Habari za Punde

Hotuba ya Dk Shein aalipofungua michezo ya Zahlife

HOTUBA YA RAIS WA ZANZIBAR NA MWENYEKITI WA BARAZA LA MAPINDUZI MHE. DK. ALI MOHAMED SHEIN, KATIKA UFUNGUZI WA MASHINDANO YA MICHEZO YA VYUO
VIKUU NA TAASISI ZA ELIMU YA JUU ZANZIBAR
(ZAHILFE - GAMES) UWANJA WA AMAAN ZANZIBAR
TAREHE 21 MEI, 2016


Mheshimiwa Waziri wa Elimu na Mafunzo ya
Amali, Zanzibar,

Mheshimiwa Waziri wa Habari, Utalii, Utamaduni na
Michezo, Zanzibar,

Mwenyekiti wa Baraza la Michezo, Zanzibar,

Waheshimiwa Mawaziri mbali mbali mliohudhuria,

Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa wa Mjini Magharibi,

Wajumbe wa Bodi ya Wadhamini wa Shirikisho la Vyuo
Vikuu na Taasisi za Elimu ya Juu, Zanzibar,

Viongozi mbali mbali wa Serikali mliohudhuria,

Wakuu wa Vyuo na Skuli mbali mbali mliohudhuria,

Wanamichezo na Wanafunzi wote,

Ndugu Wananchi,

Mabibi na Mabwana,

Assalamu Aleikum,

Kwanza kabisa, napenda nianze kwa kumshukuru Mola wetu Mtukufu Subhana Wataala; Mwingi wa Rehema kwa kutujaalia uhai na afya njema tukaweza kuungana na wanamichezo wenzetu wa Shirikisho la Vyuo Vikuu na Taasisi za Elimu ya Juu Zanzibar.  Pili, nachukua fursa hii kutoa shukurani za dhati kwa viongozi wa Shirikisho la Vyuo Vikuu na Taasisi za Elimu ya Juu Zanzibar (ZAHILFE) kupitia Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali kwa kunialika kuja kuungana na wanamichezo wenzangu kwa lengo la kuyafungua mashindano haya ya Shirikisho la Vyuo na Taasisi za Elimu ya Juu Zanzibar katika mwaka huu wa 2016.  Kwa hakika nimeupokea mwaliko huu kwa furaha na Ahsanteni Sana.

Ndugu Wanamichezo na Ndugu Wananchi,
Nachukua fursa hii kukupongezeni kwa dhati kabisa, kwani mmeamua kutekeleza kwa vitendo madhumuni ya sera ya michezo ya Zanzibar.  Sera ya michezo ya Zanzibar ya mwaka 2007 imeweka bayana umuhimu wa michezo kwa wanamichezo wote kutoka kwenye makundi tofauti katika jamii, zikiwemo Taasisi za Elimu ya Juu na Skuli kwa jumla.  Nimeridhishwa sana na jitihada za Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali kwa kusimamia vyema wajibu wa kuandaa mashindano ya michezo katika taasisi za elimu za ngazi zote. Lengo kubwa likiwa ni kuchangia jitihada zetu kwa pamoja katika kuwapata  wanamichezo bora wa Taifa na kugundua vipaji vya wachezaji kama ilivyoelekezwa katika sera ya michezo ya Zanzibar.  Hongereni Sana.


Mashindano haya ni kielelezo na nyenzo moja wapo ya kujenga umoja, maelewano na mshikamano wa kitaifa na kimataifa kwa wanavyuo, wanafunzi wa skuli na jamii kwa jumla.  Aidha, kulingana na mabadiliko ya kisiasa, kiuchumi na kijamii duniani kote, michezo hivi sasa imepata kipaumbele kikubwa mbali na ile dhana ya  tangu kale  ya kuwa michezo ni sehemu moja wapo ya burudani.  Kadhalika, michezo ni ajira kwa vijana wetu.  Naamini mnawajuwa kuwa hivi sasa vijana kadhaa wa Kitanzania ambao wanacheza soka la kulipwa nje ya nchi.  Vile vile, michezo kwa kiasi kikubwa husaidia kuimarisha nidhamu maskulini, vyuoni na katika jamii kwa jumla. Kwa upande wenu wanafunzi, nidhamu ina umuhimu mkubwa katika kupata matokeo mazuri kwenye masomo yenu.   Matarajio yetu ni kuwa kupitia michezo, wanafunzi mtakuwa na nidhamu na mahusiano mazuri kati yenu wenyewe kwa wenyewe pamoja na walimu wenu mnapokua darasani.

Ndugu Wanamichezo na Ndugu Wananchi,
Natambua kuwa nyinyi ni wanafunzi ambao mnahitaji kuimarisha afya zenu, kukuza taaluma na vipaji vyenu.  Hayo ni miongoni mwa matokeo ya kushiriki michezo.  Ili michezo iendelee kukua hapa nchini ni lazima ukuaji wa vipaji vya michezo uanzie kuandaliwa katika ngazi za maskuli, vyuoni na hatimae katika jamii yetu.  Kwa mnasaba huo, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Awamu ya Saba imeamua kulirudisha  vuguvugu la michezo katika skuli zetu na taasisi za juu za elimu. Katika kipindi cha kwanza cha Awamu ya Saba ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, tulianzisha Idara mpya ya Michezo na Utamaduni ndani ya Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali.  Idara hii imeanzishwa kwa lengo la kutekeleza Sera ya Taifa ya Michezo katika skuli ili tuibue, tukuze, tuimarishe na tuendeleze vipaji vya wanafunzi ili kupata wanamichezo bora katika nchi yetu. 

Idara hii imeanza kazi vizuri ambapo mwaka jana iliwandaa vyema wanafunzi wetu wa Sekondari kwa ajili ya kushiriki Mashindano ya Shirikisho la Skuli za Sekondari ya Afrika ya Mashariki (Federation of East African Secondary School Sports Association – FEASSSA ) yaliyofanyika Dar es Salaam.  Timu zetu za mpira wa miguu wanaume pamoja na mpira wa mikono na wavu wanaume zilifanya vizuri kwa kushika nafasi ya tatu katika makundi yaliyozijumuisha timu za Kenya, Uganda, Sudan ya Kusini na Rwanda. Kwa upande wa michezo wa riadha, timu yetu ilishika nafasi ya nne kwa jumla.  Tutafanya kila jitihada ili matokeo ya mwaka jana, yatuongezee kasi na ari ya kufanya maandalizi bora zaidi ili tupate nafasi bora katika mashindano yajayo, jambo ambalo linawezekana.  Naelewa kuwa tayari maandalizi ya vijana wetu kwa ajili ya michezo ya Umoja wa Michezo ya Shule za Sekondari Tanzania (UMISSETA) yamekwishaanza.  Hata hivyo, nataka mfanye maandalizi ya kupata kushinda na sio kushiriki.

Natoa wito kwa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali kupitia Idara ya Michezo kushirikiana vyema na Uongozi wa Wizara ya Habari, Utalii, Utamaduni na Michezo na vyama vyengine vya michezo katika kuziandaa timu zetu mbali mbali zinazoiwakilisha nchi yetu ili kuiletea heshima yetu katika nyanja za michezo, kama ilivyokuwa miaka iliyopita.  Zanzibar ina historia kubwa, ndefu ya kufanya vizuri katika michezo ya Kimataifa na kwa hivyo ni lazima sote tushirikiane katika kuirudisha hadhi yetu hiyo ya nchi yetu.


Ndugu Wanamichezo na Ndugu Wananchi,
Nataka mkumbuke kuwa, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Awamu zote imekuwa ikijitahidi kuendeleza michezo kuanzia kwenye maskuli.  Lengo hili limedhihirika wazi mara tu baada ya Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar ya tarehe 12 Januari, 1964, Serikali ilipoanzisha Wizara ya Elimu na Mila. Wakati huo, shughuli zote za michezo na utamaduni ziliratibiwa na Wizara hiyo na wanafunzi wengi wa enzi hizo tulishiriki.  Mimi na wenzangu wengi tuliopo hapa ni miongoni mwa waliopata fursa ya kuonesha vipaji vyetu katika michezo ya riadha na mpira wa miguu, tulipokuwa tukisoma katika skuli za Msingi na Sekondari.  Tuliinukia kwenye michezo hio na wengine walioendelea kuvuma na kupata sifa kem kem.

Katika Awamu hii ya Saba ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, tumejidhatiti kuendeleza michezo maskulini na vyuo vya Elimu ya Juu kwa vile msingi hasa wa kupata vipaji hivyo huanzia maskulini.  Wengi mtakumbuka jitihada zetu, tulipoanzisha mashindano ya mbio za riadha ya Wilaya zote 10 za Zanzibar.   Kwa mara ya kwanza, niliridhishwa na vipaji vya vijana wetu,  nilivyoviona, kwa wanaume na kwa wanawake.  Kutokana na jitihada nilizoziona ndipo nilipofanya uamuzi wa kuwapa wanamichezo vifaa vya michezo vya aina mbali mbali Unguja na Pemba, ili viweze kuwasaidia.  Zaidi ya hayo, Serikali imeanza kuchukua hatua za kufundishwa kwa somo la michezo maskulini ambapo Idara ya Michezo na Utamaduni ilishirikiana na Taasisi ya Elimu Zanzibar kwa kutoa mafunzo kwa walimu wanaofundisha somo la michezo katika skuli za msingi.  Jumla ya walimu 574 walifaidika na mafunzo hayo.  Vile vile, wanafunzi wameshajiishwa kupenda michezo na kuunda klabu za michezo maskulini.  Hivi sasa tayari hamasa na vuguvugu la michezo maskulini limeanza kuonekana.  Nataka nielezee jinsi nilivyofarijika pale nilipoona michezo mbali mbali inayochezwa na vijana wetu kwenye kilele cha Miaka 50 ya Maadhimisho ya Elimu bila ya malipo waliponialika kuwa Mgeni Rasmi.  Aidha, leo hii tunashuhudia hamasa za michezo ya vijana wetu wa Taasisi za Vyuo Vikuu na Taasisi za Elimu ya Juu.  Sote tujipongeze kwa mafanikio haya.



Ndugu Wanamichezo na Ndugu Wananchi,
Katika hotuba yangu ya uzinduzi wa Baraza la Tisa la Wawakilishi, niliyoitoa tarehe 5 Aprili, 2016, nilieleza wazi dhamira ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Awamu ya Saba, katika kipindi chake cha pili tulichokianza. Niliwahakikishia wananchi kuzidisha juhudi katika kuyaendeleza mafanikio tuliyoyapata katika sekta ya michezo kwa kuyaimarisha mashindano ya riadha ya Wilaya na kuliimarisha Bonanza la Michezo na vikundi vya mazoezi tunalolifanya tarehe mosi ya kila mwaka.  Aidha, tutaongeza juhudi katika kuimarisha michezo maskulini na vyuo vya elimu ya juu ambapo katika kipindi hiki Serikali inadhamiria kulifundisha somo la michezo katika skuli 6 za sekondari zilizochaguliwa, Unguja 4 na Pemba 2.  Kadhalika, ujenzi wa uwanja wa Mao Tse Tung, utaanza Disemba mwaka huu na utiaji wa tartan katika uwanja wa Gombani nao unashughulikiwa.  Vile vile, Serikali ina mpango wa kujenga viwanja vya michezo katika kila Wilaya.  Hatua nyengine ni kuhamasisha michezo ya asili ya Zanzibar ikiwemo mashindano ya resi za Ngalawa, Bao, Karata, Mchezo wa Ng’ombe na kadhalika.  Watu wenye ulemavu nao tutawahamasisha kwa kuwapatia vifaa pamoja na vyama vya michezo vinavyohusika ili waweze kushiriki kikamilifu katika kuendeleza michezo.

Ndugu Wanamichezo na Ndugu Wananchi,  
Katika mashindano tunayoyazindua leo, wasia wangu kwenu ni kuwa mfuate taratibu na sheria za michezo. Mara nyingi michezo huwatayarisha na kuwaandaa vijana wenye maadili mazuri, wasikivu, watiifu na wenye nidhamu kwa jamii nzima, ikizingatiwa kuwa nyinyi ni viongozi wa kesho.  Hivyo mnahitajika sana kujijenga na kujipamba kwa kuwa  na maadili na kuwa na nidhamu nzuri, ili muweze kufanikiwa na kuishi maisha mazuri hapo baadae. Nidhamu inamuwezesha mtu kufanya kazi zake kwa mpangilio mzuri unaokwenda sambamba na malengo yanayokusudiwa. Hii itakuwa ndio njia ya uhakika ya kuyafikia malengo yoyote yale ya kupata elimu bora pamoja na mafanikio mema katika maisha yenu ya baadae.  Nasisitiza umuhimu wa nidhamu wakati wote wa mashindano haya na katika maisha yenu ya kutafuta elimu na khatima njema ya maisha yenu hapo baadae. 

Kadhalika, natoa wito kwa jamii yetu izingatie, iendeleze na isimamie dhana halisi ya michezo. Ifahamike wazi kwamba michezo sio  inayowafanya watoto wawe wacheza na watukutu.  Ucheza, utundu na utukutu kwa mtoto ni matokeo ya mambo mengine.  Lakini, michezo ina mchango mkubwa katika kuongeza ufahamu wa masomo na kuchangamsha akili ya mwanafunzi katika kukabiliana na masomo yake.  Miongoni mwa wanafunzi wanaofanya vizuri darasani na kufanikiwa katika masomo yao na baadae kwenye maisha wamo pia walioshiriki michezo.  Hili limethibitishwa na wataalamu.  Kwa hivyo, tusiwazuwie vijana wetu kushiriki katika michezo badala yake tuwashajiishe waipende na washiriki.

