Habari za Punde

Jumla ya Bilioni 2.8 zakusanywa ununuzi wa madawati kwa skuli za Msingi na Sekondari za SMZ



STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
  Zanzibar                                                          22.04.2017
---
JUMLA ya Shilingi za Kitanzania Bilioni 2.8 zimekusanywa kwa ajili ya ununuzi wa madawati kwa skuli za Msingi na Sekondari za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar huku ikiwa bado wadau wengine wanaendelea kuhamasishwa kuchangia.

Fedha hizo zimetajwa leo na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein katika hafla ya Uhamasishaji na Uchangiaji Madawati ya Skuli za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, hafla iliyofanyika katika ukumbi wa zamani wa Baraza la Wawakilishi, mjini Zanzibar.

Dk. Shein alisema kuwa miongoni mwa fedha hizo ni Shilingi milioni mia tano (500,000,000) ambazo zimetolewa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika hafla hiyo na Tsh. Bilioni 1.8 za ahadi zilimetolewa leo ambapo milioni 483 zilishakusanywa hadi mwishoni mwa mwezi wa Machi mwaka huu.

Mapema Dk. Shein akitoa hotuba yake katika uzinduzi wa hafla hiyo alisema kuwa suala la elimu ni suala lenye historia kubwa kwa mwananadamu ambalo linagusa maendeleo yote duniani.

Dk. Shein alisema kuwa miongoni mwa ahadi za ASP wakati wa kugombea uhuru ni kutoa elimu bure kwa wananchi wote wa Unguja na Pemba pamoja na sekta nzima ya afya.

Aliongeza kuwa kutangazwa kwa Elimu bila ya malipo ndio kulikofungua milango kwa watoto wote wa wenyewe uwezo na wasio na uwezo kupata elimu kutokana na tangazo la mwanzo la elimu bure la tarehe 23.9.1964.

Alisema kuwa jitihada kubwa zimechukuliwa na Serikali tokea mwaka 1964, licha ya changamoto kuwepo na ndio maana Serikali imechukua uwamuzi wa kuwaita viongozi wake wote katika hafla hiyo ili na wao waiunge mkono Serikali yao katika kuchangia madawati.

Alieleza imani yake kuwa hilo litawezekana kwani hakuna wa kumuachia, kwani Serikali ni wananchi wenyewe na viongozi kazi yao ni kusimamia tu na kusisitiza kuwa lengo la elimu bure pamoja na Sera yake iko pake pale, na utekelezaji wake unatofautina na ule wa mwaka 1964 kwa kutokana na mabadiliko ya mazingira.

“Hatuwezi kuongoza Serikali kwa zao la karafuu peke yake na ndio maana tumeona haja ya kuongeza mambo mengine ya kuimarisha uchumi wetu ... baada ya Mapinduzi Zanzibar idadi yetu tulikuwa  laki tatu lakini leo tuko milioni moja na laki nne”alisisitiza Dk. Shein.

Aidha, alieleza kuwa baada ya Serikali kukwazwa na mambo mengi ndio hapo iliwaomba wananchi wachangie na hadi kufikia mwaka 2014 katika Sherehe za Mapinduzi alitangaza tena uwamuzi ule ule wa Marehemu Mzee Abeid Karume kuwa wazee wasichangie tena elimu na jukumu hilo litachukuliwa na Serikali.

Aliongeza kuwa azma ya Serikali kwa hapo baadae ni kuhakikisha kuwa Skuli za Sekondari nazo hazitokuwa na michango ya aina yoyote na kusisitiza kuwa dhana ya Elimu bure ni kuhakikisha mambo yote yanasimamiwa na Serikali ikiwa ni pamoja na kujenga skuli, vifaa, mishahara, umeme, maji na mambo yote ya kuendesha skuli ni jukumu la Serikali.

Dk. Shein alimshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania John Pombe Magufuli kwa kuipatia Zanzibar mgao madawati ikiwa ni mchango wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania  katikan kukabiliana na tatizo la madawati kwa skuli za Zanzibar.

