Habari za Punde

Hotuba ya Balozi Seif alipofunga mkutano wa pili wa BLW

HOTUBA YA MAKAMU WA PILI WA RAIS WA ZANZIBAR, MHESHIMIWA BALOZI SEIF ALI IDDI YA KUFUNGA MKUTANO WA PILI WA BARAZA LA WAWAKILISHI, ZANZIBAR TAREHE 29 JUNI, 2016

UTANGULIZI:
1.            Mheshimiwa Spika, awali ya yote napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu Mtukufu kwa kutujaalia uhai na afya njema na kutuwezesha kufanikiwa vizuri kushiriki na kukamilisha Mkutano huu wa Pili wa Baraza la Tisa la Wawakilishi ulioanza tarehe 18 Mei, 2016 kwa lengo la kujadili Bajeti ya Serikali yetu ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa mwaka wa fedha 2016/2017. Kwa uwezo wake Mola Mtukufu, kazi zote zilizopangwa katika ratiba ya mkutano huu wa pili tumezikamilisha kwa mafanikio mkubwa.

2.            Mheshimiwa Spika, shukrani maalum nazitoa kwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mheshimiwa Dkt. Ali Mohamed Shein, kwa kuendelea kuiongoza nchi yetu katika hali ya amani na utulivu. Tunamuomba Mwenyezi Mungu amzidishie uwezo, hekima na busara ili aendelee kuiongoza na kuzidi kuiletea maendeleo nchi yetu katika kipindi hiki cha pili cha uongozi wake.
3.            Mheshimiwa Spika, kwa heshima kubwa, napenda kutoa shukurani zangu za dhati kwako wewe binafsi, Naibu Spika, Wenyeviti na wasaidizi wako wote kwa kukusaidia kuliendesha Baraza hili Tukufu kwa umahiri na umakini mkubwa. Pia, nawashukuru Waheshimiwa Wenyeviti na Wajumbe wa Kamati mbali mbali za Kudumu za Baraza hili kwa michango, ushauri na maelekezo yao kwa Serikali katika utekelezaji wa majukumu yake.


4.            Mheshimiwa Spika, nawapongeza Waheshimiwa Wajumbe wote wa Baraza hili la Tisa la Wawakilishi, Mawaziri, na Naibu Mawaziri kwa umahiri wao mkubwa katika kuchangia mijadala na hoja mbali mbali ndani ya Baraza hili. Aidha, nawashukuru Makatibu Wakuu, Wakuu wa Mikoa, Wakuu wa Wilaya na Watendaji wote wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa kuendelea kutekeleza majukumu yao ya kila siku kwa mafanikio makubwa.

5.            Mheshimiwa Spika, nachukua pia fursa hii kuelezea kuridhika kwangu na upeo na uelewa mkubwa walionao Waheshimiwa Wawakilishi kwa jinsi walivyotoa michango ya kujenga na sio ya kubomoa, kushutumiana au kukomoana. Nawapongeza sana kwa uelewa na ukomavu wao kisiasa na jamii kubwa ya Wazanzibari na wengine wanajifunza kwa utendaji wetu vipi kiongozi anapaswa kuwa hasa anapojadili masuala ya wananchi.  Katika kuchangia hoja mbali mbali za Serikali, wapo waliochangia kwa hamasa, wapo waliochangia kwa upole, wapo waliochangia kwa jazba na hata kulia lakini wote hao nia yao ni kuikosoa na kuishauri Serikali ili ifanye kazi zake kwa usahihi zaidi.

6.            Mheshimiwa Spika, nimeona dalili ya baadhi yetu kutetea mambo ya kibinafsi kuliko yale ya wananchi walio wengi, hili naomba tuliache, tuwasilishe katika chombo chetu hichi mambo ambayo wananchi yanawagusa na ambayo wametutuma tuje kuyatetea, tupite kwa wananchi tujadiliane nao na mnachokubaliana nao ndicho tukiwasilishe katika Baraza hili Tukufu. Haitokuwa vyema tukaongea vitu ambavyo tukirudi Majimboni kwetu wananchi wakatueleza kuwa yale uliyokuwa unaongea Barazani sio shida zetu au sio tuliyoyapa kipaumbele.

7.            Mheshimiwa Spika, nachukua fursa hii kuwaomba Waheshimiwa Wawakilishi wajitahidi kuwatumikia wananchi wao kwa nguvu zao zote na hasa wale walioshinda katika Majimbo ambayo kipindi cha nyuma yakishikiliwa na wawakilishi wa Chama cha Upinzani, ambao wengi wao hawakuwa wanawaletea maendeleo wananchi wao ambao wengi wao walihama katika Majimbo yao na kukimbilia mijini. Na baadhi yao kutoka Majimbo ya Pemba walikimbilia na kuhamia Unguja.  Wananchi wa Majimbo hayo walikata tamaa na sasa nakuombeni sana mkae na wananchi hao na kuwarejeshea matumaini na pia waweze kuona faida ya kuwa na Wawakilishi kutoka CCM.

8.            Mheshimiwa Spika, naomba nitoe mwito maalum kwa Waheshimiwa Wawakilishi kutenga muda wa kutosha kuzisoma hotuba za bajeti na miswada inayowasilishwa na michango yetu ikakita katika vitabu au nyaraka zilizowasilishwa kwa kufanya rejea ya maeneo hayo na kushauri nini kifanyike.  Baadhi yetu tumeonekana kusikiliza msemaji aliyepita na kurejea yale yale hata kama hayamo katika hotuba inayojadiliwa, si vibaya kurejea au kuzungumza jambo ambalo halikutajwa katika hotuba husika mradi ina nia ya kujenga au kuondoa kero fulani inayowasumbua wananchi wetu hata wageni wanaotembelea nchi yetu.

