Serikali ni kuimarisha upatikanaji wa huduma hizo hadi kufikia asilimia 97 katika miji na asilimia 85 katika vijiji ifikapo mwaka 2020.

Aidha, tunatarajia kulipatia ufumbuzi, tatizo la maji safi na salama katika Manispaa ya mji wa Zanzibar kufuatia kutiwa saini Mkataba wa Mradi wa Maji Mjini tarehe 29 Disemba, 2015 unaogharimu  Dola za Kimarekani milioni 21.  Mradi huo unatarajiwa kumalizika katika miezi 18 ijayo.

Ndugu Wananchi,
Katika mwaka 2015 jitihada zetu za kuiendeleza Hospitali ya Mnazi mmoja kuwa ya Rufaa zimefanikiwa sana.  Ujenzi wa jengo la utibabu wa watoto na wagonjwa wenye matatizo ya figo unaendelea vizuri ambapo tarehe 5 Januari, 2016 umewekewa jiwe la msingi pamoja na jengo lilokuwa la kiwanda cha madawa limeanza kufanyiwa ukarabati mkubwa kwa ajili ya huduma za wajawazito na watoto.    Majengo haya mawili yanagharamiwa na Serikali ya Norway, Uholanzi pamoja na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar. 

Kazi za kuzipandisha daraja hospitali ya Koteji ya Makunduchi na Kivunge zinaendelea vizuri.  Kwa utoaji wa huduma, hospitali ya Makunduchi na Kivunge tayari zimefikia hatua nzuri cha kiwango cha hospitali za wilaya na kwa hospitali za Micheweni na Vitongoji kazi hio nayo inaendelea vizuri.

Ndugu Wananchi,
Katika mwaka wa 2015, hospitali ya Abdalla Mzee Pemba imeanza kujengwa upya kwa msaada wa Serikali ya Jamhuri ya Watu wa China.  Utakapokamilika ujenzi wa hospitali hii itakuwa ni ya kisasa yenye uwezo wa kutoa huduma zote za utibabu na uchunguzi wa maradhi na  itakuwa na hadhi ya hospitali ya rufaa ya Mkoa.

Kwa lengo la kuimarisha upatikanaji wa dawa,  Serikali imeongeza bajeti ya dawa kutoka TZS  bilioni moja kwa mwaka 2013/2014 hadi kufikia TZS bilioni 4.3 kwa mwaka 2015/2016. Gharama za kuchangia  huduma za uchunguzi wa maradhi kwa kutumia “X-Ray”, “CT-Scan” na “Ultra Sound”, zimeondolewa  hivi sasa zinatolewa bila ya malipo kwa wananchi wote. 

Nchi yetu imepiga hatua kubwa katika kupunguza vifo vya mama na watoto kutokana na kinamama kujifungulia hospitalini na kuenea kwa huduma za uzazi vijijini. Katika mwaka 2014, kiwango cha kinamama waliojifungulia hospitali kimefikia asilimia 67.8 ikilinganishwa na asilimia 56.1 ya mwaka 2013. Aidha, kutokana na jitihada za kuwasomesha madaktari tumepata mafanikio ya  kutia moyo katika kuimarisha utoaji wa huduma kwa uwiano wa daktari kwa wananchi wanaohudumiwa.  Kwa sasa uwiano wa daktari na idadi ya watu anaowahudumia ni daktari mmoja kwa watu 8,885 (1:8885), kutoka kiwango cha daktari mmoja kwa watu 9,708 (1:9708) mwaka jana.

Ndugu Wananchi,
Serikali imefanya jitihada kubwa katika kuimarisha huduma za kinga na tiba.  Katika kipindi cha mwaka 2015, Serikali iliweka mkazo maalum katika kuyakinga na kuyadhibiti maradhi ya kuambukiza na yasio ya kuambukiza ambayo yameendelea kuwa tatizo kwa watu wa Zanzibar.

Vita dhidi ya Malaria vimeendelezwa na kiwango cha malaria bado kipo chini ya asilimia moja.  Kazi ya usambazaji na ushajiishaji wa matumizi sahihi ya vyandarua, ufukizaji wa dawa na kuulia mbu majumbani pamoja na uchunguzi na tiba kwa wagonjwa wa Malaria inaendelezwa. Katika kupambana na Malaria, kati ya Julai 2014 hadi Machi 2015, jumla ya vyandarua 114,394 sawa na asilimia 51 ya makisio ya mwaka uliomalizika vimegawiwa. Aidha, jumla ya nyumba 70,368 zilikusudiwa kupigwa dawa ambapo utekelezaji halisi ni nyumba 66,497 sawa na asilimia 94.5 ya makisio.  Kuhusu uchunguzi wa vimelea vya Malaria, jumla ya watu 172,972 walichunguzwa ambapo watu 1,648 sawa na asilimia 0.9 waligundulika kuwa na vimelea vya maradhi ya malaria.

Kuhusu tatizo la kipindupindu ambalo lilianza mwishoni mwa mwaka 2015 zilifanyika jitihada kubwa katika kuyadhibiti maradhi hayo.  Jumla ya wagonjwa 843 waliripotiwa kupata kipindupindu, Unguja na Pemba.  Kwa bahati mbaya wapo wachache miongoni mwao waliofariki.  Hali ya maradhi ya kipindupindu imedhibitiwa na  kasi yake imepungua sana.  Naupongeza uongozi wa Wizara ya Afya kwa kazi nzuri ulioifanya.  Nawaomba wananchi waendelee kuzingatia maelekezo ya wataalamu wa afya kuhusu maradhi haya.

Ndugu Wananchi, 
Katika sekta ya habari, jitihada zimeendelea kuchukuliwa  katika kuimarisha shughuli za Shirika la Utangazaji la Zanzibar pamoja na Gazeti la Zanzibar Leo.  Kupitia Shirika la Utangazaji la Zanzibar (ZBC), Serikali imetekeleza vyema wajibu wake wa kuielimisha jamii na kuipa habari na burudani.  Matangazo ya radio na televisheni za ZBC yameendelea kurushwa hewani kwa saa 24.  Chaneli 2 za ZBC-TV (ZBC na ZBC2) zimeendelea kufanya kazi kwa ufanisi hasa katika kutengeneza vipindi vya kienyeji katika nyanja tafauti. Matangazo ya radio ya ZBC yameimarishwa na kusikika katika masafa ya kati na masafa ya mbali na kurudisha tena chaneli ya “Spice FM Radio”. 

Kadhalika, Shirika la Magazeti la Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar limeendelea kuimarisha huduma zake za kuwapasha habari za matukio mbali mbali wananchi na kuwashajiisha katika kushiriki masuala ya maendeleo kupitia gazeti la Zanzibar Leo linalotolewa kila siku.  Aidha, kupitia gazeti la Zaspoti; wananchi hupata habari mahsusi za michezo na utamaduni kutoka ndani na nje ya nchi.  Gazeti la Zanzibar Leo linazidi kupanua wigo kwa kuuzwa Unguja na Pemba pamoja na mikoa mbali mbali ya Tanzania Bara.

Ndugu Wananchi,
Jengo jipya la Chuo cha Uandishi wa Habari linakamilishwa ujenzi wake ulioanza Juni 2015 katika eneo la Kilimani na unatarajiwa kumalizika hivi karibuni.  Kukamilika kwa ujenzi wa jengo hili litatoa fursa kwa wanafunzi wengi zaidi kujifunza taaluma hiyo.

Aidha, Serikali iliahidi kujenga Studio ya kisasa ya muziki na filamu kwa ajili ya wasanii wa Zanzibar katika jengo lilokuwa la Sauti ya Tanzania Zanzibar liliopo Rahaleo.  Ahadi hio imetekelezwa  baada ya jengo hilo kukarabatiwa na vifaa vya studio vipya kununuliwa.  Studio hio ilizinduliwa rasmi tarehe 8 Januari, 2016. Studio hiyo itatumiwa na wasanii kufanya kazi zao kwa ufanisi mkubwa. Vile vile, Tamasha la Utamaduni wa Mzanzibari na Tamasha la Filamu la Nchi za Jahazi (ZIFF) yameendelea kufanyika na yanaendelea kutoa mchango mkubwa katika  kutoa ajira kwa vijana pamoja na kuchochea kukua kwa sekta ya utalii nchini.

