Habari za Punde

Watumiaji wa Barabara Kutoendesha Vyombo Vyao Mwendo wa Kasi.

STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE   
Zanzibar                                                                                                             27.06.2017
---
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhaj Dk.Ali Mohamed Shein ametoa wito kwa madereva wote hapa nchini kutoendesha vyombo vyao kwa mwendo wa kasi ili kuepuka ajali zisizo za lazima hasa katika kipindi hichi cha Sikukuu ya Idd- El- Fitri ambacho wananchi walio wengi hutumia huduma za usafiri wa barabarani wakiwemo watoto.

Alhaj Dk. Shein aliyasema hayo wakati akifanya mahojiano na watoto wanaotayarisha kipindi cha “Watoto na Sikukuu” kutoka Shirika la Utangazaji la Zanzibar (ZBC), huko Ikulu mjini Zanzibar, ikiwa ni miongoni mwa shamrashamra za skukuu ya Idd El Fitri.

Katika maelezo yake, Dk. Shein alisema kuwa uendeshaji wa vyombo vya moto kwa kasi ni hatari hali ambayo inaweza kusababisha ajali zisizo za lazima kwani hakuna sababu ya kufanya hivyo kwa kuepuka kuleta madhara hasa kwa watoto huku akisisitiza haja kwa askari wa barabarani kuwa makini kwa madereva wote wanaoendesha vyombo vyao kwa kasi.

Hivyo, Alhaj Dk. Shein aliwataka madereva wa vyombo vyote vya moto kufuata taratibu, sheria za barabarani sambamba na kuwa makini wakati wakiendesha vyombo vyao kwani katika kipindi hichi cha Sikukuu wananchi waliowengi wakiwemo watoto hutumia barabara kwa safari zao mbali mbali zikiwemo za kwenda kutembeleana pamoja na kwenda katika viwanja vya skukuu.

Alhaj Dk. Shein alisisitiza kuwa Sikukuu ni furaha hivyo kila mmoja ana nafasi na fursa ya kusherehekea lakini kwa upande wa madereva ni vyema wakatumia furaha yao kwa kwenda mwendo mzuri pamoja na kufuata, sheria, kanuni na taratibu za barabara ili kuepuka ajali.

“Na nyinyi watoto msije kuingia kwenye gari halafu mkawatia pampu madereva kwa kuwapigia kelele, ili waendeshe gari zao mbio, huku mkiema ndio babu hivyo hivyo engeza mwendo, si vizuri na mkiiona gari inakwenda mbio basi msipande”,alisisitiza Alhaj Dk. Shein.

Aidha, Alhaj Dk. Shein alieleza azma ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuimarisha michezo kwa watoto ikiwa ni pamoja na kuutekeleza Mpango wa “Sport 55”, unaolenga kuongeza hamasa ya ushiriki wa wanafunzi katika michezo kwa kuzipatia vifaa vya michezo skuli 55 Unguja na Pemba kwa hatua ya awali, kutengeneza viwanja, mafunzo ya kiufundi na kiutawala kwa walimu na viongozi wa michezo kwa kila Wilaya na Mikoa.

Pia, Alhaj Dk. Shein alieleza kuwa katika kutekeleza hilo tayari jumla ya TZS milioni 300 zimeshakushanywa kwa lengo la kutekeleza azma hiyo huku akisisitiza kuwa kila wilaya kutajengwa viwanja vya michezo na zitaanza Wilaya tano na tayari viwanja viwili vimeshaanza kujengwa. “Tunafanya Mpango mkubwa ili watoto wapate kucheza na wacheze katika mazingira yalio bora na yalio mazuri”,alisema Alhaj Dk. Shein.

Akizungumzia juu ya maradhi ya kipindupindu, Dk. Shein alitoa wito kwa wananchi wakiwemo watoto kulipa kipaumbele suala zima la usafi kwani maradhi hayo chanzo chake kikubwa ni uchafu.

Alhaj Dk. Shein aliwaeleza watayarishaji hao uzoefu wake wa maradhi hayo katika mwaka 1968 na mwaka 1998 pamoja na miaka ya hivi karibuni kwa jinsi maradhi hayo yalivyoleta athari kubwa vikiwemo vifo na kueleza umuhimu wa kuimarisha usafi ukiwemo usafi wa mtu mwenyewe, mazingira anayoishi, katika miji na sehemu zote zilizoizunguka jamii.

Kwa upande wa vita dhidi ya dawa za kulenya, Alhaj Dk. Shein alieleza mikakati ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kupambana na dawa hizo kwa wanaoingiza, wanaouza na hata wale wanaotumia na hatua zitaendelea kuchukuliwa kwa mujibu wa sheria na taratibu za nchi.

Kutokana na hatua hiyo, Alhaj Dk. Shein alitoa wito kwa watoto kutoiga tabia za matumizi ya dawa za kulevya na wakimbie wala wasizikurubie kwani zinamadhara makubwa, huku akiwaeleza jinsi Serikali kwa upande wake itakavyoendelendea kuwalinda, kuwaenzi na kuwatunza watoto wote.

Sambamba na hayo, Alhaj Dk. Shein alitoa wito kwa wazazi na walezi kuchukua jitihada za kuwalea watoto vizuri na kuwafundisha maadili mema na silka za Kizanzibari huku akisisitiza haja kwa wazazi na walezi  kuwaandalia watoto vyakula vizuri katika kipindi hichi cha Sikukuu.

Hivi karibuni Alhaj Dk. Shein alipofanya mazungumzo na Mkuu wa Jeshi la Polisi wa Tanzania (IGP) Simon Nyakoro Sirro, aliyefika Ikulu mjini Zanzibar kwa ajili ya kujitambulisha rasmi kwa Rais alimueleza haja ya kuwepo mashirikiano ya kutosha kwa askari wa barabarani pamoja na taasisi husika inayotoa leseni za udereva wa vyombo vya moto ili kuepusha ajali zisizo za lazima ambazo zimekuwa zikitokezea mara kwa mara.

Nao watoto hao kwa niaba ya watoto wenzao wote walitoa pongezi na shukurani kubwa kwa Rais Alhaj Dk. Shein kwa juhudi za makusudi anazozichukua katika kuhakikisha Serikali anayoiongoza inawapenda, inawatunza, inawajali na inawathamini watoto.

Mapema Dk. Shein alipeana salamu za Idd el Fitri na viongozi wa dini pamoja na viongozi wa Serikali hapo Ikulu mjini Zanzibar na baadae kutoa skukuu kwa wananchi mbali mbali waliofika katika viwanja vya Ikulu wakiwemo watoto.
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.