Habari za Punde

Zanzibar yavuliwa uanachama CAF, Wadumu kwa miezi minne tu


SHIRIKISHO la Soka Afrika (CAF) limeiondoa Zanzibar katika orodha ya nchi wanachama wake, miezi minne tu tangu iipe hadhi hiyo.

Rais wa CAF, Ahmad Ahmad amesema Zanzibar, ambayo ni sehemu ya Tanzania haikupaswa kuwa mwanachama wa 55 wa CAF mwezi Machi.

"Walikubaliwa bila kuangalia vizuri sheria ambazo ni wazi," alisema Ahmad. "CAF haiwezi kukubali vyama viwili tofauti kutoka nchi moja.".

"Utambulisho wa nchi unatokana na kwa mwanachama wa Umoja wa Afrika na Umoja wa Mataifa," aliongeza Ahmad  katika Mkutano Mkuu wa CAF nchini Morocco wiki hii.



FIFA walikataa kuipa Zanzibar uanachama, baada ya CAF, chini ya Ahmad kuingia madarakani akimuangusha Mcameroon Issa Hayatou na kukikubalia kisiwa hicho cha 
Afrika Mashariki kuwa mwanachama wake.


Zanzibar ni sehemu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, lakini imekuwa ikiendesha shughuli zake za soka yenyewe.

Machi 16, 2017 ilikuwa ni siku nzuri na yenye historia kubwa kwa Zanzibar baada ya kuingizwa rasmi kuwa Mwanachama wa 55 wa Shirikisho la Soka Barani Afrika “CAF” kufuatia Kikao cha 39 cha Mkutano Mkuu wa Shirikisho hilo kilichofanyika Addis Ababa nchini Ethiopia lakini leo July 21, 2017 ni siku mbaya kwa Zanzibar baada ya kuvuliwa rasmi uanachama huo.

1 comment:

  1. Masikini Zanzibar ni jinamizi gani limekuelemea!

    ReplyDelete

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.