Habari za Punde

Kumbukumbu ya Hijja na athari zake - 5

Bado niko katika siku yangu ya tatu ya mafunzo na nilipomaliza funzo la Tawaaf nikaanza funzo la Sa’iy.

 Sa’iy ni kwenda matiti kati ya Jabal Swafaa na Jabal Marwah. Milima hii imo ndani ya Msikiti ambako kumetengenezwa eneo maalum la kjufanya ibada hii. Fundisho hili ni muhimu kwa ni mojawapo katika mambo ambayo lazima niyafanye ili Hijja yangu ikamilike ni mojawapo ya nguzo za Hijja.

Fundisho hili lina mazingatio makubwa kwani linatukumbusha kisa cha mke wa Nabii Ibrahiym ‘alayhis salaam alipomwacha mkewe bi Hajrah na mtoto mchanga Nabii Ismaail ‘alayhis salaam kwenye jangwa lisilokuwa na chochote wakati huo. Na Bi Hajrah alimuuliza Nabii Ibrahiym ‘alayhis salaam: “kwanini unatuacha hapa?” Nabii Ibrahiym ‘alayhis salaam hakumjibu kitu mpaka alipomuuliza: “hivi ndivyo alivyokuamrisha Mola wako?” Akajibu: “naam” basi Bi Hajra akasema: “Mola wetu hatotuacha mkono”.

Ni kisa kirefu ila fundisho muhimu ni pale Bi Hajrah alipoishiwa na maji na akawa anatafuta kila upande akihaha huku na kule akienda katika ya Jabal Swafaa na Marwah. Na kila akipita sehemu alipomwacha Ismaaiyl na kumsikia akilia alizidisha mwendo kutafuta maji.

Naam tunafanya Sa’iy kwa kumkumbuka mke wa Nabii Ibrahiym ‘alayhis salaam alipokuwa akihangaika kutafuta, maji kwa ajili ya mwanawe.

Nikafika Jabal Swafaa ambapo hutakiwa kuanzia na kumalizia Marwah. Nilipoweka mguu wangu kwenye mlima Swafaa nikasoma aya Inna Swafaa walmarwata min sha’aairi Llaah, faman hajjal bayta awi’itamara falaa junaah ‘alayhi an yatawwafa bihimaa, wamna tattawa’a khayran, Fainna Llaah Shaakirun ‘aliym. (Suuratul Baqarah 158)

Nilipomaliza nikasema kama alivyosema Mtume Swalla Allaahu ‘alayhi wasallam – abdau bimaa bada-a Llaahu bihi ( Ninaanza kwa kile ambacho Allaah alianzia)

Kisha nikapanda Jabal Swafaa (ukitaka kulipata Jabal Swafaa itakubidi ufanye Sa’iy chini na si kwenye ghorofa ya kwanza au ya pili) mpaka kufikia sehemu ambayo ninaweza kuliona Al Ka’abah, nikaelekea qiblah na kisha nikaomba dua’a aliyotufundisha Mtume Swalla Allaahu ‘alayhi wasallam

Kisha nikaanza kutembea kutoka Jabal Swafaa nikielekea Marwah ili kukamilisha mzunguko mmoja.

Nilipofika kwenye alama za taa za kijani (karibu na Jabal Swafaah) nikaongeza mwendo na kwenda mwendo wa haraka (ni Sunnah kwa wanaume tu jambao ambalo pia hushangaza kwani alietuletea utaratibu huu ni mwanamke , mke wa nabi Ibarhiym ‘alayhis salaam) na zilipomalizika alama nikaendelea na mwendo wa kawaida hadi nilipopanda Jabal Marwah nikasoma kama nilivyosoma nilipanza Jabal Swafaa na kuendelea na sa’iy.

Nilikithirisha kuomba du’aa na kumkumbuka Allaah ‘Azza wa Jall muda wote wa Sa’iy mpaka nnamaliza.

Kila nikijaribu kupata mazingatio katika Sa’iy naona tuna mengi ya kujifunza kwani chimbuko la maji ya zamzam ni kutokana na Sa’iy aliyoifanya Bi Hajrah. Tukio hili ambalo mamilioni ya waislamu duniani hulifanya kila mwaka ni limeanzia na Bi Hajrah wakati alipokuwa akihangaika kwa ajili ya mwanaye mchanga. Kwanini Nabii Ibrahiym ‘alayhis Salaam amuwache mkewe kwenye jangwa ambalo halina kitu wala watu wala maji? Majibu ya masuala haya ndiyo hii nyumba ya mwanzo iliyoasisiwa kwa Ibada. Allaahu Akbar.  

Alhamdulillaah nimemaliza fundisho muhimu la Hijja ambalo limehitaji kutumia mwendo wa miguu kama ilivyokuwa Tawaaful Ifaadhah, kama ilivyokuwa safari yangu kutoka Mina hadi Jamaraat, Jamaraat hadi Aziziyah, Aziziyah hadi Haram.

Naam mwili sasa niliusikia kama umechoka na kipande cha kurudi Aziziyah nilipofikia kilikuwa si kidogo kutembea kwa miguu na bado nitatakiwa kutembea tena usiku kurudi Mina.

Niliamua kuchukua Taxi na kurudi Aziziyah ambapo nilipofika kabla ya kupumzika nilitekeleza fundisho jengine la Hijja la kunyoa nywele zote.  Naam mara nyingi huwa sinyoi kipara, hupunguza tu nywele zangu lakini ili Hijja yangu iwe na ubora niliamua kunyoa kwani Mtume Swalla Allaahu ‘alayhi wasallam aliwaombea du’aa mara tatu walionyoa na mara moja waliopunguza.

Baada ya kumaliza kunyoa sasa nimetahallal kikamilifu yaani yale mambo yote niliyokatazwa wakati nipo katika Ihraam sasa nimeruhusiwa mpaka kustarehe na mke .

Natumai uliebahatika kusoma waraka huu utaweza kufaidika japo kidogo hasa kwa kuzingatia ibra – mazingatio yanayopatikana katika Ibada ya Hijja na Umrah na Allaah atuwafikishe katika kila lililokuwa na kheri kwetu.

Aamiyn


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.