Habari za Punde

PBZ yalipa kodi sh.2.6bn, yasiadia mayatima


Na Mwandishi wetu
BENKI ya Watu wa Zanzibar (PBZ) imesema mtaji wake umeimarika kutoka shilingi milioni 16 wakati ikianzishwa Juni 30, 1966 hadi shilingi bilioni 40 Juni 30, 2016 huku faida  katika kipindi cha Januari hadi Juni mwaka huu ikifikia shilingi bilioni 8.

Mkurugenzi Mtendaji wa benki hiyo, Juma Ameir, alisema hayo katika hafla ya miaka 50 tokea kuanzishwa benki hiyo iliyofanyika hoteli ya Zanzibar Beach Resort Mazizini.

Aidha alisema katika kipindi cha Januari-Judi mwaka huu, benki imelipa kodi serikalini inayofikia shilingi bilioni 2.6.

Alisema katika kipindi cha miaka 50 benki imeimarisha zaidi huduma zake baada ya kuwa benki kamili ya biashara ikiwemo kuongeza vituo vya kutolea huduma na mashine za ATM, ambapo hivi karibuni itaweka kituo cha huduma katika kijiji cha Kiwengwa mkoa wa kaskazini Unguja.

Pia benki itaongeza mashine za ATM katika maeneo ya Kibweni, Kivunge, Mperani na Baraza la Wawakilishi pamoja na kuanzisha mawakala  wa benki (agency banking) na mfumo wa kukusanya mapato ya serikali.

Hata hivyo, licha ya mafanikio hayo, alisema benki bado inakabiliwa na changamoto kadhaa ikiwemo baadhi ya huduma kuendelea kutolewa kwa mfumo wa kizamani (manual).


Aidha alisema pia benki inakabiliwa na changamoto za kimahakama, ambapo baadhi ya wateja wanaodaiwa na  benki  wanaposhindwa kulipa deni benki huamua kuchukua mali zao kwa ajili ya kufidia.

Hata hivyo, alisema wateja hao huamua kukimbilia mahakamnani hali inayosababisha kesi kukaa muda mrefu huku benki ikishindwa kurejesha deni lake.

Aliiomba serikali kuwawezesha wafanyabiashara wadogo, akisema kama serikali haitakubali kuwapunguzia mzigo wa kodi hawataendelea na watakuwa hawakubaliki kukopeshwa katika taasisi za fedha.

“Mfumo wa sasa wa kodi haubagui mfanyabiashara mdogo, wa kati wala mkubwa, wote walipa kiwango sawa, sasa hii haiwezi kuwasaidia wafanyabiashara wadogo, lazima serikali iwaangalie hawa vyenginevyo hawawezi kukua na ni vigumu kukopesheka.

Mapema Naibu Katibu Mkuu wizara fedha na mipango, Ali Khamis Juma, aliwataka wafanyakazi wa benki hiyo kuendelea kuchapa kazi ili benki ipate mafanikio zaidi.

Wakati huo huo, benki hiyo benki hiyo imetoa msaada wa vyakula, magodoro na mashuka kwa taasisi mbali mbali za serikali na binafsi.
Taasisi zilizofaidika ni Chuo cha Mafunzo ambacho kilipatiwa magodoro 100, hospitali ya wagonjwa wa afya ya akili ambayo ilipatiwa mashuka 200 na tende.

Kijiji cha kulelea watoto (SOS) kilipatiwa tani moja ya unga wa ngano, sukari nusu tani, mchele nusu tani na mafuta ya kupikia lita 250.

Mayatima wanaolelewa katika nyumba ya mayatima Mazizini walipatiwa kilo 200 za unga wa ngano, sukari kilo 10, mchele kilo 100 na mafuta lita 50.

Taasisi nyengine zilizofaidika ni pamoja na Isla Centre iliyopo Mpendae ambayo inajishughulisha na kutunza watoto, Omar Bin Khatab iliyopo Fumba, kituo cha mayatima cha Magogoni Chake Chake.


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.