STATE
HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF
THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar 30.11.2016
![---](file:///C:/Users/User/AppData/Local/Temp/msohtmlclip1/01/clip_image002.gif)
RAIS wa Zanzibar
na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amesema kuwa Zanzibar
itaendeleza uhusiano na ushirikiano wa kihistoria uliopo kati yake na Kenya na
kuahidi kurejeshwa utamaduni wa safari za meli kati ya Zanzibar na Mombasa kwa
kutumia meli yake mpya ya MV Mapinduzi II.
Dk. Shein aliyasema
hayo leo, huko Ikulu mjini Zanzibar wakati alipofanya mazungumzo na Balozi wa Kenya katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Chirau Ali Mwakwere.
Katika mazungumzo
hayo, Dk. Shein alimueleza Balozi Mwakwere kuwa mbali ya ujirani wa mipaka kati
ya Zanzibar na Kenya pande mbili hizo pia, zina udugu wa asili ambao ulikuza uhusiano wa kiuchumi na
kiutamaduni, hivyo ipo haja ya kuuendeleza.
Aidha, Dk. Shein
amelipokea mikono miwili ombi la Balozi huyo la kuimarisha ushirikiano katika usafiri
wa baharini kwa kuanzisha safari za meli kati ya Zanzibar na Mombasa, jambo
ambalo Rais alisema kuwa limo katika mipango ya kutekelezwa.
Alieleza kuwa Serikali
ya Mapinduzi ya Zanzibar imedhamiria kurejesha safari za meli zilizokuwepo hapo
siku za nyuma baina ya Mombasa na visiwa vya Zanzibar na si muda mrefu safari
hizo zitaanza huku akieleza kuwa safari za Tanga, Mtwara, Dar-es-Salaam na hata
Comoro nazo zitajumuishwa.
Mbali na hilo, Dk.
Shein aliunga mkono wazo la Balozi Mwakwere la kubadilishana uzoefu wa
kitaalamu kati ya wanafunzi wa Vyuo Vikuu vya Zanzibar na vyuo vikuu vya nchini
Kenya na kueleza kuwa hatua hiyo itazidi kuimarisha uhusiano na ushirikiano
uliopo kati ya pande mbili hizo sambamba na kuinua sekta ya elimu.
Dk. Shein alimueleza
Balozi Mwakwere kuwa kumekuwa na uhusiano wa kidugu na wa kihistoria kati ya Tanzania
na Kenya hatua ambaye imeipelekea kuwepo kwa Ubalozi Mdogo wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania huko mjini Mombasa.
Aidha, Dk. Shein
alieleza kuwa nchi mbili hizo zimekuwa na historia ya kusaidiana pale nchi moja
wapo inapopata matatizo, hivyo ana imani kubwa utamaduni huo utaendelezwa kwa
manufaa ya pamoja.
Nae Balozi wa Kenya
katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Chirau Ali Mwakwere alimueleza Dk.
Shein kuwa Kenya inajivunia uhusiano na ushirikiano wa kihistoria uliopo kati
yake na Zanzibar na kuahidi kuukuza na kuuendeleza.
Katika kuendeleza na
kuukuza uhusiano na ushirikiano huo, Balozi Mwakwere alitoa ombi maalum kwa Dk.
Shein kurejeshwa utamaduni uliokuwepo hapo siku za nyuma za kuwemo usafiri wa baharini
kati ya Zanzibar na Mombasa.
Aidha, Balozi Mwakwere
alimueleza Dk. Shein haja ya kuwepo kwa uhusiano na ushirikiano wa kubadilishana
uzoefu na utaalamu wa wanafunzi kati ya
vyuo vikuu vya Zanzibar na vile vya kenya ili vijana waweze kuutambua na
kuukuza uhusiano uliopo.
Balozi Mwakwere
alitumia fursa hiyo kutoa pongezi kwa Dk. Shein kwa kuendelea kuiongoza
Zanzibar kwa amani, utulivu na maendeleo na kuahidi kuwa Kenya chini ya uongozi
wa Rais Uhuru Kenyata itaendelea kuiunga
mkono Zanzibar katika juhudi zake hizo.
Alisema kuwa kwa vile
Kenya hasa maeneo yake ya ukanda wa pwani tamaduni, silka na desturi zake
zimeshabihiana na Zanzibar ni vyema uhusiano na ushirikiano wa kihistoria uliopo
ukaimarishwa zaidi hasa katika sekta ya biashara na utalii.
Aidha, alisema kuwa
Serikali ya Kenya imechukua juhudi za makusudi katika kuhakikisha maeneo ya ukanda
wote wa Pwani ya nchi hiyo unaendelea kutunza utamaduni, silka na desturi zao
za asili.
Sambamba na hayo,
Balozi Mwakwere alipongeza hatua za kuendelea kuyalinda na kuyatunza Mapinduzi
ya Januari 12, 1964 ambayo yaliondosha unyonge na kuleta utu na demokrasia na
kuifanya Zanzibar iweze kujisimamia mambo yake wenyewe.
Balozi Mwakwere alitoa
pongezi kwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na watu wake kwa kuendelea kuilinda
na kuitunza lugha ya Kiswahili ambayo imekuwa lugha maarufu ndani na nje ya Bara
la Afrika na kusema kuwa wananchi wa Kenya wamekuwa wakikizungumza na kukipenda
Kiswahili cha Zanzibar ambacho ndicho cha asili.
Rajab
Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment