Habari za Punde

Rais Dk Shein ahuzunishwa na maafa, aahidi wananchi misaada na kurekebisha miundo mbinu




STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar                                                                  14.05.2017
---
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amehuzunishwa kwa kiasi kikubwa na maafa yaliotokezea Unguja na Pemba kufuatia mvua zinazoendelea kunyesha na kuwaahidi wananchi kuwa Serikali yao itahakikisha inawapa misaada inayohitajika pamoja na kuzifanyia kazi athari zilizotokea zikiwemo uharibifu wa miundombinu ya barabara.

Dk. Shein aliyasema hayo leo katika ziara yake aliyoifanya katika maeneo mbali mbali ya Unguja yaliyoathirika na mvua kubwa za masika zinazoendelea kunyesha ambazo zimepelekea baadhi ya wananchi kukosa makaazi baada ya nyumba zao kubomoka, kuharibika kwa miundombinu ya barabara, madaraja pamoja na kuharibika kwa mazao.

Miongoni  mwa maeneo aliyoyatembelea katika ziara yake hiyo ni eneo linalotuama maji Mwanakwereke, kuangalia mafanikio ya ujenzi wa mtaro mkubwa wa kupitishia maji kupitia Mradi wa Huduma za Jamii Mijini (ZUSP) huko Karakana, Bumbwisudi kwa Goa, Mwera Gudini, Fuoni Kibonde Mzungu,  Daraja la Mwanakwerekwe Nyumba Mbili ambapo katika Mkoa huo wa Mjini Magharibi nyumba zilizoathirika ni 1,130.

Katika ziara yake hiyo ambayo viongozi mbali mbali walishiriki, Dk. Shein pia, alipewa taarifa mbali mbali kutokana na athari za mvua hizo za masika kutoka kwa viongozi husika ambao pia, walieleza juhudi zinazoendelea kuchukuliwa sambamba na azma ya Serikali katika kukabiliana na maafa kama hayo katika maeneo yaliyoathirika.

Akiwa katika eneo linalotuama maji la Mwanakwerekwe, Dk. Shein alisisitiza haja ya kufanywa kwa uchunguzi wa kina katika kulitafutia ufumbuzi tatizo la kutuama maji katika eneo hilo ambalo historia yake halioneshi kuwa eneo hilo linakaa maji kama lilivyo hivi sasa.

Aliongeza kuwa miongoni mwa hatua hizo za uchunguzi ni pamoja na kulifanyia kazi wazo la wa maji hayo yanayotuama kuyapeleka Ziwa Maboga ama kuyatafutia njia kuyapeleka Sebleni, kuyahifadhi maji katika eneo hilo ili yaweze kutumika kwa mahitahji mengine huku akieleza haja ya kufanya taratibu katika kuhakikisha barabara iliyopo katika eneo hilo iweze kupitika wakati wa  msimu wa mvua.

Katika eneo la Karakana Dk. Shein alipongeza mafanikio yaliyopatikana kutokana na Mradi wa (ZUSP)  na kuutaka uongozi wa Jimbo la Chumbuni kwa kushirikiana na wananchi wao kuyaenzi na kuyalinda maeneo ya wazi ambayo hapo siku za nyuma yalikuwa yakituama maji ili waweze kuyafanyia shughuli nyengine za kijamii.

Katika eneo hilo Mkurugenzi wa Idara ya  Mipango Miji Kazi na Ujenzi, Idara ya Manispaa Zanzibar Mzee Khamis Juma alimueleza Dk. Shein mafanikio yaliopatikana kutokana na mradi huo na kumueleza kuwa katika kipindi hichi hakuna mwananchi aliehama ama kupata athari za maji ya mvua zinazoendelea na kueleza jinsi wananchi walivyofurahishwa na juhudi hizo za Serikali.

Nao uongozi wa Jimbo la Chumbuni ulipongeza juhudi za Serikali katika ujenzi wa mradi huo ambao kwa maelezo ya Mbunge wa Jimbo hilo Ussi Salum Pondeza, mafanikio makubwa yamepatikana na kuahidi kushirikiana na Serikali katika kuyaendeleza maeneo ya wazi ambayo siku za nyuma wakati wa mvua za masika yalikuwa yakituama maji.

Dk. Shein pia, alitumia fursa hiyo kuwapa pole wananchi wa Bumbwisudi kwa Goa kwa kupata maafa yaliyotokana na mvua na kupelekea nyumba 66 kuharibika na nyengine kuangua kabisa na kuwapongeza wananchi hao kwa kuonesha moyo mkubwa wa kusaidiana na kustiriana wakati wa maafa hayo kwa wale walioathirika na mvua hizo.

Aliwapongeza wananchi hao kwa kustahamili,kutohadhibika na kutoilaumu serikali na badala yake waliipokea hali hiyo na kumshukuru Mwenyezi Mungu na kueleza juhudi zilizochukuliwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuwapelekea miradi ya maendeleo wananchi wa Bumbwisudi ikiwemo barabara, umeme, elimu, afya na mengineyo. “ Bumbwisudi ya leo sio ile ya zamani”,alisisitiza Dk. Shein.

Dk. Shein aliwaeleza wananchi hao hatua za makusudi zitakazochukuliwa na serikali katika kuhakikisha inaendeleza juhudi zake za maendeleo kwa kutoa mashirikiano kwa wananchi wa Bumbwisudi na maeneo mengine kutokana na athari walizozipata, ikiwa ni pamoja na kuwekwa kwa misingi katika barabara na makalbi yanayokidhi haja.

Akiwa Mwera Gudini, Dk. Shein alieleza azma ya Serikali ya kuijenga kwa kiwango cha lami barabara inayotoka Mwera kupitia Birikani hadi Fuoni meli saba (Kwa Chimbeni), kutokana na umuhimu wake mkubwa.

Huko Fuoni Kibonde Mzungu, Dk. Shein alipata maelezo juu ya hatua zitakazochukuliwa na Serikali kupitia Wizara husika juu ya ujenzi wa daraja litakalokidhi haja katika eneo hilo mara tu mradi wa ujenzi wa barabara kutoka Mwanakwerekwe hadi Tunguu utakavyoendelea awamu ya Pili kutoka Fuoni Polisi ulipofikia hadi Tunguu.

Pamoja na hayo, Dk. Shein alipata maelezo juu ya ujenzi wa daraja la Mwanakwerekwe nyumba mbili, ambalo kwa maelezo ya uongozi wa Wizara ya Ujenzi, Mawasiliano na Usafirishaji, daraja hilo litajengwa kwa kuengezwa upana  ili gari ziweze kupishana pamoja na kuzidishwa umadhubuti zaidi.

Akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya kukamilisha ziara yake hiyo, Dk. Shein alisema kuwa Serikali imekuwa ikijipanga wakati wote katika kukabiliana na maafa na pale yanapotokea  huchukua hatua za makusudi katika kukabiliana nayo.

 Sambamba na hayo, Dk. Shein alisisitiza kuwa Serikali ipo na itaendelea kuwatunza na kuwasaidia wananchi wake pamoja na kushirikiana nao katika maafa kama hayo na kuwataka wananchi kustahamili na kutulia na kusubiri Serikali inasema nini juu ya athari hizo.

Dk. Shein anatarajiwa kuelekea kisiwani Pemba hapo kesho kwa ziara kama hiyo katika maeneo mbali mbali yaliyopata maafa na kuathirika na mvua za masika zinazoendelea hapa nchini.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.