Kuhusu sekta ya michezo, Serikali iliadhimisha kwa mafanikio makubwa siku ya mazoezi inayofanyika kila mwaka ifikapo tarehe mosi Januari kwa lengo la kuhamasisha umuhimu wa kufanya mazoezi, kwa madhumuni ya kuzitunza afya zetu. Ni jambo la kufurahisha kwamba mahudhurio ya mwaka huu ya wanamichezo yalitia fora.  Aidha,  mashindano ya riadha ya wilaya zote za Zanzibar yalifanywa kwa juhudi kubwa ili  kuimarisha michezo maskulini.  Kadhalika, katika kuiimarisha miundombinu ya michezo, kazi ya uwekaji wa mpira wa kukimbilia katika uwanja wa Gombani iliyoanza mwaka 2015 inatarajiwa kukamilika hivi karibuni.   Vile vile, kazi ya ujenzi wa uwanja mpya wa Mao-tse-tung itaanza rasmi mwezi Februari, 2016 na inatarajiwa kukamilika mwaka ujao.

Ndugu Wananchi,
Katika mwaka 2015 Serikali imeendelea kuchukua hatua ya kuimarisha maslahi ya wafanyakazi kwa kadri hali ya ukuaji wa uchumi wetu inavyoruhusu. Katika mwaka huo wa 2015, Serikali ilifanya marekebisho ya mishahara kwa watumishi wenye uzoefu na elimu ya kiwango cha Stashahada ambao utumishi wao umefikia zaidi ya miaka 15. Zoezi la kuwapanga watumishi wote wa Serikali kulingana na madaraja yao limekwishaanza kwa hatua za awali za kukusanya taarifa, ili kazi hiyo ifanywe kwa uangalifu mkubwa na kupata ufanisi. 

Serikali imeendelea kuchukua hatua ya kuwawezesha wananchi kiuchumi ili kuwajengea uwezo wa kujiajiri na kupambana na umaskini.  Kupitia Mfuko wa Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi, hadi kufikia mwezi Novemba 2015, jumla ya mikopo 286 yenye thamani ya TZS milioni 436.2 imetolewa. Mikopo hiyo imewanufaisha wananchi wapatao 8,976.  Kuanzia Januari hadi Novemba, 2015, jumla ya TZS milioni 397.2 zilikusanywa ikiwa ni marejesho ya mikopo hio. Aidha, Serikali ilisajili taasisi 4 za Wakala binafsi za ajira na kuongeza idadi ya taasisi hizo kufikia 8. Jumla ya vijana 240 wamepata ajira kupitia mawakala hao wa ajira.

Ndugu Wananchi,
Kwa lengo la kuwasaidia vijana kuondokana na tatizo la ajira, Serikali kupitia Mfuko wa Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi imeongeza fedha za dhamana katika Benki ya CRDB kutoka TZS milioni 100 hadi TZS milioni 150 katika mwaka 2015. Kutokana na hatua hiyo, Benki ya CRDB imeweza kutoa mikopo yenye thamani ya TZS milioni 975.3 kwa vijana 2,952. 

Ndugu Wananchi,
Miongoni mwa shabaha ya Mapinduzi ya mwaka 1964 ilikuwa ni kuwapatia wazee  waliokuwa hawana uwezo, matunzo mazuri ya maisha yao kwa kuwapatia nyumba bora za kuishi na huduma nyengine.  Hii ndio sababu iliyopelekea mara tu baada ya kufuzu kwa Mapinduzi, Serikali ilijenga nyumba za wazee za Sebleni, Selemu na  sehemu ya Limbani na kuwaweka wazee ambao wamepatiwa huduma za malazi, matibabu na fedha za matumizi.  Katika mwaka 2015, Serikali imelipa jumla TZS milioni 14.3 kila mwezi kwa wazee wanaotunzwa katika nyumba za Sebleni, Welezo Limbani na Makundeni.

Kwa lengo la kuwapunguzia ukali wa maisha wazee wastaafu, Serikali inaendelea na matayarisho ya uanzishwaji wa Mpango wa Pensheni Jamii kwa wazee waliofikia umri wa miaka 70 na kuendelea.  Zoezi la usajili linaendelea ambapo tayari jumla ya wazee 22,443 waliostaafu Serikalini na waliokuwa hawajafanya kazi Serikalini wamekwishasajiliwa. Utaratibu wa kuanza kuwalipa wazee hao kupitia mpango huu kiasi cha TZS 20,000 kwa mwezi, kitatolewa kuanzia mwezi Aprili mwaka huu wa 2016. Kwa wale waliostaafu Serikalini wataendelea kupata pensheni yao ya kisheria.

Ndugu Wananchi,
Kuhusu watu wenye ulemavu, Serikali imechukua hatua za kuhakikisha wanapatiwa haki zao na kuwekewa mazingira mazuri yanayozingatia mahitaji yao pamoja na kushirikishwa katika masuala mbali mbali ya kijamii na kitaifa.  Watoto wenye ulemavu wanapatiwa haki yao ya elimu katika skuli zetu kwenye mpango wa elimu mjumuisho.  Ujenzi wa majengo ya huduma umeendelea kufanywa kwa kuzingatia watu wenye mahitaji maalum.  

Kadhalika, jitihada zimefanywa na Serikali katika kuwashirikisha kinamama katika masuala ya maendeleo pamoja na kulinda haki zao kwa kupiga vita vitendo vyote vya udhalilishaji wanawake na watoto ambapo Serikali ilianzisha kampeni hiyo mwaka jana.  Kampeni hii inaendelea vizuri ingawa changamoto bado zipo. Wito wangu kwenu ni kuwa sote tushirikiane katika kuifanikisha Kampeni hii.

Ndugu Wananchi,
Pamoja na mafanikio yaliyopatikana katika sekta zote nilizozielezea katika kipindi cha mwaka mmoja uliopita wa 2015, vile vile, tulipata mafanikio makubwa katika taasisi za sheria na utawala bora.  Ni katika kipindi hiki ambapo Sheria ya Maadili ya Viongozi imetungwa na ipo tayari kutumika. Vile vile, katika kipindi hiki Serikali ilikabiliwa na changamoto kadhaa, katika utekelezaji wa mipango yake.  Baadhi ya changamoto hizo zimeanza kushughulikiwa na nyengine zinafanyiwa kazi.
Ndugu Wananchi, 
Nyote mtakumbuka kwamba, nchi yetu iliingia katika Uchaguzi Mkuu tarehe 25 Oktoba, 2015 ambapo wananchi wa pande zote mbili za Muungano walipata fursa ya  kuwachagua Viongozi wao.

Uchaguzi wa Viongozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania uliosimamiwa na Tume ya Uchaguzi ya Taifa ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania umemalizika na sote tunafahamu kwamba, Chama cha Mapinduzi kimepata ushindi mkubwa.  Kwa mara nyengine tena nampongeza Mheshimiwa Dk. John Pombe Magufuli kwa kuchaguliwa kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kuchaguliwa kuwa Makamu wake wa Rais.  Aidha, nawapongeza wabunge wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na madiwani waliochaguliwa kwa upande wa CCM. 

Kwa upande wa Zanzibar, Tume ya Uchaguzi iliufuta uchaguzi wa Zanzibar  tarehe 28 Oktoba, 2015, baada ya kubainika kutokea kwa kasoro kadhaa kama zilivyoelezwa na Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar.  Kadhalika, uamuzi huo wa Tume ulitangazwa katika Gazeti Rasmi la Serikali la tarehe 6 Novemba, 2015 kwamba Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar imeyafuta matokeo yote ya Uchaguzi Mkuu wa Zanzibar wa tarehe 25 Oktoba, 2015 na kwamba uamuzi wa Tume wa tarehe nyengine ya kurudiwa Uchaguzi Mkuu wa Zanzibar utatangazwa baadae.  

Kwa mujibu wa Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984 na Sheria ya Uchaguzi ya mwaka 1984 na Sheria ya Uchaguzi Namba 11 ya mwaka 1984, Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar ndio yenye jukumu la kusimamia na kuendesha uchaguzi wa Rais, Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi na Madiwani. Kwa hivyo, nawaomba wananchi waendelee kuishi kwa amani na kupendana huku tukisubiri Tume ya Uchaguzi Zanzibar itangaze tarehe nyengine ya kurudia uchaguzi.

Aidha, katika suala zima la hali ya kisiasa ya Zanzibar, iliyojitokeza baada ya kufutwa kwa Uchaguzi Mkuu, viongozi wenu tulishauriana tukutane ili tufanye mazungumzo ya kutafuta suluhu kwa njia ya amani, ili nchi yetu iendelee kuwa na amani, umoja na mshikamano. Hatimaye tulikubaliana tuanze mazungumzo hayo. Mazungumzo haya yanatuhusisha viongozi sita, tuliopo madarakani na waliostaafu mimi nikiwa Mwenyekiti. Mazungumzo hayo bado yanaendelea. Taarifa ya pamoja ya mazungumzo hayo itatolewa na wajumbe tunaofanya mazungumzo mara tu mazungumzo hayo yatakapokamilika.  Katika kipindi hiki bado nawaomba wananchi waendelee kuwa wavumilivu na wastahamilivu na waendelee na shughuli zao za maisha za kila siku kwa amani.

Ndugu Wananchi, 
Kudumishwa kwa Mapinduzi ya Zanzibar ambayo leo yametimiza miaka 52, lazima kwende sambamba na kudumishwa na kuendelezwa kwa Muungano wa Tanzania ambao ifikapo tarehe 26 Aprili mwaka huu wa 2016, utatimiza miaka 52 tangu kuasisiwa kwake.  Muungano wa Tanzania ni kielelezo muhimu cha umoja wa Watanzania na udugu wa damu uliopo tangu kale na dahari kwa wananchi wa pande mbili za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Katika kipindi chote tangu kuasisiwa kwake tarehe 26 Aprili, 1964, wananchi wameendelea kunufaika kiuchumi, kisiasa na kijamii pamoja na kujitokeza changamoto ambazo zimekuwa zikifanyiwa kazi kwa ufanisi mkubwa na Kamati ya pamoja katika Ofisi ya Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika Awamu ya Nne.

Napenda nimhakikishie Mheshimiwa John Pombe Magufuli Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Watanzania na wote kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar,  Awamu ya Saba, itaendelea kuwa muumini wa dhati wa Muungano wa Tanzania na kuendelea kuyatekeleza kwa vitendo kwa malengo yale yale ya Waasisi wetu,  Marehemu baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na Marehemu Mzee Abeid Amani Karume.

Ndugu Wananchi,
Mafanikio tunayoyapata yanatokana na kuwepo kwa hali ya amani na utulivu nchini.  Natumia fursa hii kusisitiza kauli yangu niliyoitoa tarehe 26 Juni, 2015 katika hotuba yangu ya kulivunja Baraza la Nane la Wawakilishi, kwamba ni jukumu la viongozi wote wa Serikali, wanasiasa, viongozi wa madhehebu ya dini, viongozi wengine katika jamii na wananchi wote kutekeleza wajibu wetu na kuhakikisha tunadumisha amani na utulivu na kufuata sheria.  Sote tuna wajibu mkubwa wa kuitii Katiba ya Zanzibar na Sheria zake na kutambua kuwa ni msingi muhimu wa kulinda na kuendeleza amani na utulivu wetu.

Katika kipindi chote cha Uongozi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Awamu ya saba, nimeridhishwa sana na kazi nzuri inayofanywa na vyombo vyetu vya ulinzi na usalama vya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Idara Maalum za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kusimamia amani na usalama nchini. Napenda niwahakikishie wananchi wote kuwa Serikali zetu zote mbili; Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar zitaendelea kuchukua hatua madhubuti katika kuhakikisha kuwa amani, utulivu na usalama vinaendelea kudumishwa  nchini.  Nchi yetu inaongozwa kwa Katiba na Sheria na hivyo hakuna mtu au taasisi yoyote iliyo juu ya Katiba na Sheria.  Kwa mnasaba huo, suala la kutii Sheria na Katiba ya nchi halina mbadala wala mjadala.


Ndugu Wananchi,
Kwa niaba yenu natoa shukurani kwa nchi rafiki, mashirika ya Kimataifa na washirika wetu wote wa maendeleo kwa kushirikiana nasi katika utekelezaji wa mipango yetu ya maendeleo.  Napenda nikiri kuwa mafanikio tuliyoyapata, yametokana na jitihada zetu za pamoja katika utekelezaji wa mipango yetu ya maendeleo kwa kukuza uchumi na kuimarisha ustawi wa jamii. Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inathamini ushirikiano wetu na itauendeleza kwa lengo la kupiga hatua zaidi za maendeleo.

Natoa shukurani zangu tena kwa Viongozi wote waliohudhuria katika sherehe hizi wakiongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.  Natoa shukurani Maalum kwa Wasaidizi wangu; Makamu wa Kwanza wa Rais, Maalim Seif Sharif Hamad na Mhe. Makamu wa Pili wa Rais, Balozi Seif Ali Iddi kwa kunisaidia kuiongoza Zanzibar kwa mafanikio. Aidha, nawashukuru Mawaziri wote, Makatibu Wakuu, Wakurugenzi, Viongozi mbali mbali wa Serikali na Wafanyakazi wote kwa jitihada zao katika kuwatumikia wananchi.

Ndugu Wananchi,
Nakamilisha hotuba yangu kwa kutoa shukurani na kuipongeza Halmashauri ya Maadhimisho ya Kitaifa inayoongozwa na Makamu wa Pili wa Rais Mheshimiwa Balozi Seif Ali Iddi kwa kazi nzuri iliyofanywa ya kuyafanikisha maadhimisho ya mwaka huu.  Navipongeza kwa dhati Vikosi vyote vya Ulinzi kwa gwaride zuri lenye ukakamavu.  Nawashukuru washiriki wote wa Maandamano na vikundi vya sanaa na burudani vilivyotumbuiza na kuongeza hamasa katika siku hii ya kilele. Kadhalika, natoa shukurani zangu kwa waandishi wa habari na wamiliki wa vyombo vya habari kwa kuzitangaza sherehe zetu kwa ufanisi mkubwa tangu tulipoanza tarehe 3 Januari, 2016.

Natoa shukurani zangu maalum kwenu wananchi nyote kwa kushiriki kwa wingi katika matukio mbali mbali tokea tulipoanza Sherehe za Maadhimisho ya miaka 52 ya Mapinduzi na leo katika siku hii ya kilele.  Aidha, nakushukuruni kwa kuonesha umoja na mshikamano na kushereheka Sherehe hizi kwa amani, hamasa kubwa na uzalendo.  Hiki ni kielelezo muhimu kwamba wananchi wa Zanzibar na Tanzania kwa jumla tunayaenzi na tunayadumisha Mapinduzi kama ni msingi muhimu wa uhuru wetu na maendeleo ya nchi yetu. Tuendelee kusimamia amani, umoja na mshikamano ambazo ni nguzo muhimu kwa maendeleo yetu. Tumuombe Mwenyezi Mungu atupe nguvu za kuitekeleza mipango yetu ya maendeleo kwa ufanisi zaidi.

Nakutakieni kheri na baraka za mwaka mpya wa 2016.
MAPINDUZI DAIMA
MUNGU IBARIKI ZANZIBAR
MUNGU IBARIKI TANZANIA
MUNGU IBARIKI AFRIKA.


Ahsanteni kwa kunisikiliza.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.