Habari za Punde

Kilio cha Jumba la treni kimesikilizwa


Makala hii ilitoka mwaka 2013. Na Nimefarijika baada ya mchango wangu mdogo kusikilizwa na ZSSF kuamua kulifanyia ukarabati jengo la Treni. Tujikumbushe
Maarufu nnajulikana kama ni Jumba la Treni hebu nitazame hali yangu hivi kweli kwa hadhi niliyonayo nnastahiki kuwa hivi?.

Ingawa jina lenyewe silipendi lakini nimeitwa Jumba la treni eti kwa sababu ninafanana na treni! Mmh. 

Nipo katika eneo la hifadhi ya mji mkongwe jirani na iliyokuwa marikiti kuu.  Nipo katika sehemu kuu ya biashara ambapo nimesheheni maduka pande zangu zote mbili za uchejua na urejua.

Ninamilikiwa na Serikali  yangu kwani niliwekwa wakfu muda mrefu na wenye maduka wote ni hunilipia kodi ambayo huingia moja kwa moja katika Idara ya nyumba na majengo ambao ndie mlezi wangu na msimamizi wangu na ndio anenisimamia katika kuhakikisha niko katika hali nzuri muda wote. Alhamdulillah ninamshukuru kwa hili.

Nipo katika sehemu nzuri ambapo takriban watalii wengi, kama si wote, wanaofika Unguja lazima watembezwe katika eneo la marikiti sehemu yenye historia muhimu kwa visiwa vyetu na hivyo lazima waoneshwe uwepo wangu na huku wakinitania eti ni jumba la treni!Sehemu nilipo ni sehemu ambayo inaakisi mji wetu na haiba ya kisiwa chetu na uzuri au uzoefu wa kuhifadhi historia yetu.

Lakini hali yangu niliyo nayo na jinsi nilivyozeeka (nina umri wa zaidi ya miaka moja sasa) inanihuzunisha na kunisikitisha.



Ya laiti kama zile kodi kiduchu zinazotolewa na wenye kuendesha biashara za maduka ningelirudishiwa angalau kwa kunitia japo rangi na kunifanyia matengenezo japo ya kunirembesha na mie kidogo nionekane (cosmetic). Nikiona wenzangu wanashughulikiwa na wengine kuenziwa huingiwa na ghera kwani nimemkosea nini mlezi wangu jamani mpaka nikose sudfa ya kukumbukwa?

Siku moja nilitamani nijiangushulie mbali halafu niwaone kama watanikumbuka fadhila zangu na jitihada zungu za kuwaingizia kipato miaka nenda miaka rudi, licha ya umri wangu na bado nnalifikiria hilo maana nimeshajichokea.

Ninachotaka si kupendeza tu, bali ni kuwaongezea hicho hicho kipato ili kiendane na hadhi yangu na haiba yangu na dunia ya leo.

Ya laiti kama angelitokea mhusika mwenye ujasiri wa kunifanyia maamuzi magumu ya kunidondosha na kunijenga tena katika mfumo ule ule wa majengo ya  uhifadhi wa mji mkongwe na kuniwezesha kuwa na sehemu nyingi zenye maduka ya biashara (chini na juu) na pia kuwa katika hali nzuri basi ningelimshukuru sana.


Maana sijui kama waliopo wananijali jinsi ninavyodhikika na kuwa na unyonge na upweke mpaka najifikiria labda nifikiriwe na mhisani nitakaemsubiri kujitolea kama serikali yenyewe haijaniwekea mkakati wowote wa kunifikiria.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.