Habari za Punde

Taarifa kwa Vyombo vya Habari.

Maadhimisho ya Miaka 50 tangu kuanzishwa kwa Tume ya Kudumu ya Uchunguzi (TKU) 
Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora kwa kushirikiana na Taasisi ya Mwalimu Nyerere (The Mwalimu Nyerere Foundation) zinaujulisha umma kwamba tarehe 21 Oktoba, 2016 kutakuwa na Maadhimisho ya miaka 50 tangu kuanzishwa kwa Tume ya Kudumu ya Uchunguzi wa malalamiko ya wananchi kuhusu matumizi mabaya ya madaraka, yatakayofanyika katika ukumbi wa Karimjee  jijini Dar es Salaam kuanzia saa mbili asubuhi hadi saa saba mchana.

Maadhimisho hayo yatakayowashirikisha viongozi, watu mashuhuri na wawakilishi kutoka taasisi mbalimbali ndani na nje ya nchi, yatahusisha Kongamano litakalojadili mada mbalimbali kuhusu utawala bora na utawala wa sheria nchini.

Mgeni rasmi katika Maadhimisho hayo atakuwa Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Harrison Mwakyembe (Mb) atakaye mwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Joseph Magufuli.

Tume ya Kudumu ya Uchunguzi ilikuwa taasisi ya kwanza ya ‘Ombudsman’ kuanzishwa barani Afrika mwaka 1966. Kauli mbiu ya Maadhimisho ni: “Utawala wa Sheria ndiyo Msingi Mkuu wa Utawala Bora” (Rule of law is the foundation for good governance).

Aidha, Maadhimisho haya yanalenga kuangalia uzoefu tulioupata na kujifunza kutokana na mafanikio/mapungufu na changamoto zilizojitokeza katika kipindi hicho, kwa lengo la kuangalia hali ilivyo hivi sasa; ikiwa ni tathimini ya kuona iwapo TKU ilifikia matarajio ya wananchi au la; na kuona jinsi ambavyo THBUB imeendelea na majukumu ya TKU tangu mwaka 2001 hadi sasa.

Pamoja na Kongamano litakalofanyika, Maadhimisho haya yatatumika kutambua michango ya watu mbalimbali katika kuinua masuala ya utawala bora nchini.

Kwa upande wa Kongamano, miongoni mwa mada zitakazowasilishwa ni pamoja na: Chimbuko, changamoto na mafanikio ya TKU: 1966 – 2001 (Origin, challenges and successes of PCE: 1966 – 2001), itakayotolewa na Jaji mstaafu wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Gad Mjemmas, ambaye pia aliwahi kufanyakazi TKU, kama Mwanasheria (Legal Officer) na baadaye kama Katibu Mtendaji wa THBUB.

Mada nyingine ni: Uzoefu wa Afrika wa Taasisi za ‘Ombudsman’ (African Experiences with Ombudsman Institutions), itakayowasilishwa na Mwakilishi kutoka Jumuiya ya taasisi za Uchunguzi wa Malalamiko ya Wananchi na Wapatanishi Afrika (African Ombudsman and Mediators Association – AOMA).

Prof. Paramagamba Kabudi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam atawasilisha mada itakayoangalia “Kutoka TKU hadi THBUB: Tathimini Linganifu ya Changamoto zilizopo na Matarajio” (From PCE to CHRAGG: Comparative Analysis of Contemporary Challenges and Expectations.

Aidha, Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi Tanzania, Mhe. Jaji mstaafu Damian Lubuva atatoa hotuba itakayoeleza uzoefu wake na TKU ukizingatia kuwa alifanyakazi kama Mwanasheria (Legal Officer) wa TKU na baadaye kushika nyadhifa muhimu hapa nchini.

Hivyo, Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora inapenda kukumbushia umuhimu wa kuzingatia utawala wa sheria, na kwa kufanya hivyo tutakuwa tunamuenzi Hayati Baba wa Taifa, Mwl. Julius Kambarage Nyerere na kudumisha mawazo yake ambayo ndiyo ulikuwa msingi wa kuanzishwa kwa Tume ya Kudumu ya Uchunguzi.

Nimalize kwa kuwashukuru ndugu zangu waandishi wa habari kwa ushirikiano wenu na kwa kuitikia wito wetu na kuhudhuria mkutano wa leo.

Ahsanteni kwa kunisikiliza.

Utawala wa Sheria ndiyo Msingi Mkuu wa Utawala Bora”.
  
(SIGNED)

Iddi Ramadhani Mapuri
Makamu Mwenyekiti

TUME YA HAKI ZA BINADAMU NA UTAWALA BORA
  
Kwa taarifa zaidi tafadhali wasiliana na:

Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora

+255 784 329 900; 714 000 341; 784 345 352

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.