STATE
HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF
THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar
24.08.2017
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa
Baraza la Mapinduzi, Dk Ali Mohamed Shein, ametoa muda wa Miezi sita kwa Wizara
ya Elimu na Mafunzo ya Amali kuhakikisha inapeleka vifaa vya maabara katika
skuli ya Sekondari na Msingi Chokocho, ili wanafunzi wapate kujifunza kwa
vitendo masomo yao ya Sayansi.
Dk Shein alisema ili wanafunzi
waweze kusoma vizuri na kufahamu masomo ya sayansi, lazima maabara ya skuli
hiyo iwekewe vifaa vya maabara, ili wanafunzi waweze kusoma kwa vitendo kwani
haiwezekani kusomesha sayansi kwa nadharia.
Kauli hiyo alitoa mara baada ya
kulifungua jengo la skuli hiyo ya Chokocho iliyopo Wilaya ya Mkoani, Mkoa wa
Kusini Pemba lililojengwa kwa nguvu za wananchi na Serikali ya Mapinduzi ya
Zanzibar kupitia Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali kumalizia ujenzi wake
ambapo miongoni mwa changamoto iliopo ni ukosefu wa vifaa vya maabara.
“Huwezi kusomesha wanafunzi wa
masomo ya sayansi bila ya kuwemo kwa vifaa katika maabara, wanafunzi watasoma
vipi masomo hayo, ili kuwa na wataalumu lazima masomo ya vitendo yawepo kwa
kiasi kikubwa”,alisema Dk. Shein.
Aidha, Dk. Shein aliwaagiza Wakuu
wa Mikoa na Wilaya pamoja na Wakaguzi wa Wizara wa Elimu kuhakikisha wanapita
katika skuli, kufuatia mahudhurio ya walimu na wakibaini kuwepo kwa mwalimu
mtoro wamchukulia hatua za kisheria.
“Tunafuatilia wenyewe maana
wasimamizi wanatuangusha na wale walimu ambao hawawajibiki watafukuzwa kazi kwa
mujibu wa Sheria na taratibu zilizopo”,alisema Dk. Shein.
Alisema kuwa kuna baadhi ya walimu
wamekuwa watoro, wengine huchukuwa likizo bila malipo na kufanya shuhuli zao
huku bado wanachukua mishahara, jambo ambalo ni kosa na kupelekea uwepo wa
wafanyakazi hewa hasa katika Wizara hiyo ya Elimu.
“Mwalimu yotote atakae bainika
kutokuwajibika ipasavyo, mtoleeni taarifa ili achukuliwe hatua kali za
kisheria, wapo walimu wengi wanataka ajira sasa wewe umeajiriwa hutekelezi
wajibu wako”aliongeza Dk. Shein.
Hata hivyo, aliwataka wazee
kuwashajihisha watoto wao kusoma, masomo ya sanyani, kushirikiana na walimu na
kuwataka baadhi ya walimu wanaochanganya siasa na elimu kuachana na jambo hilo.
Aliwataka wanafunzi kutambua kuwa
Chokocho, Michenzani, Kisiwa Panza itajengwa na wananchi wenyewe baada ya
kupata elimu hiyo.
Waziri wa Elimu na Manzo ya Amali, Riziki Pembe Juma, alisema kuwa
changamoto za vifaa vya sayansi bado zipo na kuahidi kuwa Wizara yake itazitatua
pamoja na uhaba wa walimu.
Katibu mkuu wa Wizara hiyo Khadija
Bakari, alisema jengo hilo lenye vyumba vinne na maabara, limejengwa kwa nguvu
za wananchi viongozi wa serikali pamoja na Serikali ambapo limegharimu zaidi ya
Milioni 96, nguvu za wananchi ni Milioni Milioni 21.
Akiwa katika Kituo cha KMKM, mara baada ya kukiweka jiwe la
msingi, Dk. Shein alisema kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imeamua
kujenga vituo sita vya uokozi Unguja na Pemba, ili kujilinda na majanga
yanayotokea baharini.
Alisema matukio makubwa mawili yametokea, ikiwemo kuzama kwa meli
ya MV Spice Islander na MV Skagit na kupoteza maisha ya watu, hali iliyopelekea
kuundwa kwa sheria inayokataza uingizwaji wa meli Zanzibar iliyozidi miaka
15.
