Habari za Punde

Kumbukumbu ya HIjja na athari zake - 4

Tulipofika Mina nikaendelea na siku yangu ya tatu ya mafunzo, siku hii huitwa siku ya kuchinja – Yawmun Nahr. Ndio siku yenye mafundisho mengi kuliko siku nyengine za Hijja. Tuendelee

Nikaianza safari yangu kuelekea Jamaraat (kupiga mawe) nikitokea Mina kwa miguu ni mwendo wa nusu saa tu, lakini kutokana na msongamano wa watu jinsi walivyokuwa wengi ilinichukua saa 1.30 kufika Jamaraat.

Siku kila aliyekuja kuhiji hutakiwa kupiga mawe Jamaratul ‘Aqabah au kubra. Mnara mkubwa katika minara mitatu iliyopo eneo la Jamaraat.

Nilifika salama usalimini eneo la kupiga mawe (hii ni sehemu ya hatari katika sehemu zote za hijja kwa kuwepo msongamano mkubwa kila mwaka ambao mara nyingi hupelekea vifo vya mahujjaaj). Nikakoma kusema Talbiyah kwani kisheria nikifika sehemu ya Jamaratul ‘Aqabah ndiyo sehemu ya mwisho ya kusema Talbiyah ambayo niliikuwa nikiisoma tokea nilipovaa Ihraam siku ya tarehe 8 dhulhijjah.

Nikatafuta sehemu muwafaka ya kurusha mawe kutokana na wingi wa watu na nilipoipata nikaanza kurusha kijiwe cha kwanza huku nikisema: Bismillaah Allaahu Akbar. Nikafuatanisha na chengine kwa kusema Allaahu Akbar pekee bila ya bismillaah hadi nikamaliza vijiwe saba. Jamaratul kubra ukimaliza kupiga mawe hutakiwi kusimama baada yake na kuomba du’aa kama ilivyo kwa minara mengine na pia ni Jamarah pekee ambalo limeruhusiwa kupigwa kabla ya Zawaal siku ya iyd (kuchinja).

Nilipomaliza nikaendelea na safari yangu kwa miguu kutoka Jamaraat hadi ‘Aziziyah kitongoji kimojawapo kaskazini mwa Makkah tulipofikia. Kutokana na msongamano safari hii pia ilinichukua takriban saa nzima.

Alhamdulillah nikatumiwa ujumbe mfupi kwenye simu yangu (kutoka kwa kiongozi wa kundi letu) kwamba kichinjwa changu tayari kimeshachinjwa kwani hii pia ni mojawapo ya Ibada inayotakiwa kufanyika katika siku hii au ziku za Tashriyq (yaani tarehe 11,12 na 13 Dhulhijjah). Nikaulizia nini maana ya Tashriyq? Nikajuulishwa na wenye weledi na Hijja ni ile nyama inayochinjwa siku ya Eid huanikwa juani hadi kukauka na kuhifadhiwa ndiyo maana yake. (kumbuka miaka hiyo hawakuwa na majokofu ya kuhifadhi nyama kama tulivyo siku hizi)

Baada ya kupumzika kidogo, nilikoga na kuvua Ihraam zangu kwani hapa tayari nimekuwa nimetahallal (kutoka ihram) kidogo kwani nimeruhusiwa kufanya mambo yote isipokuwa kustarehe na mke nikatakiwa kuendelea na mafunzo yangu kwa siku kwa kuelekea Al Ka’abah kwa ajili ye kutekeleza nguzo mbili kuu za Hijja, kufanya tawaaf kufanya Sa’iy.

Safari yangu kutoka Aziziyah hadi Al Ka’abah ilinichukua saa 1.15 naam kwa miguu. Nilipofika Al Ka’abah ambapo umati uliokuwepo hapo siku hii ukiteleza nguzo za Hijja na umati mwengine ambao niliuacha Mina nikajisemea moyoni Alhamdulillaah, haya ndio matunda ya kazi aliyoifanya Mtume Muhammad Swalla ‘Allaahu ‘alayhi Wasallam. Ninayoshuhudia kwa macho yangu ni ushuhuda kwamba Mtume Muhammad Swalla ‘Allaahu ‘alayhi Wasallam amefikisha ujumbe na kutimiza amana aliyopewa na Allaah ‘Azz wa Jall. Nina imani Allaah ‘Azza wa Jall anashuhudia kwamba Mtume Swalla Allaahu ‘alayhi wasallam amefikisha ujumbe kama alivyoagizwa.

Nikaingia msikitini kwa kuomba du’aa ya kuingia msikitini na kuelekea sehemu ya kuanzia Tawaaf.

Tawaaf ni ibada unayotakiwa uizunguke Al Ka’abah mara saba ukianzia sehemu lilipo jiwe jeusi (Hajarul aswad). Unatakiwa kuzunguka ilhali Al Ka’abah ipo upande wako kushoto ( anti clockwise). Ni mojawapo katika nguzo za Hijja na lazima ifanyike veynginevyo Hijja haitosihi.

