Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa, Serikali za Mitaa na Idara maalum za SMZ Haji Omar Kheir akizungumza na waandishi wa habari juu ya kuanzishwa Mamlaka za Serikali za Mitaa Zanzibar katika Ukumbi wa Wizara ya Habari, Utalii, Utamaduni na Michezo Kikwajuni.
Baadhi ya Waandishi wa habari wakimsikiliza Waziri Haji Omar Kheir alipokuwa akitangaza kuanzishwa Mamlaka za Serikali za Mitaa Zanzibar.
Na.Khadija Khamis – Maelezo Zanzibar.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa, Serikali za Mitaa na Idara Maalum za SMZ Haji Omar Kheir ametangaza rasmi kuanzishwa Mamlaka za Serikali za Mitaa na kuwateua Madiwani 56 kwa mujibu wa sheria Namba 7 ya mwaka 2014.
Akitangaza Mamlaka hizo katika Ukumbi wa Wizara ya Habari, Utalii, Utamaduni na Michezo, Waziri Haji Omar Kheir alisema lengo la kuanzishwa Mamlaka hizo ni kuimarisha misingi ya Utawala bora Zanzibar.
Alisema katika Mkoa wa Mjini Magharibi kutakuwa na Mabaraza matatu ya Manispaa ambayo ni Baraza la Manispaa la Mjini, Baraza la Manispaa la Magharibi ‘A’ na Baraza la Manispaa la Magharibi ‘B’.
Katika Mkoa Kaskazini Unguja kutakuwa na Halmashauri ya Wilaya ya Kaskazini ‘A’ na Halmashauri ya Wilaya ya Kaskazini ‘B’ Wakati Mkoa wa Kusini Unguja kutakuwa na Halmashauri ya Wilaya ya Kati na Halmashauri ya Wilaya ya Kusini.
Alisema Pemba kutakuwa na Baraza la Mji Mkoani na Baraza la Mji Chake chake kwa Mkoa wa Kusini na Mkoa wa Kaskazini kutakuwa na Baraza la Mji Wete na Halmashauri ya Wilaya ya Micheweni.
Aidhaa Waziri Kheir amefuta baadhi ya Mamlaka za Serikali za Mitaa zilizokuwepo awali ambazo ni Halmashauri ya Wilaya Magharibi, Halmashauri ya Wilaya ya Wete, Halmashauri ya Wilaya ya Mkoani na Halmashasuri ya Chake chake.
Amesema hatua ya kuunda Mabaraza zaidi ya moja ndani ya Mkoa wa Mjini Magharibi ni moja ya maandalizi ya Serikali ya kuanzisha Jiji la Zanzibar katika siku za baadae.
Aliwataka wananchi kuendelea kupata huduma katika Mamlaka za Serikali za Mitaa kwa kushiriki kikamilifu katika vyombo vya maamuzi kwa lengo la kukuza ustawi wa Zanzibar.
Wakati huo huo Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa, Serikali za Mitaa na Idara maalum za SMZ ametangaza majina ya Madiwani 56 aliowateua kuungana na Madiwani waliochaguliwa na wananchi kuzitumikia Mamlaka hizo.
Kwa mujibu wa uteuzi huo madiwani 36 ni wanawake ambao ni sawa na asilimia 64 na madiwani 20 ni wanaume.
Ameyaagiza Mabaraza yote kuwaapisha madiwani kuyatumika mabaraza yao na kuandaa taratibu za uchaguzi na kufanya uchaguzi wa viongozi kwa Mabaraza ya Miji na Halmsahauri kabla ya tarehe 20 Julai mwaka huu.
No comments:
Post a Comment