Ndugu Wanamichezo na Ndugu Wananchi,
Kabla sijamalizia hotuba yangu, natumia fursa hii kukukumbusheni kuwa wakati mnapofurahia michezo yenu hii, iwe michezo salama tangu mwanzo  leo hii hadi siku ya mwisho.  Natoa kauli hiyo, nikiimaanisha furaha yenu hii itaendelea kudumu iwapo tutaendelea kuwa salama na tuwe na tahadhari kubwa juu ya maradhi ambayo yameikumba nchi yetu yakiwemo maradhi ya kipindupindu, UKIMWI na matatizo yanayosababishwa na dawa za kulevya.  Ni imani yangu kwa sasa kila mmoja wetu anaelewa vyema jinsi madhara ya maradhi haya  yalivyotusibu katika jamii yetu.  Ni wajibu wetu kila tukipata fursa tuendelee kukumbushana ili tuchukue hatua za lazima za kukabiliana na maradhi hayo kwa kuwa huchangia katika kuzirudisha nyuma jitihada zetu za kuleta ustawi bora wa jamii yetu.  Maradhi haya yanachangia katika kupunguza nguvu kazi yetu kwa kasi kubwa. Miongoni mwa tahadhari mnazostahiki kuchukua ni kuwa waaminifu michezoni, kujiepusha na marafiki ambao si waadilifu, kuweka mazingira safi na kufuata maelekezo ya wataalamu wetu wa afya katika kukabiliana na maradhi hayo thakili.

Ndugu Wanamichezo na Ndugu Wananchi,
Kwa mara nyengine tena napenda niipongeze kwa dhati kabisa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali pamoja na Wizara ya Habari, Utalii, Utamaduni na Michezo kwa jitihada zao katika kuwaunganisha na kuwaweka pamoja wanafunzi wote wa Shirikisho la Vyuo Vikuu na Taasisi za Elimu ya Juu hapa Zanzibar, pamoja na Bodi ya Wadhamini ya Shirikisho na kuandaa mashindano haya yaliyofana sana.  Katika kuyafanikisha mashindano ya mwaka huu, nimesikia kuna waliochangia kwa njia mbali mbali.  Napenda niungane na waandaaji wa mashindano haya kwa kuwashukuru na kuwapongeza sana kwa moyo wao wa kizalendo.  Naipongeza Benki ya Afrika, Baraza la Manispaa Zanzibar, Halmashauri ya Wilaya ya Magharibi, Unguja, Mfuko wa Hifadhi ya Taifa (NSSF), Kituo cha Azam Media, ZSSF, Shirika la Bandari na wahisani wote waliosaidia kuyafanikisha mashindano haya yenye kauli mbiu inayohamasisha michezo, elimu bora pamoja na mazingira safi na salama ambayo ndio njia kuu ya kupambana na maradhi ya kuambukiza kikiwemo kipindupindu.

Ndugu Wanamichezo na Ndugu Wananchi,
Kabla sijamalizia kutoa nasaha zangu, napenda nisisitize kuwa michezo kama hii itumike katika kuwatafuta na kuwaandaa wanamichezo bora watakaoweza kuendelezwa na hatimae kuwapata wachezaji mahiri wa michezo mbali mbali watakaoiletea sifa nchi yetu katika medani za kimataifa.  Kwa hivyo, walimu wa michezo na waamuzi,  wahakikishe kuwa mashindano haya yanaendeshwa kwa kuzingatia sheria za michezo za kimataifa.  Vile vile, mashindano haya yawe ni maandalizi kwa timu zetu zinazotuwakilisha kwenye mashindano mengine.    Namaliza hotuba yangu kwa kukutakieni kila la kheri na mafanikio katika kipindi hiki cha mashindano.  Michezo ni furaha, michezo ni umoja, michezo ni amani na michezo ni afya.  Yazingatieni mambo hayo katika mashindano yenu.

Baada ya kusema hayo, sasa natamka kwamba Mashindano ya Michezo ya Shirikisho la Vyuo Vikuu na Taasisi za Elimu ya Juu Zanzibar ya mwaka 2016, yamefunguliwa rasmi.

Ahsanteni kwa kunisikiliza.


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.