"Meli zinazoingizwa nchini ziwe mpya au chini ya miaka 14,
hata MV Maendeleo tumeizuwia baada ya kuona umri wake umekuwa mkubwa, bahari
haina fundi wala mwenyewe na ndio maana serikali ikajenga vituo hivi vya uokozi
Unguja na Pemba"alisema.
Aidha, aliwaeleza wananchi kuwa, vifaa vya kisasa vilivyowekwa katika
kituo cha uokozi Nungwi, vitasaidia kutambua chombo chochote kitakachopata
hitilafu kitaonekana moja kwa moja na kuwataka wananchi kukubali mafunzo ya
ukozi yatakayotolewa na kikosi cha KMKM yakiwemo kuogolea, ili kuokoa maisha
yao yanapotokea majanga.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais,
Tawala za Mikoa, Serikali za Mitaa na Idara maalumu za Smz, Haji Omar Kheir
alisema kituo cha KMKM Mkoani kitawekewa vifaa vya kisasa vya uokozi kama
ilivyo vituo vya Unguja kwani tayari vifaa hivyo vimeshawasili.
Nae Katibu Mkuu Wizara ya Nchi
Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa, Serikali za Mitaa na Idara Maalum za SMZ Radhia
Rashid alisema kuwa kituo hicho ni miongoni mwa vituo sita vya uokozi
vinavyojengwa Unguja na Pemba ambacho kimeanza ujenzi wake 2016 na kinatarajiwa
kukamilika Disemba mwaka huu.
Alisema kuwa kitakapokamilika tu
kitaanza kutoa huduma kwani tayari vifaa vyake vyote vipo huku akieleza kuwa
tayari baadhi ya wananchi wakiwemo wavuvi wameshaanza kukitumia kituo cha
uokozi cha Nungwi ambacho Dk. Shein alikiwekea jiwe la msingi tarehe 13 mwezi
huu.
Akizungumza baada ya uwekaji wa jiwe la msingi, Tawi la CCM
Milimuni Chokocho, DK. Shein amewataka wanaCCM kuendelea kukiimarisha chama
chao na kuishi kwa kupendana, kuwa wamoja na washirikiane na sio watengenezeane
majungu baina yao.
Alisema katika Ilani ya CCM hakuna kitu fitna wala majungu, hivyo
wanachama wanapaswa kuhakikisha wanashirikiana na kushikamana, kwa ajili ya
maslahi ya CCM na kuhakikisha Serekali yao inarudi tena madarakani mnamo mwaka 2020.
Alifahamisha kuwa kazi kubwa ya chama, iko Matawini kwani ndiko
kwenye wanachama wa CCM, hivyo aliwataka viongozi kutambua kuwa wana kazi kubwa
ya kukiimarisha chama hicho kupitia Matawini, Wadi hadi kwenye Jimbo.
Hata hivyo, DK. Shein aliahidi kuchangia Milioni 10, kwenye jengo
hilo ambalo kwa sasa limeshagharimu TZS milioni 20 na zimebaki TZS milioni 16 na makadirio ni kugharimu
TZS milioni 36 hadi kukamilika kwake ambapo viongozi wa chama hicho na Serikali
walichangia hapo hapo zaidi ya TZS milioni 7.
Mapema asubihi Dk. Shein akipokea taarifa ya utekelezaji kwa Mkoa
wa Kusini Pemba, aliwataka mawaziri wa wizara zote za Serikali na taasisi zake,
kukaa vikao na kujitathmini Juu ya utendaji wao wa shuhuli zao, baaada ya
kumaliza ziara yake.
Alisema baada ya kufanya hivyo watajuwa wapi taasisi zao
hazikuweza kufikia malengo, kutokana na mipango kazi walioipanga ikiwa ni
utekelezaji wa Ilani ya CCM.
Mkuu wa Mkoa wa Kusini Pemba,
Mwanajuma Majid Abdalla akitoa taarifa ya Mkoa huo alisema Mkoa wake bado Ukoa
salama na umeweza kutekeleza vyema Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2015-2020 kwa
kiasi kikubwa.
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment