Habari za Punde

Rais Magufuli amekata Kiu



Napenda kuungana na Mamilioni ya Watanzania kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. John Pombe Joseph Magufuli kwa kufanya mabadiliko madogo mapya kwenye Baraza jipya la Mawaziri alilolitangaza Jumamosi Oktoba 7, 2017 Ikulu jijini Dar es Salaam.



Katika Baraza hilo jipya limeongezeka Wizara mbili mpya ambazo ni Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi imetenganishwa na kuwa Wizara ya Kilimo na  Wizara ya Mifugo na Uvuvi; na Wizara ya Nishati na Madini imetenganishwa na kuwa Wizara ya Nishati na Wizara ya Madini kufanya Wizara kuwa 21 toka 19 za awali.

Pia kuna ongezeko la Mawaziri 2 na Manaibu Waziri 5. Baadhi ya wapya walioongezeka ni Mhe. Abdallah Ulega, Mhe. Kangi Lugola, Mhe. Faustine Ndugulile, Mhe. Mary Mwanjelwa, Mhe. Juliana Shonza, Mhe. Kakunda n.k

Mabadiliko haya mapya madogo yamekuja wakati ambao Wizara mbalimbali zikiwa hazina Mawaziri na Manaibu Waziri na hivyo kuja kuzipa mapengo yaliyokuwa yakisababisha kusua sua kiutendaji. Baadhi ya Wizara hizo ni Wizara ya Tamisemi na Wizara ya Nishati na Madini.

Ukamilifu huu uliotokana na mabadiliko haya madogo umepeleka injini ya kuongoza nchi kukamilika na kuwa mpya na Watanzania tunatarajia maboresho makubwa ya utendaji kazi ya utekelezaji ilani ya uchaguzi kwa kasi ili kuharakisha upatikanaji wa maendeleo nchini.

Naendelea kumpongeza Rais Magufuli kwa kuteua Baraza lililokata kiu ya uteuzi kwa kuhakikisha kila kanda inapata uwakilishi, kuchanganya wakongwe na wapya, kuchanganya dini zote lakini Kubwa nina imani Baraza limejaa Watu weledi, wasomi wanaoendana na  nafasi walizopewa.

Katika mabadiliko haya Rais Magufuli ameendelea kuonyesha yeye ni kipenzi na Vijana kwa kuteua vijana wengi kwenye Baraza hili jipya la Mawaziri. Baadhi ya vijana waliopata fursa ya kuaminiwa ni Juliana Shonza, Abdallah Ulega, Dk. Faustine Ndugulile, Anthony Mavunde, Dk. Hamis Kigwangallah, Hamad Masauni, Mwigulu Nchemba, Mhe. Jafo, January Makamba na wengineo.

Vijana hawa wote walioteuliwa ni Watu weledi, makini na sahihi kabisa waliokuja kwa wakati sahihi. Kiukweli wametosha kabisa katika nafasi zao na watunze heshima ya asilimia 60 ya Vijana Watanzania na heshima ya Rais Magufuli aliyewaamini na kuwateua.

Rai yangu kwa Wateuliwa wote kwenda kufanya kazi kweli kweli ya kumsaidia Rais Magufuli kutekeleza ilani ya uchaguzi, kumsaidia kutimiza lengo la kuifanya nchi yetu kuwa Tanzania ya Viwanda yenye kufikia malengo ya uchumi wa kati na kwenda kutatua kero na shida za Watanzania.

Kama ambavyo Mhe. Rais Dk. John Pombe Magufuli alivyowaamini, hata nami nikiwa sehemu ya Watanzania nina imani Kubwa na Baraza hili jipya la Mawaziri. Wakafanye Kazi kweli kweli.

Hakika kimya kingi kina mshindo mkuu. Hongera sana Rais Dk. Magufuli kwa kusuka Baraza la Mawaziri linaloendelea kuleta imani na amani kwa Watanzania la Hapa kazi Tu!

Mungu Mbariki Rais Dk. Magufuli
Mungu Ibariki Tanzania.

IMETOLEWA NA:

Emmanuel J. Shilatu

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.