9.            Mheshimiwa Spika, nimelazimika kutoa ushauri huu baada ya kuona wachache kati yetu wamekuwa wakitoa michango ambayo iko nje ya suala la msingi linazungumzwa au wanauliza kitu ambacho majibu yake yamo katika hotuba inayojadiliwa.  Tukisoma kwa makini na kuchangia baada ya kukielewa kilichowasilishwa tutaongeza ufanisi wa shughuli zetu kuokoa muda ambao tungeweza kuutumia kwa shughuli nyengine za Baraza letu Tukufu.  Aidha, wananchi wetu wanafuatilia kwa makini sana kinachowasilishwa na michango yetu na nimekuwa nikipokea maoni ya wananchi kuwa baadhi yetu tunatoka sana nje ya mada za msingi.

10.         Mheshimiwa Spika, kwa namna ya pekee naomba nimshukuru Mheshimiwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mheshimiwa Dkt. Ali Mohamed Shein, kwa kuunda Baraza la Mawaziri pamoja na Naibu Mawaziri lenye watu imara, mahiri, wenye ari ya kufanya kazi na wanaowajibika ipasavyo.  Kazi yangu katika Baraza lako Tukufu imekuwa nyepesi kutokana na utendaji wao mzuri. Napenda kuwapongeza Mawaziri hao na Manaibu wao kwa kazi nzuri wanayoifanya Barazani na kwenye Wizara zao.

11.         Mheshimiwa Spika, Mawaziri na Naibu Mawaziri wengi wana muda mchache katika ofisi zao, lakini kwa kipindi kifupi sana wameweza kuzielewa kazi zao na changamoto zinazowakabili. Kinachonipa faraja zaidi ni kuwa hoja za Waheshimiwa Wawakilishi zimeweza kujibiwa kwa usahihi na umakini mkubwa sana, nakupongezeni sana.
12.         Mheshimiwa Spika, naomba pia nipongeze mashirikiano ambayo yapo baina ya Waheshimiwa Wawakilishi na Mawaziri, hali inayopelekea kila changamoto inayojitokeza kupatiwa ufumbuzi kwa mashirikiano, huku ndiko kujenga nchi. Hatuwezi kupiga hatua ikiwa hatuna mshikamano na mashirikiano katika ujenzi wa nchi yetu. Siasa chafu kama zinazofanywa na wapinzani zinalenga kuipaka rangi ya ubaya nchi yetu na viongozi wake zimepitwa na wakati na tusiruhusu siasa uchwara kuenea nchini mwetu.

13.         Mheshimiwa Spika, kama nilivyokupongeza hapo awali, naomba niendelee kukupongeza na kutambua usimamizi wako wa chombo hiki kikubwa katika nchi yetu. Wewe mwenyewe binafsi, Naibu wako na Wenyeviti mmefanya kazi kubwa na ya weledi mkubwa sana, kuendesha vikao vya Baraza la Wawakilishi kuna changamoto nyingi ikiwamo kuzielewa Kanuni na Taratibu za Baraza hasa inapotokea mitazamo tofauti juu ya hoja au suala linalojadiliwa. Ninachoweza kusema ni kuwa chombo kimepata manahodha wanaokijua, wanaojua tunakoelekea na changamoto za kufikia tunakokwenda, hongereni sana Mhe. Spika.


TAARIFA YA MAMBO MBALI MBALI:
(i)                   HALI YA KISIASA:
14.         Mheshimiwa Spika, baada ya Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar kupitia Mwenyekiti wake kufuta matokeo ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba, 2015 kufuatia kubainika kwa kasoro nyingi ambazo zingeyafanya matokeo hayo kutokuwa ya uhuru na haki, Katibu Mkuu wa Chama cha CUF Maalim Seif Sharif Hamad amekuwa akipita maeneo mbali mbali kuwadanganya wananchi hasa wanachama wa chama chake na Jumuiya za Kimataifa kwamba, Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete alitoa amri kwa Mwenyekiti wa Tume ya Uchanguzi Zanzibar, Mhe. Jecha Salum Jecha, kufuta matokeo hayo jambo ambalo sio la kweli, na kauli hiyo ilikuwa kama tusi kwa Dk. Shein, maana amemaanisha kuwa kama Dk. Kikwete asingemwamuru Mhe. Jecha kufuta uchaguzi, Dk. Shein angekubali kudhumuliwa.  Hii ni porojo tu. 

15.         Mheshimiwa Spika, napenda ieleweke kuwa Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar ni chombo huru chenye mamlaka na kinafanya kazi zake bila ya kuingiliwa na mtu au chombo kingine chochote.  Maamuzi ya kufuta matokeo hayo yalikuwa ni halali baada ya kubainika kwa kasoro nyingi, ukiukwaji mkubwa wa sheria na kanuni za uchaguzi hasa Kisiwani Pemba. Tume ya Uchaguzi inafanya kazi zake ili kusimamia haki na kuhakikisha matakwa na ridhaa za wananchi katika kuwachagua viongozi wanaowataka zinatimia bila ghilba na udanganyifu wowote.

(ii)                  ZIARA ZA MAALIM SEIF SHARIF HAMAD:
16.         Mheshimiwa Spika, tokea kumalizika kwa uchaguzi wa marejeo uliofanyika tarehe 20 Machi, 2016 na CCM kupata ushindi wa kishindo, Katibu Mkuu wa Chama cha CUF, Seif Sharif Hamad pamoja na viongozi wengine wa chama hicho wamekuwa wakifanya ziara mbali mbali ndani na nje ya nchi. Serikali imezifuatilia kwa karibu ziara hizo na kubaini kwamba msingi wake ni kutapatapa kwa kiongozi huyu baada ya kushindwa uchaguzi huo wa marejeo. Ziara hizo zimekuwa ni muendelezo wa vitendo vya uchochezi na hujuma, kwani anayoyasema wakati wa ziara hizo yanaongeza chuki na uhasama miongoni mwa wananchi wa Zanzibar.  Tunayaona au kuyasikia yanayotokea huko Pemba hivi sasa.

17.         Mheshimiwa Spika, nawaomba wananchi wasibabaishwe na kauli hizo za Seif Sharif Hamad kwani haziwezi hata kidogo kuiteteresha Serikali halali inayoongozwa na Chama cha Mapinduzi iliyowekwa madarakani na wananchi wa Zanzibar katika uchaguzi wa marejeo uliofanyika tarehe 20 Machi, 2016. Wala kauli zao hizo haziwezi kututoa kwenye malengo yetu ya kuwaletea wananchi maendeleo.  Uchaguzi huo aliukataa yeye mwenyewe na kilichobakia ni kusubiri uchaguzi mwengine hapo mwaka 2020 panapo majaaliwa.  Huko nchi za nje nako alisikika akidai kuundwa kwa Serikali ya Mpito ya miezi sita itakayoongozwa na Mzanzibari asiyefungamana na upande wowote wa kisiasa, Zanzibar na baada ya hapo uitishwe Uchaguzi Mkuu utakaosimamiwa na Jumuiya au Taasisi ya Kimataifa.  Huu ni upuuzi mwingine kwani jambo hilo haliwezekani kutokea hata siku moja.  Tunachojua sisi ni kuwa uchaguzi umekwisha, uchaguzi mwingine hadi 2020.  Kabla ya hapo hakuna Serikali ya Mpito wala ya Mpeta.  Hapa ni Kazi tu ya kuwatumikia wananchi ya kuzitatua kero zao na kutekeleza ahadi tulizozitoa kupitia Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya 2015 – 2020.

(iii)                MATUKIO YA UHALIFU NA HUJUMA:
18.         Mheshimiwa Spika, nchi yetu imeshuhudia matukio mbali mbali ya uhalifu na hujuma yanayopangwa na kutekelezwa na baadhi ya wafuasi wa Chama cha Upinzani cha CUF wasioitakia mema nchi yetu, ikiwa ni utekelezaji wa maagizo ya viongozi wao ambao wana nia ya kuhatarisha hali ya amani na utulivu uliopo. Matukio hayo yamejitokeza kabla na baada ya uchaguzi wa marejeo uliofanyika tarehe 20 Machi, 2016, ikiwemo uchomaji moto nyumba, ofisi za CCM na vituo vya afya; wananchi kunyimwa au kubaguliwa kwenye huduma za kijamii; na kukata na kuharibu mikarafuu na mazao mengine, ikiwemo mpunga, muhogo, migomba na vipando vingine.

19.         Mheshimiwa Spika, Serikali inasikitishwa sana na matukio hayo, ambayo sio tu yanaathiri wananchi walengwa, bali pia yanaleta athari kubwa za kimazingira kutokana na uharibifu mkubwa wa miti ya mikarafuu na mazao mengine. Wanaofanya vitendo hivi ni wahujumu uchumi na watakaopatikana ni bora kushitakiwa chini ya Sheria ya Uhujumu Uchumi.

20.         Mheshimiwa Spika, uchunguzi uliofanywa na Jeshi la Polisi Zanzibar unaonyesha kwamba Chama cha CUF kimekuwa na mpango wa kuendeleza hujuma hizo katika maeneo mbali mbali, ikiwemo nyumba za Viongozi Waandamizi wa Serikali na Chama cha Mapinduzi.  Kwa mujibu wa uchunguzi huo, vitendo hivi vinatokana na maelekezo ya Chama cha CUF yaliyotolewa na Katibu Mkuu wao, Seif Sharif Hamad. Aidha, upo ushahidi wa kutosha kwamba Seif Sharif Hamad amekuwa akitoa hotuba za uchochezi kupitia mikutano yake ya ndani aliyoifanya katika maeneo mbali mbali, hasa Kisiwani Pemba.  Serikali inakamilisha taratibu za kuwachukulia hatua za kisheria wale wote waliohusika na vitendo hivyo.  Wasije wakailalamikia Serikali kwa hatua itakazochukua.

Nichukue fursa hii kwa niaba ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kutoa pole kwa wananchi wa Pemba kwa madhila waliyoyapata ya kuharibiwa na kuchomewa nyumba zao, kukatiwa vipando vyao mbali mbali na kubaguliwa, Serikali iko pamoja nao.  Serikali itawashughulikia wahalifu hao vipasavyo.

MARADHI YA KIPINDUPINDU:
21.         Mheshimiwa Spika, kama tunavyofahamu kuwa nchi yetu bado imekabiliwa na maradhi ya kipindupindu katika maeneo mbali mbali ya Unguja na Pemba. Kuanzia Septemba, 2015 hadi kufikia katikati ya mwezi wa Juni, 2016, jumla ya wagonjwa 4,242 (Unguja 2,608 na Pemba 1,624) walilazwa katika vituo vilivyotengwa vya Unguja na Pemba, na kati ya hao, watu 68 wamefariki dunia (Unguja 49 na Pemba 19). Serikali, imeendelea kuchukua hatua mbali mbali za kukabiliana na maradhi haya zikiwemo utoaji wa elimu ya kujikinga na maambukizi ya maradhi hayo.  Serikali inaendelea kuwasisitiza wananchi kutokufanya biashara za vyakula vya maji maji katika maeneo yasiyoruhusiwa.

22.         Mheshimiwa Spika, kutokana na kupungua kwa kasi ya maradhi ya kipindupindu na kwa kuzingatia mahitaji ya huduma za chakula katika mikahawa, Serikali kupitia Wizara ya Afya imeamua kuzifanyia ukaguzi sehemu za kuuzia vyakula na kuruhusu baadhi ya sehemu hizo baada ya kukidhi vigezo vya afya. Nachukua fursa hii kuzitaka sehemu zilizoruhusiwa kutoa huduma ya chakula kuendelea kuweka usafi na kuzingatia masharti ya afya katika sehemu zao na kwa wale ambao sehemu zao hazijaruhusiwa wahakikishe kuwa sehemu hizo zinakuwa safi ili kukidhi vigezo vya afya.

(iv)                 UTOAJI WA PENSHENI KWA WAZEE:
23.         Mheshimiwa Spika, hivi karibuni, Waziri wa Fedha na Mipango, Mheshimiwa Dkt. Khalid Salum Mohamed kwa niaba ya Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mheshimiwa Dkt. Ali Mohamed Shein alizindua Mpango wa Utoaji wa Pensheni kwa Wazee hapa Zanzibar. Chini ya Mpango huo, Serikali hadi sasa imeorodhesha wazee 21,750 wenye umri wa miaka 70 na kuendelea na kutoa pensheni kwa wazee hao kwa awamu mbili za malipo. Zaidi ya Shilingi Milioni 400 zinatumika kulipia pensheni hizo za wazee kwa kila mwezi. Nachukua fursa hii kukumbusha agizo la Mheshimiwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi kwamba watendaji wanaohusika na pensheni hizo wawe makini na waadilifu katika kuwabaini, kuwafikia na kuwahudumia wazee hao. Vyenginevyo, Serikali haitasita kuwachukulia hatua kali watendaji watakaoharibu mpango huo wa Serikali.

(v)                  KUWAENDELEZA WAJASIRIAMALI:
24.         Mheshimiwa Spika, katika jitahada za kuwaendeleza wajasiriamali, Serikali imekifungua rasmi Kituo cha Kulelea na Kukuza Wajasiriamali kilichopo Mbweni. Kituo hiki kimeweza kutoa mafunzo ya ujasiriamali kwa vijana 815 wa Unguja na Pemba, ambao wengi kati yao wameweza kujiajiri kupitia miradi midogo midogo, na hivyo kujiongezea kipato. Nachukua fursa hii, kuwashajihisha vijana wa kike na kiume kujiunga na kukitumia kituo hiki ili kupata taaluma na ujuzi wa uzalishaji na kuendesha biashara kwa faida na tija.  Ni mategemo ya Serikali kwamba kituo hiki kitakuwa ni msaada mkubwa kwa vijana wetu katika kusaidia kutatua tatizo la ajira.

(vi)                USIMAMIZI WA BEI ZA BIDHAA MUHIMU:
25.         Mheshimiwa Spika, upatikanaji wa bidhaa muhimu za chakula, ikiwemo mchele, sukari na unga wa ngano umekuwa wa kuridhisha hapa nchini. Takwimu zinaonyesha kwamba hadi kufikia Machi 2016, jumla ya tani 72,535 za mchele, tani 16,322 za sukari na tani 29,472 za unga wa ngano zimekidhi mahitaji ya matumizi ya soko la ndani. Mwenendo wa bei za bidhaa hizo uliendelea kuwa ya utulivu (stable) kutokana na Serikali kuendelea kuchukua hatua za kisera za kusimamia bei za bidhaa muhimu kwa kushirikiana na wafanya biashara. Nachukua fursa hii kutoa shukrani kwa wafanya biashara kwa kuzingatia maelekezo ya kisera na hali za wananchi katika kutoa huduma hizo za bidhaa muhimu.

(vii)               TATIZO LA AJIRA KWA WATOTO:
26.         Mheshimiwa Spika, suala la kuwepo kwa ajira kwa watoto hapa Zanzibar bado ni kubwa na Serikali inaendelea na jitihada za kulikomesha tatizo hili ili kuendana na sera na miongozo ya Kimataifa juu ya kuondokana na tatizo hili. Serikali tayari imezisaidia familia masikini 1,500 katika Wilaya zote 11 za Unguja na Pemba ambazo imegundulika kwamba watoto wao wanajishughulisha na kazi mbali mbali za kujipatia kipato. Jumla ya watoto 5,067 kutoka familia hizo ambao walitoroka skuli tayari wamerejeshwa kuendelea na masomo yao badala ya kufanya kazi. Aidha, jumla ya familia 1,065 zimepatiwa sare za skuli kwa watoto wao pamoja na vifaa vya kuanzishia miradi ya kiuchumi vikiwemo mafriji na mifugo.

27.         Mheshimiwa Spika, kutokana na tatizo hilo la ajira kwa watoto kuwa kubwa, nawasihi wazazi kuacha kabisa kuwatumikisha watoto katika kazi mbali mbali na hasa zile hatarishi kwa kisingizio cha kujiongezea kipato cha familia zao. Bado familia zina jukumu kubwa la kuhakikisha watoto wao wanapata haki zao za msingi ikiwemo elimu na malezi bora ili kuwajengea mazingira mazuri ya maisha yao ya baadae.

(viii)        UDHALILISHAJI WA WANAWAKE, WATOTO NA WATU WENYE ULEMAVU:
28.         Mheshimiwa Spika, suala la udhalilishaji na ukatili kwa wanawake, watoto na watu wenye ulemavu bado ni tatizo sugu hapa nchini. Kwa upande mmoja, tatizo hili limekuwa likichangiwa na migogoro ya kifamilia, na kwa upande mwengine linatokana na ucheleweshaji wa taratibu za kushughulikia tuhuma za vitendo vya udhalilishaji na ukatili katika vyombo husika.  Nachukua nafasi hii kutoa wito kwa wananchi kujiepusha na migogoro ya kifamilia, na iwapo ikitokea waitatue kupitia vyombo vinavyohusika. Aidha, navitaka vyombo vyetu vya sheria kuchukua hatua za haraka katika kushughulikia malalamiko na kesi zinazohusu udhalilishaji na ukatilii kwa wanawake, watoto na watu wenye ulemavu.  Malalamiko makubwa ya wananchi ni kwamba vyombo vya Sheria havichukui hatua madhubuti za kushughulikia kesi za udhalilishaji wa kijinsia, na wakati mwingine hazishughulikiwi kabisa hata kama ushahidi utakuwa wazi kiasi gani.  Naviomba vyombo vya Sheria vichukue hatua za haraka kuwashughulikia wale wote watakaohusika na kesi za aina hii.  Kushughulikiwa kesi hizi kwa haraka kutaepusha watu kuchukua sheria mikononi mwao.

(ix)          USHIRIKI WA ZANZIBAR KATIKA JUMUIYA ZA KIKANDA NA KIMATAIFA:
29.         Mheshimiwa Spika, kwa suala la ushiriki wa Zanzibar katika Jumuiya za Kikanda na Kimataifa, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itahakikisha kuwa inawakilishwa vizuri katika mikutano inayoandaliwa na Jumuiya za Kikanda na Kimataifa. Mikutano hiyo itawahusisha Maofisa kutoka katika sekta mbali mbali za Serikali. Madhumuni ya mikutano hii ni kuiwezesha Zanzibar kunufaika na fursa zinazopatikana kwenye Jumuiya hizo pamoja na kujenga mahusiano mema na nchi wanachama.

(xi) USHIRIKIANO NA WAZANZIBARI WANAOISHI NJE YA NCHI:
30.         Mheshimiwa Spika, kuhusu suala la ushirikiano wa Wazanzibari wanaoishi nje ya nchi au Diaspora, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imedhamiria kuwashirikisha Wanadiaspora wa Zanzibar kushiriki maendeleo ya nchi yao. Katika kufanikisha hilo, Serikali itahakikisha kuwa Sera ya Diaspora inamalizika na kuanza kutumika. Sera hii itaweka miongozo sahihi na mazingira rafiki yatakayowawezesha WanaDiaspora wa Zanzibar kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya Zanzibar.  Aidha, katika mwezi Agosti 2016, Serikali itaandaa kongamano la Watanzania wanaoishi nje ya nchi hapa Zanzibar.

(xii) SEKTA YA ARDHI:
31.         Mheshimiwa Spika, katika sekta hii, Serikali itafanikisha kazi za kutayarisha Hati Miliki 1,350 na Vitambulisho vya Umiliki Ardhi za Eka Tatu 60, kutayarisha Mikataba ya ukodishaji ardhi 130, kuingiza taarifa za ardhi katika mfumo wa komputa sawa na hati za mikataba itakayotayarishwa, kukagua maeneo yote yatakayohitajika kutayarishiwa Mikataba ya Uekezaji na maeneo ya kilimo (Eka Tatu) pamoja na kufanya utambuzi wa maeneo 6,000 kwa Shehia za Unguja na Pemba mijini na vijijini.

32.         Mheshimiwa Spika, vile vile Serikali itaendelea kuhimiza matumizi bora na endelevu ya ardhi na kuendelea kupanga miji midogo ya Zanzibar kwa kupanga matumizi ya ardhi ya miji miwili midogo mji wa Wete huko (Pemba) na mji wa  Makunduchi hapa (Unguja) sambamba na kufanya mapitio ya mpango wa maendeleo ya utalii, katika eneo la Pwani ya Mashariki kutoka Chwaka mpaka Nungwi.

Migogoro ya ardhi:
33.         Mheshimiwa Spika,  bado migogoro ya ardhi imekuwa changamoto kubwa kwa Serikali yetu.  Hii ni kwa sababu ya wananchi wetu hawataki kuheshimu Sheria ya Ardhi ndiyo maana kila siku migogoro ya ardhi inaibuka.  Kuimaliza migogoro hii, naiomba Mahakama ya Ardhi kuzishughulikia kesi za migogoro ya ardhi kwa haraka iwezekanavyo.


(xiii) SEKTA ZA HABARI NA MICHEZO:
34.         Mheshimiwa Spika, katika sekta ya habari, Serikali imo mbioni kukamilisha ujenzi wa Chuo cha Uandishi wa Habari kilichopo Kilimani ili kiweze kupokea idadi kubwa ya wanafunzi katika fani ya habari, ambapo Chuo kitaongeza madarasa matano (5) na kutoa fursa kwa wanafunzi wengi kujiunga katika chuo hicho. Ujenzi utakapomalizika, Chuo kitakuwa na uwezo wa kuchukua wanafunzi 304 kwa mwaka, ikilinganishwa na idadi ya sasa ya wanafunzi 204 kwa mwaka. Aidha, kutaanzishwa kozi nyengine mpya za masomo zikiwemo Uhusiano wa Kimataifa na Diplomasia (International Relations & Diplomacy), Language & Interpretation, Language Art of Public Speaking, Graphic Design na Chinese Language & Chinese Culture. Hivyo Chuo kitaweza kukuza na kuongeza upatikanaji wa habari kwa ufasaha na kukuza ajira kwa wanahabari.

35.         Mheshimiwa Spika, kwa upande wa sekta ya michezo, nchi yetu imeshuhudia migogoro mbali mbali hasa katika mpira wa miguu.  Migogoro hii inaathiri sana ukuaji wa michezo kwa namna moja ama nyengine nchini. Serikali kupitia Wizara ya Habari, Utalii, Utamaduni na Michezo kwa kushirikiana na wadau mbali mbali wa michezo inaendelea kuchukua hatua za utatuzi wa migogoro hiyo ili kuendeleza sekta ya michezo na kuleta tija kwa wananchi na Taifa kwa ujumla.

36.         Mheshimiwa Spika, Serikali imekusudia kujenga na kuviendeleza viwanja mbali mbali vya michezo ili kuwawezesha vijana wetu kupata fursa ya kushiriki na kukuza vipaji vyao vya michezo. Katika kulitekeleza hili, jumla ya viwanja tisa vikiwemo Gombani, Mao-Tse-Tung, Tibirinzi, Nungwi na Matumbaku tayari vimeshapimwa na vinasubiri kuanza kwa ujenzi.  Viwanja hivi vikikamilika kujengwa vitasaidia kuimarisha michezo nchini.

(xiv) SEKTA YA KILIMO:
37.         Mheshimiwa Spika, kwa upande wa sekta za kilimo, mifugo na uvuvi, Serikali itaweka mkazo zaidi katika kuimarisha uzalishaji na tija katika kilimo kwa kushajiisha matumizi ya teknolojia za umwagiliaji maji, kushajiisha ufugaji wa kibiashara wa kuku na ng’ombe wa maziwa, kuimarisha uwekezaji katika uvuvi wa bahari kuu na katika viwanda vya kusarifu matunda, samaki na mwani pamoja na kuwaunganisha wakulima, wafugaji na wavuvi na masoko ya ndani na nje ya nchi.

38.         Mheshimiwa Spika, suala la usimamizi wa rasilimali zetu ni muhimu sana. Serikali itaendelea kupiga vita uvuvi haramu kwa kuimarisha mfumo wa doria pamoja na kuandaa utaratibu wa kuwapatia wavuvi wadogo wadogo zana bora za uvuvi. Aidha, Serikali itaendelea kudhibiti wimbi la uvamizi wa maeneo yote ya kilimo, misitu na mifugo ambayo katika siku za hivi karibuni uvamizi huu umeongezeka sana kwa watu kukata miti ovyo na kujenga katika maeneo yenye rutuba hasa katika mabonde ya mpunga na katika maeneo ya hifadhi ya misitu na kuchimba mchanga katika mashamba yanayofaa kwa kilimo. Nachukua fursa hii kuwataka wale wote wanaojishughulisha na vitendo hivyo vya kuharibu rasilimali zetu, waache mara moja tabia hiyo, vyenginevyo Serikali itawachukulia hatua za kisheria mara moja. Aidha, Serikali itaendelea na utoaji wa miche ya mikarafuu bila ya malipo na kuhakikisha kuwa pembejeo muhimu za kilimo, ikiwemo mbolea, mbegu na madawa ya kuulia magugu yanapatikana kwa wakati na kwa wingi unaohitajika ili kuweza kuleta mabadiliko ya tija na uzalishaji kwa kilimo cha mpunga.

(xv) SEKTA YA NYUMBA NA MAKAAZI:
39.         Mheshimiwa Spika, kwa upande wa Sekta ya Nyumba na Makaazi, Serikali kupitia Shirika la Nyumba la Wizara ya Ujenzi, Mawasiliano na Usafirishaji itaendelea kuimarisha huduma bora za makaazi kwa wananchi wote kwa kuendeleza miradi ya kuwapatia wananchi makaazi bora, salama na ya kisasa na yenye gharama nafuu. Matarajio makubwa ya Serikali ni kutatua tatizo la makaazi kwa wananchi hapa Zanzibar.

(xvi) UIMARISHAJI WA SEKTA YA ELIMU:
40.         Mheshimiwa Spika, katika kuimarisha sekta ya elimu nchini Serikali imo katika hatua za kutayarisha mpango mkuu wa miaka mitano 2016 hadi 2020 ambao utakuwa dira ya elimu kwa kipindi hicho katika ngazi za maandalizi, msingi, sekondari na vyuo.  Kupitia mpango huo changamoto zote za msingi zinazoikabili sekta ya elimu kama vile, upungufu wa madawati, madarasa, maabara na maktaba pamoja na miundombinu na vifaa vyengine zinapatiwa ufumbuzi.

41.         Mheshimiwa Spika, suala la mchango wa madawati ya wanafunzi limezungumzwa sana katika vikao hivi vya Baraza lako Tukufu. Serikali ilikuwa ikitoa fedha kupitia makusanyo ya Kodi ya Bandari kwa ajili ya kununulia madawati ili kupunguza tatizo la vikalio katika skuli zetu. Mchango huu ulianza kutolewa katika mwaka wa fedha wa 2012/2013. Jumla ya TZS 3,452,662,465.00 zilipatikana kupitia kodi hiyo ya bandari katika kipindi cha miaka minne, na hadi kufikia mwaka 2015/2016, jumla ya Madawati 4,285, Viti 3,706 na Meza 3,704 yalinunuliwa kwa kutumia fedha hizi na kusambazwa katika skuli za Unguja na Pemba na yanatumika kwa ajili ya wanafunzi na walimu wetu.  Niwaombe Waheshimiwa Wawakilishi kutumia alau sehemu ndogo ya mifuko yao ya Majimbo kusaidia kupunguza matatizo hayo, hasa upungufu wa madawati kwenye skuli zilizoko ndani ya Majimbo yao.

MAMBO MUHIMU YALIOJITOKEZA BARAZANI:
42.         Mheshimiwa Spika, katika mkutano huu wa pili, Baraza lako Tukufu lilikamilisha mambo makuu tisa (9) yafuatayo:-
(a)          Kujibu maswali yaliyoulizwa na Waheshimiwa Wajumbe.
(b)         Limepokea na kujadili Hotuba ya Mpango wa Maendeleo wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar wa 2016/2017.
(c)          Limepokea na kujadili Hotuba ya Bajeti ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ya mwaka wa fedha 2016/2017.
(d)         Limepokea na kujadili Ripoti ya Mkaguzi na Mdhibiti wa Hesabu za Serikali na Mashirika.
(e)          Limepokea na kujadili Mswada wa Sheria ya Fedha (Finance Bill) na Uchaguzi wa Wabunge watano kuliwakilisha Baraza letu Tukufu.
(f)           Limefanya uchaguzi wa Mwenyekiti wa Baraza na Uchaguzi wa Wajumbe wa Tume ya Bajeti ya Baraza la Wawakilishi.
(g)         Limepokea, kujadili na kupitisha Hotuba za Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara za SMZ kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
(h)         Limepokea na kujadili Mswada wa Sheria ya Matumizi.
(i)           Limepokea na kujadili Mswada wa Dharura wa Sheria ya kuanzisha Hospitali ya Mnazi Mmoja.

43.         Mheshimiwa Spika, katika Mkutano huu jumla ya maswali ya msingi 85 na maswali ya nyongeza 246 yaliulizwa na Waheshimiwa Wajumbe na kujibiwa na Waheshimiwa Mawaziri wa Sekta husika. Nawapongeza Waheshimiwa Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi waliouliza maswali ya msingi na ya nyongeza ambayo yalikuwa na lengo la kudadisi utekelezaji na ufanisi wa shughuli za Serikali. Aidha, nawapongeza na kuwashukuru Waheshimiwa Mawaziri kwa kutoa majibu sahihi ambayo yamewejengea uelewa Waheshimiwa Wawakilishi pamoja na wananchi kwa jumla.  Kwa dhati kabisa, napenda kuwapongeza Mawaziri na Naibu Mawaziri wapya ambao walijibu maswali katika Baraza hili kwa mara ya kwanza na kujibu vizuri sana kwa umakini na kwa kujiamini.

44.         Mheshimiwa Spika, kuhusiana na Mpango wa Maendeleo wa Zanzibar, Serikali imepanga kutumia Mkakati mpya wa maendeleo ambao unakusudia kuendeleza mageuzi ya kiuchumi na kijamii kwa kuimarisha uchumi endelevu na kuimarisha ubora wa huduma za kijamii ikiwemo elimu, afya, mazingira endelevu na misingi ya utawala bora.

45.         Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2016/2017 maeneo yatakayopewa kipaumbele katika utekelezaji wa Mpango wa Maendeleo ya Zanzibar yameainishwa na kufafanuliwa vyema katika hotuba ya Serikali iliyotolewa na Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango mwanzoni mwa kikao cha kwanza cha Mkutano wa Pili wa Baraza hili la Tisa. Hata hivyo, kutokana na umuhimu wake mkubwa katika kuendeleza uchumi wetu na kuimarisha huduma za jamii na utawala bora kwa jumla, naomba nichukuwe fursa hii kukumbusha tena maeneo hayo ya kipaumbele tuliyojiwekea kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
i)             Kuendeleza miundombinu ya msingi ya barabara, bandari, viwanja vya ndege na nishati.
ii)                    Kuendeleza Mpango wa Matokeo kwa Ustawi (R4P).
iii)            Kuimarisha huduma za kijamii hasa elimu, afya na maji.
iv)                  Kuimarisha kilimo.
v)            Kuimarisha maendeleo ya Sekta ya Viwanda Vidogo Vidogo na vya kati.
vi)                   Kuendeleza Program za Kukuza Ajira kwa Vijana.
vii)           Kuongeza juhudi ya kutunza mazingira dhidi ya mabadiliko ya tabianchi kitaifa na kijamii kwa jumla.
viii)                Kufanya tafiti katika sekta mbali mbali.
ix)                  Kuimarisha misingi ya utawala bora na sheria.

46.         Mheshimiwa Spika, ni wajibu wa Taasisi zote za Serikali kuhakikisha kuwa mipango na programu zao zinaendana na utekelezaji wa malengo haya makuu ya Serikali kwa mwaka 2016/2017. Aidha, mipango ya muda wa kati hadi kufikia mwaka 2020 haina budi kuendana na malengo ya Mkakati mpya wa Maendeleo wa Zanzibar wa 2016 – 2020. Kwa mnasaba huu, Taasisi zote za Serikali ni vyema zikaandaa utaratibu wa haraka wa kufanya mapitio ya mipango mikakati yao (Strategic Plans) ili kuoana na mpango mkuu wa Serikali unaochukua nafasi ya MKUZA II ambao unamalizika muda wake mwishoni mwa mwezi wa Juni, 2016.

47.         Mheshimiwa Spika, mkutano huu pia umepokea na kujadili na kupitisha Hotuba ya Bajeti ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ya mwaka wa fedha 2016/2017. Jumla ya fedha TShs: Bilioni 841,477,500 zimepitishwa. Kati ya hizo, TShs: Bilioni 445.6 ni kwa ajili ya kazi za kawaida na TShs: Bilioni 395.9 kwa matumizi ya kazi za maendeleo. Nawashukuru na kuwapongeza Waheshimiwa Wawakilishi wote kwa kuipitisha Bajeti hiyo kwa kauli moja.

48.         Mheshimiwa Spika, ripoti ya Mkaguzi na Mdhibiti wa Hesabu za Serikali na Mashirika imewasilishwa Barazani na itajadiliwa na Waheshimiwa Wajumbe wa Baraza lako Tukufu katika vikao vijavyo vya Baraza.

49.         Mheshimiwa Spika, mkutano huu pia ulijadili na kupitisha Hotuba za Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara zote 13 za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa mwaka wa fedha 2016/2017. Ni matumaini yangu kwamba Waheshimiwa Mawaziri watasimamia kwa umakini utekelezaji wa malengo yaliyowekwa katika programu na programu ndogo za Wizara hizo.  Aidha, Waheshimiwa Mawaziri wajitahidi kuzitekeleza ahadi walizozitoa Barazani hapa.

50.         Mheshimiwa Spika, katika mkutano huu Wajumbe pia walipata fursa ya kuwachagua Wajumbe watano wa Baraza hili watakaotuwakilisha katika Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kipindi cha miaka mitano ijayo. Wajumbe hao waliochaguliwa ni Mheshimiwa Machano Othman Said, Mheshimiwa Wanu Hafidh Ameir, Mheshimiwa Amina Iddi Mabrouk, Mheshimiwa Jaku Hashim Ayoub na Mheshimiwa Hussein Ibrahim Makungu.  Kwa mara nyengine tena nawapongeza kwa uchaguzi huo na pia nawaomba watuwakilishe vyema katika Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

51.          Mheshimiwa Spika, katika mkutano huu wa Baraza lako Tukufu, Waheshimiwa Wajumbe walipata fursa ya kujadili mambo mbali mbali muhimu kwa Taifa letu. Miongoni mwa mambo hayo ni pamoja na ukusanyaji wa mapato kupitia Halmashauri na Manispaa; kuimarisha ulinzi katika bandari bubu (zisizo rasmi); uimarishaji wa Shirika la Utangazaji Zanzibar (ZBC); utatuzi wa migogoro katika michezo; uvuvi wa bahari kuu; pembejeo za kilimo kwa wakulima; vifaa vya kukabiliana na maafa; uimarishaji wa makaazi ya Viongozi wa Kitaifa na suala la wafanyakazi hewa kwa kutaja machache.

52.         Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Halmashauri za Wilaya na Mabaraza ya Miji itahakikisha ukusanyaji wa mapato unaongezeka pamoja na kuziba mianya ya uvujaji wa mapato hayo. Hali hii itaiwezesha Serikali kutekeleza mipango ya maendeleo iliyowekwa katika Halmashauri hizo na Taifa kwa ujumla.

