Habari za Punde

Umoja wa Mataifa washirikiana na FURSA kuwafikia vijana zaidi ya 10,000

Umoja wa Mataifa umeingia ushirikiano na FURSA ili kuongeza uelewa wa malengo ya maendeleo endelevu kwa vijana zaidi ya 10,000 katika mikoa mitatu ya Dodoma, Dar es Salaam pamoja na Kigoma.
Fursa, ambayo imekuwa ikifanyika kwa miaka mitatu iliyopita, imejikita katika kuwajengea uwezo vijana wa kuzitambua fursa katika maeneo yao wanayoishi lakini pia namna ya kutengeneza miradi na biashara kupitia fursa hizo.
Ushirikiano wa Fursa na Umoja wa Mataifa utalenga kuwafikia vijana wanaohudhuria semina za Fursa kuelewa namna Malengo ya Dunia yanavyohusiana na maisha yao ya kila siku na wajibu wa kila kijana katika kushiriki kuyakamilisha.
Akizungumza wakati wa kuzindua semina za Fursa mkoani Dodoma, Mratibu Mkazi wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa nchini na Mwakilishi wa Shirika la Maendeleo (UNDP), Alvaro Rodriguez alisema semina za Fursa zimeweza kubadilisha maisha ya vijana wengi na hivyo ushirikiano wake na Umoja wa Mataifa katika kufikia vijana utatoa nafasi ya vijana kuyaelewa Malengo ya Dunia.
‘Vijana wengi wana ari ya kushiriki katika kufanikisha Malengo ya Dunia, ndio maana Umoja wa Mataifa umeamua kushirikiana na Fursa ili kuhakikisha vijana wengi zaidi wanayafahamu malengo haya lakini pia wanashiriki katika kuyatekeleza’ alisema Alvaro.
Kwa upande wake, Mwanzilishi wa Fursa, Ruge Mutahaba amesema kwa zaidi ya miaka mitatu sasa Fursa imefanikiwa kuwafikia zaidi ya vijana milioni 5, na kuwapa mbinu na maarifa ya kuweza kutumia fursa katika maeneo yao.
‘Tunaushukuru Umoja wa Mataifa kwa kushirikiana na Fursa kuwafikia vijana katika mikoa ya Dodoma, Dar es Salaam na Kigoma, ili sio tu wapate nafasi ya kupata mafunzo ya Fursa na biashara balipia mafunzo juu ya Malengo ya Dunia’ alisema Ruge.


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.