Habari za Punde

Naibu Waziri wa Elimu Akabidhi Msaada wa Vitabu Kutoka Jumuiya ya PSI.

Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar Mh. Mmanga Mjengo Mjawiri akimkabidhi msaada wa vitabu kutoka kwa PSI Mwalimu Kaimu Mwalimu Mkuu wa Skuli ya Mauwani Nd.Mussa Mohd Abass.
Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali Mh. Mmanga Mjengo Mjawiri akitoa nasaha zake kwa Walimu Wakuu wa Skuli zilizopatiwa msaada wa vitabu kutoka kwa Jumuiya ya Pemba  Support Island (PSI)Pamoja na Maafisa mbali mbali wa Elimu Kisiwani Pemba.
Walimu Wakuu wa Skuli zilizopatiwa msaada wa vitabu kutoka kwa Jumuiya ya Pemba Support Island (PSI) pamoja na Maafisa mbali mbali wa Elimu Kisiwani Pemba.

Na Ali Othman Ali
Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar Mh. Mmanga Mjengo Mjawiri amekabidhi msaada wa vitabu vya Sayansi, Hesabati na Kiingereza Uliotolewa na Jumuiya ya Pemba Support Island (PSI) kwa Skuli nne za Sekondari ambazo ni Chasasa, Konde, Shamiani na Mauwani.

Makabidhiano hayo na Walimu Wakuu wa Skuli hizo yamefanyika katika ukumbi wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Chake Chake Pemba mbele ya Maafisa na watendaji mbali mbali wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Kisiwani Pemba.

Akitoa nasaha zake kabla ya kukabidhi vitabu hivyo vyenye thamani ya Shilingi za Kitanzania milioni nne, Tsh 4,000,000/- Mh. Naibu waziri amempongeza Mratibu wa Idara ya Mafunzo ya Ualimu Pemba Maalim Mkubwa Ahmed Omar kwa juhudi zake za makusudi katika kuimarisha huduma za elimu Kisiwani Pemba na amewataka watendaji wengine kuiga mfano wake.

Mh. Mjawiri amewataka walimu hao kuenzi na kutunza vifaa vya zamani kwa matumizi endelevu huku akionesha kutoridhishwa na tabia ya kuvidharau na kutokuvishughulikia vifaa vyazamani na badala yake kujikita katika kushughulikia vifaa na majengo mapya. Ameiamuru Idara ya Ukaguzi kuingiza kipengele cha Ukaguzi katika eneo la vifaa ili kuhakikisha kwamba vinatumika kwa ufanisi na kwa uangalifu.

Aidha, Mh. Naibu Waziri amesisitiza haja ya waalimu kuwa na uzalendo katika utendaji wa kazi zao. Akifafanua dhana ya uzalendo Mh. Mmanga amesema ipo haja kwa walimu kuwa na upendo kwa jamii yao, upendo kwa kazi yao na upendo kwa masomo wanayofundisha ambapo Mh. Naibu Waziri ameonesha wasiwasi wake juu ya kupungua au kutokuwepo kwa moja kati ya hayo.

Kwa upande wa utoaji wa taaluma Mh. Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali amewataka walimu kutimiza wajibu wao katika kuwafundisha wanafunzi na kuwatanabahisha kwamba wanawajibu mkubwa wakusimamia malezi ya vijana.

“Walimu tujikumbushe kwamba tunawajibu wa kulea hivyo basi tufanye kazi kulingana na taaluma zetu, mfanyaka kazi mwenye taalumu hasukumwi katika kutenda majukumu yake, taaluma ndio inayomuongoza kusimamia vyema kazi hiyo”

Mh. Mmanga amesisitiza haja ya kuwashajiisha wanafunzi wawe na moyowakujisomea vitabu kwa wingi akitanabahisha kwamba kufanya hivyo kutawapatia uwezo wa kujenga hoja kitaaluma.

Awali Afisa Mdhamini Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Pemba Mh. Salim Kitwana Sururu amemshukuru Mh. Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar kwa kuwa karibu katika harakati za kukuza maendeleo ya elimu Zanzibar.

Pemba Support Island ni Jumuiya ya misaada ambayo ilisajiliwa rasmi mwaka 2010 ikiwa na namba usajili (CHY 19162) ambapo inatoa misaada mbali mbali yakimaendeleo kisiwani Pemba.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.