53.         Mheshimiwa Spika, kuhusiana na suala la uimarishaji wa ulinzi katika bandari zisizo rasmi (bandari bubu), Serikali inaendelea na mikakati ya kuzitambua na kuziwekea utaratibu maalum bandari hizo ili kutoa huduma katika hali ya usalama na kusaidia kuchangia upatikanaji wa mapato ya Serikali. Aidha, Serikali kwa kushirikiana na Kikosi Maalum cha Kuzuia Magendo imekuwa ikifanya doria za mara kwa mara katika maeneo yote ya mwambao wa visiwa vyetu ikiwemo maeneo ya bandari bubu kwa lengo la kuhakikisha maeneo hayo hayatumiki kuendeshea biashara haramu na yanabaki salama.

54.         Mheshimiwa Spika, katika hatua za kukabiliana na maafa nchini, Serikali imeendelea kutekeleza mipango na mikakati mbali mbali inayowezesha kupunguza athari za maafa iwapo yatatokezea. Miongoni mwa hatua muhimu zilizochukuliwa na Serikali ni pamoja na kuanzisha Kamisheni ya Kukabiliana na Maafa badala ya Idara ili kuwa na uwezo mkubwa zaidi wa kuratibu vizuri zaidi masuala ya kukabiliana na maafa hapa nchini.  Aidha, Serikali kupitia Kamisheni hii imeendelea kutoa elimu ya kukabiliana na maafa kwa jamii na kuandaa miongozo ya kujiandaa na kukabiliana na maafa katika ngazi mbali mbali. Serikali itaendelea kuzijengea uwezo wa kitaaluma na kivifaa Taasisi zote zinazohusika na masuala ya kukabiliana na maafa nchini.

55.         Mheshimiwa Spika, katika kuimarisha makaazi ya Viongozi Wakuu pamoja na nyumba za Serikali zilizopo katika maeneo mbali mbali kwa Unguja na Pemba, Serikali inaendelea kuzifanyia matengenezo na kuziwekea vifaa muhimu ili ziweze kutumika kama zilivyokusudiwa.

56.         Mheshimiwa Spika, kuhusiana na suala la wafanyakazi hewa, Serikali inaendelea na uhakiki wa watumishi wote wa umma na itahakikisha wale wote wasiositahiki kuwepo katika orodha ya watumishi wa umma wanatolewa. Aidha, Serikali itawachukulia hatua kali za kinidhamu na kisheria wale wote watakaobainika kwa namna moja au nyengine kushiriki katika uhaulifu huo.

HITIMISHO:
57.         Mheshimiwa Spika, kwa mara nyengine tena, naomba kuchukua nafasi hii kukushukuru na kukupongeza wewe binafsi, Mheshimiwa Naibu Spika na Wenyeviti wa Baraza kwa kuuendesha Mkutano huu wa Pili wa Baraza hili la Tisa kwa umahiri na umakini mkubwa.  Vile vile, narudia kuwapongeza na kuwashukuru Waheshimiwa Wajumbe wa Baraza hili Tukufu kwa michango yao katika kupitisha bajeti ya Serikali na za Wizara zote katika mazingira ya ushirikiano yenye lengo la kuleta tija na kuimarisha utendaji na uwajibikaji Serikalini.

58.         Mheshimiwa Spika, nawashukuru sana na kuwapongeza Waheshimiwa Mawaziri kwa kutoa ufafanuzi wa hoja zilizotolewa na kujibu maswali ya Waheshimiwa Wajumbe kwa ufasaha.  Pia nawashukuru waandishi wa habari na wakalimani wa lugha ya alama kwa kazi yao nzuri ya kuwapatia taarifa wananchi kuhusu majadiliano ya Baraza katika mkutano huu. Shukrani maalum nazitoa kwa Shirika la Utangazaji Zanzibar (ZBC) kwa kutangaza na kuonesha moja kwa moja (live) shughuli zote za mkutano huu bila kusita.

59.         Mheshimiwa Spika, mwisho napenda kuvipongeza vyombo vyote vya ulinzi na usalama pamoja na Idara Maalum za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa mchango wao mkubwa katika kudumisha usalama na utulivu uliopo hapa nchini.
60.         Mheshimiwa Spika, zipo kauli zinazosambazwa kupitia mitandao ya kijamii kuwa Serikali itachinja ng’ombe waliowakamata na kuuza nyama kwa bei rahisi ya Shs. 3,000 kwa kilo na kutolewa tahadhari kuwa watu wasinunue nyama hiyo eti siyo halali na ni nyama ya kifo.  Napenda kuweka bayana kuwa kauli hizo hazina ukweli wowote.  Hakuna ng’ombe yoyote atakayechinjwa na Serikali na kuuzwa Maisara kwa bei rahisi.  Huu ni uongo na uzushi mtupu.  Vile vile kuna kauli nyeingine ya kuwazuia watoto wasiende kufurahi Mnazi Mmoja wakati wa Sikukuu eti kutatokea fujo na vurugu.  Huu ni uongo mkubwa na uzushi usio na kifani.  Serikali inawahakikishia wananchi kuwa hali ya nchi yetu iko salama na utulivu na itabaki hivyo siku zote.  Kauli hizo ni propaganda za wapinzani kutaka kuwahamanisha wananchi wapenda amani.  Wananchi wanahakikishiwa kuwa viwanja vyote vya sikukuu vitakuwa salama.

61.         Mheshimiwa Spika, tukiwa tumo katika kumi la mwisho la Mfungo wa Mwezi Mtukufu wa Ramadhani, tunamuomba Mwenyezi Mungu atukubalie swaumu zetu na atujaaliye kumaliza faradhi hii  kwa salama. Kwa vile hatutokaa tena katika kikao kama hiki kabla ya kumalizika mwezi Mtukufu wa Ramadhan, nachukua fursa hii kuwatakia Waheshimiwa Wawakilishi pamoja na wananchi wote sikukuu njema ya Eid-el-Fitri inayotarajiwa hivi karibuni INSHAALLAH.  Kuluam wa Antum Bukheir.

62.         Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo hayo, sasa naomba kutoa hoja ya kuliakhirisha Baraza lako Tukufu hadi siku ya Jumatano, tarehe 21 Septemba, 2016 saa 3.00 barabara za asubuhi panapo majaaliwa.

Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja.


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.