Habari za Punde

Tembeleeni hospitali kushuhudia changamoto


Na Haji Nassor, Pemba

WAJUMBE wa baraza la wawakilishi, wameshauriwa kujenga utamaduni wa kutembelea hospitali na vituo vya afya kila muda mfupi, ili kubaini changamoto zilizomo na kuisaida serikali kuzitatua.

Rai hiyo imetolewa na mjumbe wa baraza la wawakilishi nafasi za vijana mkoa wa kusini Pemba, Mhe: Zulfa Mmaka Omar, wakati alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari, mara baada ya kushiriki usafi katika hospitali ya Chakechake na kutembelea wodi ya watoto na kuwapa zawadi.

Alisema wajumbe wa baraza hilo, kama wakijenga utamaduni wa kuvitembelea vituo hivyo, wanaweza kukumbana na changamoto kadhaa na kisha kuzitatua.

Alisema suala la huduma za afya kwa jamii, wala halihusiana na chama chochote, bali ni la wananchi wote wakiwemo hao wawakilishi, ambao wanaweza kuishauri serikali wakati wowote.

Mhe: Zulfa alisema pamoja na wizara ya afya kujitahidi katika kutoa huduma kwa wananchi na kwa wakati, lakini changamoto kubwa inayojitokeza, ni ongezeko la idadi ya watu kila siku.

“Mimi naona huduma zipo vizuri, lakini na sisi wajumbe wa baraza la wawakilishi, tunayo nafasi ya kuisaidia serikali yetu, kwa kutembelea na kujiona kwa macho yetu mapungufu yaliomo’’,alifafanua.

Akizungumzia zoezi la usafi alioufanya kwa kushirikiana na vijana, alisema waliamua kutokana na jengo hilo kutumiwa na kila mmoja.

“Hatukupenda kufanya usafi kwenye majengo ya chama wala ofisi na taasisi za serikali, maana humo wamo wahusika tu, lakini hapa hospitali kila mmoja anafika kufuata huduma’’,alifafanua.

Aidha alisema waliamua kufanya usafi huo, ili kuunga mkono juhudi za viongozi wa nchi, ambao wamekuwa wakihamasisha usafi wa mazingira katika maeneo kadhaa.

Akizungumza mara baada ya usafi huo, mkuu wa bustani wa hospitali hiyo  Ali Omar Ali, alisema hatua ya kushirikiana katika usafi huo, umempa ahuweni kwa vile pana upungufu wa wafanyakazi katika sekta hiyo.

Nae Mwenyekiti wa Vijana shehia ya Wara alieungana na mwakilishi huyo Halib Bedui Khamis, alisema kwa sasa wanafikiria kila mwisho wa mwezi, kufanya usafi katika hospitali hiyo.

“Mwakilishi wetu wa vijana mkoa wa kusini Pemba, ametuamsha kwamba usafi ni lazima, sasa na sisi tunafikiria kukutana kila mwezi ili kufanya usafi’’,alifafanua.

Nae daktari dhamana wa hospitali hiyo Ali Habib, alimpongeza mwakilishi huyo kuendeleza sera ya usafi na kuamua kuingia hospitalini hapo.

“Mimi kwa niaba ya uongozi na wafanyakazi wa hospitali hii ya Chakechake, niseme tumefarajika sana kupata kikundi cha vijana wakiongozwa na Mwakilishi kufanya usafi, na hii ni sadaka kubwa’’,alifafanua.

Nae mwakilishi wa Jimbo la Chakechake Mhe: Suleiman Zaharan alisema wataendelea kufanya usafi na kusaidia dawa kwenye hospitali mbali mbali, ili kuunga mkono juhudi za serikali.


Mwakilishi huyo wa nafasi za vijana mkoa wa kusini Pemba, pamoja na vijana na wananchi wengine walifanya usafi nje za wodi za watoto, wagonjwa wa TB na kukata majani hospitalini hapo.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.