Habari za Punde

STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
  Zanzibar                                                                                                              16.08.2017
---
MAWAZIRI kutoka vyama vya upinzani walioteuliwa na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein katika serikali anayoiongoza wameahidi kuendelea kumuunga mkono na kushirikiana nae kwani ameonesha nia thabiti ya kuwaletea maendeleo wananchi bila ya ubaguzi kwa kutambua kuwa maendeleo hayana upinzani.

Viongozi hao waliyasema hayo kwa nyakati tofauti katika ziara ya Dk. Shein ya kutembelea miradi ya maendeleo sambamba na kuangalia utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2015-2020 jinsi inavyotekelezwa katika Mikoa yote ya Unguja na Pemba, ziara ambayo kwa hivi sasa inaendelea katika Mkoa wa Kusini Unguja.

Waziri wa Kilimo, Maliasili,  Mifugo na Uvuvi  Hamad Rashid, katika kijiji cha Mlilile alieleza hatua ambazo Wizara anayoiongoza itazichukua katika kuhakikisha wananchi wa kijiji hicho wanapata mafanikio sambamba na kuweza kuitumia vyema ardhi yao ya mawe na bahari waliyonayo kwa kusogezewa miradi na Serikali ya Mapindyuzi ya Zanzibar.

Waziri Rashid ambaye ni Mwenyekiti wa  Chama cha Alliance for Democratic Change (ADC) alipongeza juhudi za Rais Dk. Shein katika kuwapelekea maendeleo wananchi wa Zanzibar bila ya ubaguzi na kuahidi kuendelea kumuunga mkono kwani maendeleo hayana upinzani.

Alisisitiza kuwa huu ni wakati wa wananchi kwa kushirikiana na viongozi wao wa Serikali kujiletea maendeleo na sio wakati wa kudanganywa na baadhi ya wanasiasa.

Katika ziara ya Dk. Shein akiwa katika kijiji cha Ukongoroni Waziri Rashid alimpongeza Dk. Shein kwa kufanya kazi kwa uadilifu mkubwa na kuifanyia mambo mengi Zanzibar na kusisitiza kuwa si busara kupinga kila kitu kinachofanywa na Serikali anayoiongoza kwani ameifanya mambo makubwa ikiwa ni pamoja kuitoa nchi kuwa tegemezi na kubaikia asilimia saba tu kwani sio jambo rahisi.

Aliongeza kuwa hatua hiyo, hufanywa na Rais makini na aliyetulia kama alivyo Dk. Shein ambaye ameifikisha Zanzibar katika hatua hiyo ambayo ameifanya vizuri huku akieleza hatua za Serikali kupitia Wizara anayoiongoza kwa mashirikiano na Mradi wa MIVARF katika kuwasaidia wakulima wa ndimu wakiwemo wale wa Ukongoroni.

Waziri asiyekuwa na Wizara Maalum, Juma Ali Khatib ambaye pia, ni Mjumbe wa Baraza la Mapinduzi alieleza kuwa wao wakiwa viongozi kutoka vyama vya upinzani wamekuwa wakishuhudia juhudi kubwa anazozifanya Dk. Shein katika kutekeleza Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2015-2020,

Aliongeza kuwa wananchi na wanasiasa wote ni vyema wakatambua na kuthamini juhudi kubwa anazozichukuwa Dk. Shein katika kuwaletea maendeleo wananachi wote wa Unguja na Pemba kwa vitendo.

Waziri Khatib ambaye anatoka chama cha ‘Ada Tadea’, alisema kuwa ahadi alizozitoa katika majukwa ya kisiasa kapmeni za uchaguzi zilizopita, na wakati wa uchaguzi, kwa kweli anatimiza hadi zake hivyo aliwasisitiza wananchi kumuunga mkono Dk. Shein pamoja na seetikali ayake anayoiongoza ili kuleta maendeleo kwa wananchi wote bila ya ubaguzi na bila ya itikadi ya kisiasa.

Aliongeza kuwa maendeleo hayo ni kwa watu wote waliokuwa na vyama na wasiokuwa na vyama na kueleza kuwa yeye yumo ndani ya Serikali anayoiongoza Dk. Shein na anatekeleza Ilani ya CCM na anamsaidia Dk. Shein katika kuhakikisha Serikali inakwenda mbele pamoja na kuhakikisha Ilani hiyo inatekelezwa.

Waziri Khatib katika maelezo yake aliwasisitiza wananchi kuwa hivi sasa hakuna uchaguzi tena na kuwataka wasiendelee kukubali kudanyaganywa kwani uchaguzi uliopo ni ule wa mwaka 2020.

“Nawasihi wananchi wenzagu tusiendelee kudanganywa tukaambiwa kesho keshokutwa asubuhi, Rais wetu ni huyu hapa Dk. Shein, Rais mpendwa watu na wala si mbaguzi maana katika serikali yake ametushirikisha vyema vyama vya upinzani, nani angeweza kufanya mambo kama haya”,alisisitiza Waziri Khatib.

Nae Waziri asiyekuwa na Wizara Maalum, Said Soud Said ambaye pia, ni Mjumbe wa Baraza la Mapinduzi na Mwenyekiti wa Chama cha Wakulima (AFP) Taifa, alisema kuwa tokea asubuhi alimuunga mkono Dk. Shein baada ya kuuona uwezo wake mkubwa wa kuwaongoza Wazanzibari na kuahidi kuendelea kumuunga mkono na kukiunga mkono Chama Cha Mapinduzi.

Alieleza sababu za kuunga mkono huko kunatokana na kuwa vyama vya siasa havikuja kwa lengo la kufarakana na kugombana na watu ama kususiana na kuwataka wananchi kuwakimbia na kuwaogopa kama UKIMWI  wale viongozi wanaoongoza vyama vya siasa wakaanzisha mambo kama hayo.

“Unapoingia katika ngoma ya beni basi ‘phisicali’ beni ni goma kubwa ambalo ni moja tu na zinazobakia zote ni ngoma ndogo ndogo, sasa na hivi vyama vyengine vyote ni vigoma vidogo vidogo, beni ni CCM ndilo linalopigwa na likaingia masikioni na kusisimua”, alisema Waziri Said.

Aidha,  alitumia fursa hiyo kuwaeleza vijana madhumuni ya Mapinduzi Matukufu ya Januari 12, 1964 ambayo yaliwafanya Wazanzibari kuamua kutekeleza mambo yao wenyewe na kuwataka Wazanzibar kutokubali kuamuliwa mambo yao.

“….na Serikali hii anayoiongoza Dk. Shein ina staili ya mdundiko mbele kwa mbele na  haina habari ya kurudi nyumba mmeeleza malalamiko yenu juu ya barabara yenu ya Ukongoroni na Charawe hapa hapa mmepata majibu ”,alisisitiza Waziri Said.

Hivyo, aliwasisitiza vijana kuheshimu Serikali yao ya Mapinduzi ya Zanzibar pamoja na kuheshimu Mapinduzi Matukufu ya Januari 12, 1964 kwa ajili ya kulinda na kujenga utu wao kama Wazanzibari.  

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.