Pia, aliwapongeza Wabunge wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wa Majimbo ya Zanzibar kwa kutoa michango ya madawati na kuyakabidhi katika skuli za majimbo yao, na kuwapongeza Wawakilishi kwa kutoa michango yao ya fedha kwa madawati ya skuli.

Alizipongeza Wizara za Serikali, Ofisi zote za Wakuu wa Mikoa, Ubalozi wa Japan pamoja na Mashirika yote ya Serikali na yasiokuwa ya Serikali huku akieleza azma ya Serikali ya kuanzisha Mfuko Maalum wa Madawati.

Dk. Shein alieleza kuwa kutoa ni moyo si utajiri na kusisitiza kuwa umoja ni nguvu na iwapo mshikamano utakuwepo fedha za kununulia madawati zitapatikana na kuhakikisha kuwa kabla ya Disemba ya mwaka huu fedha za ununuzi wa madawati zimepatikana na suala hilo litakuwa historia.

Pamoja na hayo, Dk. Shein alitumia fursa hiyo kutoa shukurani kwa Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi  ambapo mara tu baada ya uwasilishaji wa rasimu hiyo Katika Kikao cha Baraza la hilo walianza kutoa michango yao kwa ajili ya ununuzi wa madawati hayo.

Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali, Riziki Pembe Juma, alisema kuwa pamoja na juhudi kubwa ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kuongeza bajeti ya Wizara ya Elimu na Mfunzo ya Amali kila mwaka na kwa mwaka 2016/2017 imefikia asilimia 20 ya matumizi ya Serikali, kiwango ambacho ndio kinachotakiwa kimataifa lakini bado baadhi ya changamoto zipo ikiwemo uhaba wa madawati.

Aliongeza kuwa hivi sasa Wizara ya Elimu inatumia Tsh. Milioni 31 kila mwezi kwa gharama za uji kwa skuli za maandalizi, imenunua madaftari kwa ajili ya skuli za maandalizi na msingi na kueleza kuwa wazazi hivi sasa hawapaswi kugharamika kununua madaftari kwa matumizi ya watoto wao wakiwa pia watoto wa maandalizi na msingi wamepewa vitabu.

Alisema kuwa takwimu zinaonesha kuwa kuna uhaba wa madawati 41,871 kwa ajili ya skuli za msingi na viti 43,489 na meza 43,489 kwa ajili ya skuli za Sekondari za Serikali licha ya Serikali kutoa fedha kila mwaka kupitia kodi ya Bandari lakini kiwango cha fedha kinachokusanywa hakilingani na ongezeko kubwa la wanafunzi.

Nae Mwenyekiti wa Kamati hiyo ambaye pia, ni Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Katiba, Sheria, Utumishi wa Umma na Utawala Bora Haroun Ali Suleiman alimueleza Rais Dk. Shein kuwa jambo hilo ni zito lakini kutokana na mshikamano , litafanikiwa kama yalivyofanikiwa mambo mengi hapo siku za nyuma.

Alisema kuwa waliohudhuria katika hafla hiyo ni  kutoka Mashirika na Taasisi za Serikali wakiwemo viongozi wa Serikali na kueleza kuwa washirika wengine na wafanyabiashara wataalikwa kwa awamu nyengine ijayo na kuahidi kuwa tatizo hilo watalisimamia na kuhakikisha linakuwa historia kwa skuli za Unguja na Pemba

Waziri Haroun alimpongeza Dk. Shein kwa kuivalia njuga sekta ya elimu na kupunguza minung’uniko ya wazee kwa watoto wao kutokana na kuondoa  michango na kusema kuwa hatua hiyo inatekelezwa kutokana na utelekezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya mwaka 2015-2020.

Nao Wakuu wa Mikoa yote mitano ya Zanzibar walioa taarifa ya mikoa yao inayohusiana na michango ya fedha zilizopatikanwa na zinazoendelea kupatikanwa kutoka katika vyanzo mbali mbali vya fedha pamoja na wafanyabiashara, mashirika na taasisi mbali mbali za Serikali na Binafsi zilizokuwemo katika Mikoa hiyo.

Viongozi hao walitumia fursa hiyo kutoa michango yao ikiwa ni fedha taslim, ahadi za kutoa madawati na fedha kwa ajili ya kuchangia madawati kwa skuli zote za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.