Habari za Punde

Balozi Seif Atembelea Kiwanda cha Sukari Mahonda Zanzibar.

Meneja wa Kiwanda cha Sukari Mahonda Bwana Vicky Patel akimuonyesha Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi mfano wa uzalishaji wa Sukari { Sample } utakavyokuwa wakati watakapoanza uzalishaji rasmi wa sukari mwezi Julai Mwaka huu wa 2016. 
Baadhi ya mfano wa ujazo wa Sukari katika kiwango cha   Kilogramu moja, Tano na 50 utakavyofanywa na Kiwanda cha Sukari cha Mahonda wakati watakapoanza uzalishaji wao.Sukari hiyo imepewa jina la Kisiwa kulingana na mazingira halisi ya Visiwa vya Zanzibar kuzunguukwa na maji sehemu zote.( Picha na – OMPR – ZNZ.) 

Na Othman Khamis OMPR.
Uongozi wa Kiwanda cha Sukari Mahonda umeanza matayarisho ya kutengeneza mfano wa uzalishaji wa Sukari { Sample } baada ya kukamilisha kwa matengenezo makubwa ya Kiwanda hicho yaliyokwenda sambamba na ufungaji wa mashine zitakazozalisha sukari katika kiwango kikubwa zaidi.

Meneja wa Kiwanda hicho Bwana Vicky Patel alieleza hayo wakati akizungumza na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi Vuga Mjini Zanzibar akiuongoza ujumbe wa Viongozi Watatu wa Kiwanda hicho walipofika kumuonyesha mfano wa uzalishaji huo.

Bwana Vicky Patel alisema kwamba uzalishaji wa Sukari katika kiwanda hicho unatazamiwa kuanza rasmi mwezi Julai mwaka huu katika kiwango cha ujazo wa kilo moja, Tano na 50 wakilenga kuanzia kulitumia soko la ndani  ya Tanzania.

Alieleza kwamba Uongozi wa Kiwanda hicho tayari umeshajipanga pia kununua miwa kwa wazalishaji wadogo wadogo waliopatiwa mkopo wa fedha na Uongozi huo katika hatua ya awali ya matayarisho ya kuanzisha mashamba yao.

Meneja wa Kiwanda cha Sukari Mahonda alimueleza Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif kwamba Sukari itakayozalishwa na kiwanda hicho imepewa jina la Kisiwa linalofaana na mazingira halisi ya Zanzibar kuzungukwa na maji sehemu zote.

Akiangalia sampuli hiyo ya Sukari ya Kiwanda cha Sukari Mahonda Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alielezea hafaja yake kutokana na hatua ya maandalizi ya uzalishaji iliyofikiwa na Uongozi wa Kiwanda hicho.

Balozi Seif  alisema uzalishaji wa Sukari ndani ya Visiwa vya Zanzibar unaweza kusaidia kupunguza changamoto ya upungufu wa sukari  unaotokea baadhi ya wakati na kuwasumbua Wananchi walio wengi ndani ya eneo la Tanzania.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.