Tawaaf ya nguzo huitwa Tawaaful Ifaadhah au Tawaafu Ziyaarah. Lazima uwe katika hali ya tohara kabla ya kufanya tawaaf (uwe na udhu).

Sehemu ya kuanzia imewekewa ishara ya taa rangi ya kijani pamoja na maelezo kwa kiarabu kwamba hapa ndipo sehemu ya kuanzia na kumalizia Tawaaf. Nikaelekea kona lilipo Hajarul Aswad (jiwe jeusi) na kuliashiria na kusema Allaahu ‘Akbar na kuanza Tawaaf huku Al Kaabah ikiwa kushoto kwangu.

Siku hii na umri huu na umati uliokuwepo sikuwa na ubavu wa kulifikia Hajarul aswad na kulibusu kama alivyofanya Mtume Muhammad Swalla ‘Allaahu ‘alayhi wasallam nikabaki kuliashiria tu ambayo pia inakubalika kisheria. Kila nikifika Ruknil Yamani (kona ya Yemen kona ya tatu kabla ya kona ya hajarul aswad) nilitakiwa kuomba dua’a aliyotufundisha Mtume Muhammad Swalla ‘Allaahu ‘alayhi Wasallam na kusema: ` Rabbanaa aatinaa fiddunyaa hasanatan wafil akhirati hasanatan waqinaa ‘adhaaba Nnaar. (Mola wetu tupe katika dunia yaliyo mazuri na katika akhera yaliyo mazuri na utuepushe na adhabu ya moto)

Umati uliokuwepo ukifanya Tawaaf ukanikumbusha kwamba kwenye Baytul Ma’amuur, mbinguni kuna umati kama huu wa Malaika nao ukifanya Tawaaf. Tofauti na umati uliokuwepo baytul haraam na baytul ma’amuur ni kwamba umati wa baytul maa’muur hufanya tawaaf mara moja katika uhai wao na hawarudi tena! Allaahu Akbar

Nikiendelea kufanya Tawaaf kwa kuizunguka Al Ka’abah mara saba na kila nikifika eneo la Hajarul aswad niliashiria na kusema Allaahu Akbar. Ilikuwa ni wakati wa adhuhuri jua likiwa kali na tayari nimeshapata kufanya mwendo tokea Mina hadi Jamaraat, Jamaraat hadi Aziziyah, Aziziyah hadi Al Ka’abah na sasa nikiendelea na mwendo wenye kheri na Baraka wa Tawaaf, sikuhisi machofu ya aina yoyote.

Nilipofanya Tawaaf na nikabahtika kuifanya kwenye Mataaf (sehemu ya chini ya kutufu karibu na ‘Al Ka’abah) nilikuwa nnajiuliza inawezekana katika mojawapo ya sehemu nimepita ni sehemu alipopita Mtume Swalla ‘Allaahu ‘alayhi wasallam alipofanya Hijja yake kwa hivyo nimeweza kupata angalau Sunnah. Ila nitajuaje kama nimeipatia?

Naam kwenye Mataaf kuna msongamano, kuna mchanganyiko wa wanawake na wanaume lakini yote haya hayakunijia katika mawazo yangu. Kilichokuwepo katika mawazo yangu ni kupata fursa nadra ya kuwa karibu sana na Al ka’abah – nyumba ya kwanza iliyoasisiwa kwa ajili ya Ibada. Allaahu Akbar! Kama ni unyenyekevu basi ukiwa karibu na Al Ka’abah utaupata wa hali ya juu. Kama ni udhalili basi ukiwa karibu na Al Ka’abah utaupata wa hali ya juu. Ni hisia ambazo haziwezi kuelezeka mpaka uwepo mwenyewe karibu na nyumba ya Allaah ‘Azza wa Jall ndipo utakapozifahamu hisia hizi. Kama bado hujafanya ibada ya Hijja ndugu yangu katika Imani, jihimu na fanya haraka.

Nilipomaliza kufanya Tawaaf ambayo ilinichukua takriban saa 1.15 nikatafuta sehemu nyuma ya Maqaamu Ibrahim kwa ajili kusali Sunnah rakaa mbili, sikuipata kutokana na zahma na msongamano. Nikatafuta sehemu tu na nikaswali rakaa mbili , rakaa ya kwanza nilisoma Alhamdu na Qul Yaa ayyuhal Kaafirun na rakaa ya pili nilisoma alhamdu na Qul huwa Llaahu ahad. Ndivyo alivyotufundisha Mtume wetu Swala Allaahu ‘alayhi wasallam.

Baada ya hapo nikaelekea sehemu yalipo maji ya zamzam, nikanywa kadri ya kiu yangu huku kila nikinywa huomba du’aa. Mtume Swalla Allaahu ‘alayhi wasallam alituagiza tunapokunywa maji ya zamzam ni dawa ya maradhi na pia kujipangusa katika sehemu za mwili.


Nilipomaliza nilitakiwa kurudi tena na kulibusu Hajarul aswad lakini haikuwezekana kutokana na msongamano nikabakia kuliashiria tu.

Itaendelea...

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.