Waziri wa Ujenzi, Mawasiliano na
Uchukuzi, Prof Makame Mbarawa ametoa pongezi kwa kampuni mpya ya simu ya Halotel
kwa juhudi zake inazofanya katika kutekeleza mkakati wa kuhakikisha
huduma ya mawasiliano inapatikana maeneo ya vijijini.
Pamoja na ongezeko la zaidi ya asilimia 16 la idadi ya watumiaji wa simu za
mikononi nchini bado tatizo la upatikanaji wa huduma ya mawasiliano kwa maeneo
ya vijijini imekuwa ni changamoto.
Prof Mbarawa alisema serikali
imekuwa inafanya juhudi mbalimbali ili kuziba pengo la upatikanaji wa huduma ya
mawasiliano kati ya maeneo ya vijijini na mijini, na hivyo mwaka 2006 mfuko wa mawasiliano
kwa wote ulianzishwa kwa lengo la
kuhakikisha upatikanaji wa huduma za mawasiliano katika maeneo ya vijijini na
mijini.
'Kulikuwa na mwamko mdogo kutoka kwa
makampuni ya simu katika kupeleka mawasiliano vijijini kutokana na mazingira yake
na changamoto kama vile kuwa na idadi ndogo ya wakazi, ndio maana serikali ikaanzisha
mfuko wa upatikanaji wa huduma ya mawasiliano kwa wote ili kusaidia katika zoezi
la utekelezaji wa upanuzi wa huduma ya mawasiliano' alisema Mbarawa.
Hata hivyo, Prof Mbarawa amebainisha
kuwa bado mwitikio wa uombaji wa zabuni kwa ajili ya jitihada za kupanua
mawasiliano maeneo ya vijijini umekuwa ni mdogo sana na hivyo basi kusababisha maelfu
ya vijiji kukosa huduma ya mawasiliano na hivyo kuendelea kukithiri kwa hali ya umaskini .
'Wakati kampuni ya simu ya Halotel
ilipokuja nchini na mkakati wa kuwekeza
maeneo ya vijijini, sisi kama serikali tuliwapokea kwa mikono miwili na
tukaahidi kuwasadia baadhi ya mambo ili kurahisisha utekelezaji wa zoezi hilo,
lakini pia tukawapa masharti ya kuhakikisha wanaunganisha mawasiliano ya
mtandao kwa ofisi za vijiji 150, hospitali za umma 150, vituo vya polisi 150, pamoja
na ofisi za posta 65 na pia shule 450 'alisema Prof Mbarawa.
Hadi sasa, Kampuni ya simu ya
Halotel kwa sasa imeunganisha huduma ya
mawasiliano kwa vijiji 1800 ambavyo
vilikuwa havina huduma hiyo, na kufikia mwishoni mwa mwaka huu kampuni ya simu
ya Halotel itakuwa imeunganisha vijiji
vingine 1500 kwa mara ya kwanza ili kuhakikisha huduma bora ya mtandao wa 3G.
‘Kampuni ya Halotel imeunganisha zaidi
ya watumiaji wa huduma ya simu 1,800, ambao
kabla walikuwa hawajaunganishwa,na muhimu zaidi, wameunganishwa na mtandao wa kasi
wa 3G kupitia fiba yenye kilomita 18,000 na hivyo kusaidia watumiaji wa huduma
hiyo kupatikana mahali popote na kwa wakati wowote ‘ alisema Naibu Mkurugenzi
Mtendaji wa kampuni ya simu ya Halotel, Le Van Dai.
Serikali ya Tanzania na mshirika wake Kampuni ya Halotel wamewekeza jumla
ya dola za kimarekani billioni moja sawa na trilioni 2 za kitanzania katika
kutekelezeka upanuzi wa huduma ya mawasiliano kwa mikoa mikoa 26, ikiwa ni pamoja na utekelezaji wa
kuunganisha vijiji 1,500 kupitia mkonga wa mawasiliano unaovuka kilometa 2,500
pamoja na na kusambaza kilometa 18,000 za fiba nchini kote, na hivyo kuifanya kampuni
ya simu ya Halotel kuwa mtandao ulionea zaidi nchini .
No comments:
Post a Comment